Sunday, March 20, 2016

TAMKO LA KULAANI KUTEKWA KWA MWANAHABARI BI SALMA SAID

TAMKO LA KULAANI KUTEKWA KWA MWANAHABARI BI SALMA SAID

Waziri kivuli wa Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo Mh Joseph Mbilinyi

Tanzania na dunia nzima inaelewa kuwa marudio ya uchaguzi wa Zanzibar ni batili. Na kwa kuwa uchaguzi huu ni batili, watawala yaani Chama cha Mapinduzi kimeingia katika historia ya kipekee duniani kwa kuwanyima haki wananchi wake.

Matukio mbalimbali yanayoendelea Zanzibar ikiwemo matumizi ya nguvu, vitisho na hata vitendo vya kikatili dhidi ya wanaosimamia haki, vinaendelea kuitia Serikali ya CCM doa si kwa taifa letu tupekee bali pia kwa dunia nzima.

Tukio la kutekwa kwa mwanahabari Bi Salma Said wa Deutsche Welle (DW) kimezua maswali makubwa lakini hofu kubwa kwa wananchi, familia yake na wadau hasa wanahabari wa ndani ya nchi na jumuia za kimataifa. Ni dhahiri kuwa kutekwa kwa Bi. Salma Said kunatokana na kazi yake ya uanahabari na ndio maana ushahidi wa awali ambao umepatikana kwa njia ya ujumbe wa sauti ukiwa na sauti inayoaminika kuwa ni yake, unaelezea wazi kutekwa kwake kunatokana na yeye kuripoti dosari zinazoendelea hasa katika uchaguzi batili wa marudio ya Zanzibar.

Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, inalaani kwa nguvu zote kitendo cha utekaji wa mwanahabari huyu kutokana na kazi yake. Aidha, tunaitaka Serikali kuhakikisha kuwa mama, dada, rafiki na ndugu yetu Bi Salma Said anapatikana akiwa salama.
Tunaendelea kuamini kuwa kuchelewa kupatikana kwa Bi Salma Said na ukimya wa vyombo vya Serikali na Usalama ni matokeo ya uminyaji wa demokrasia kwa wale wasiofanya kazi kwa mashinikizo ya Chama tawala.
Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, itaitisha maandamano makubwa nchini ili kushinikiza upatikanaji wa haraka wa Bi Salma Said lakini pia kupaza sauti kwa ulimwengu kuwa Tanzania si mahali salama kwa wanahabari.

Kwa niaba ya Kambi ya Upinzani Bungeni, tunaungana na watanzania wote hasa familia ya Bi Salma Said na watu wote wenye mapenzi mema kumuombea heri Bi Salma na kuamini kuwa atapatikana akiwa Salama Salmin na kuwatia hatiani watekaji wake.

Imetolewa na,
Joseph O. Mbilinyi (MB)
Waziri Kivuli wa Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo.
19/03/2016

No comments:

Post a Comment