Monday, June 10, 2019

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI NA UMMA KUHUSU UBORESHAJI WA DAFTARI LA KUDUMU LA WAPIGA KURA (DKWK)

Baada ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) pia kwa kushirikiana na vyama vingine washirika, kuibana mara kadhaa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kupitia njia mbalimbali kuitaka isiendelee kukiuka Katiba ya Nchi na Sheria ya Taifa ya Uchaguzi inayoweka utaratibu wa uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura (DKWK), hatimae tume hiyo imetoa ratiba ya zoezi la uboreshaji wa daftari hilo kwa nchi nzima, ikionesha kuwa itaanza kuandikisha mwaka huu kuanzia katika mikoa ya Kilimanjaro na Arusha na kumaliza mwaka kesho, Mkoa wa Dar es Salaam.

Tofauti na wito wa Chadema ulioitaka NEC kujitokeza hadharani na kutangaza ratiba hiyo kwa umma, tume imetoa ratiba hiyo ‘kimyakimya’ kwa kuiweka mojawapo ya viambatanisho kwenye barua iliyoandika kwa vyama vya siasa na wadau mbalimbali kuhusu maandalizi ya uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura.

Nakala ya ratiba hiyo kutoka NEC iliyoandikwa “Ratiba ya Zoezi la Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura 2019/2020”, inaonesha kuwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi itaanza shughuli hiyo tarehe 23 Juni, mwaka huu, katika mikoa ya Arusha na Kilimanjaro. Itazunguka katika maeneo mengine ya Tanzania (bara na visiwani) kabla ya kumaliza kazi hiyo Mkoa wa Dar es Salaam, kuanzia tarehe 8-27 Februari, mwaka 2020. Baada ya uboreshaji kufanyika nchi nzima, NEC itaweka wazi daftari hilo mnamo Machi 27 hadi Aprili 15, mwaka 2020.

Pamoja na NEC kutoa ratiba hiyo ndani ya muda mfupi kabla ya kuanza utekelezaji wake, jambo ambalo litawapatia usumbufu mkubwa wadau wengine wa mchakato huu nyeti kuelekea uchaguzi mkuu (vyama vya siasa, asasi za kiraia, waangalizi na watazamaji), ambao wanahitaji kufanya maandalizi muhimu na makubwa ya kushiriki kwa njia mbalimbali nchi nzima, ikiwemo kuhamasisha wananchi, kutoa elimu ya uraia, kutambua, kuandaa na kuweka mawakala wa kufuatilia zoezi hilo, katika hatua hii ya sasa, Chadema inasisitiza yafuatayo;

1.NEC itangaze ratiba yote ya shughuli hiyo ya uboreshaji wa DKWK kwa ukamilifu wake hadharani ili wananchi na wapiga kura ambao ndiyo wadau wakubwa katika mchakato huu, waielewe kisha wajiandae kushiriki kikamilifu kwenye hatua hii muhimu kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020.

2. Itoe maelezo ya kina ya ratiba kwa kwa maeneo yote ili wananchi waweze kutambua na kujipanga mahali watakapoenda kujiandikisha.

3. Itaje orodha ya vituo vitakavyotumika kuandikisha uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura, kwa sababu ratiba iliyotolewa haina kipengele hicho muhimu ambacho kitawasaidia wananchi wenye sifa za kuwa wapiga kura kujiandaa na kujua mahali wanapotakiwa kujiandikisha.

4. NEC itangaze hadharani ni lini mchakato wa ajira za muda kwa ajili ya kuajiri wasimamizi wa uboreshaji wa DKWK utafanyika tena baada ya kusimamishwa na tume hiyo hivi karibuni, ikiwa ni siku chache baada ya Chadema kutoa kauli ya kuitaka NEC iongeze muda wa shughuli hiyo kwa sababu muda uliotolewa na tume kwenye tangazo lake la Mei 30, mwaka huu (kuwasilisha maombi ya kazi hiyo mwisho uliwekwa kuwa ni kabla ya Juni 2, 2019), ulikuwa hautoshi. Suala hili la kuwapata Watanzania wenye sifa zinazotakiwa kufanya kazi hiyo ni muhimu, linalohitaji umakini na maandalizi ya kutosha kwa maana ya mafunzo.

5. Watanzania wote, walioko ndani na nje ya nchi, waliofikisha miaka 18 au wanaotarajia kufikisha umri huo mwaka kesho wakati wa kupiga kura, waanze kuhamasishana na kujiandaa kujitokeze kwa wingi kujiandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura. Halikadhalika tunatoa wito pia kwa wapiga kura wote walioandikishwa kupiga kura uchaguzi mkuu wa 2015, wajiandae kufika katika vituo hivyo kuhakiki taarifa zao. Aidha wote waliopoteza vitambulisho vyao na wale ambao vitambulisho vyao vimeharibika au wamehamia makazi katika maeneo hayo kufika katika vituo hivyo kwa ajili ya utaratibu wa kuandikishwa.

6. Kwa kutambua umuhimu na unyeti wa uandikishaji wapiga kura kuwa ni mojawapo ya hatua muhimu katika mchakato wa uchaguzi, hasa Taifa linapojiandaa na uchaguzi mkuu wa 2020, Chadema kimejipanga kushiriki na kufuatilia shughuli hiyo kwa ukaribu na umakini unaohitajika, ikiwemo utaratibu wa kuwa na mawakala katika vituo vyote vya kuandikisha wapiga kura kama taratibu zinavyoelekeza.

*Hitimisho*

Ni muhimu NEC itimize wajibu wake kwa mujibu wa Katiba na Sheria za Nchi ambazo zinaipatia mamlaka ya kusimamia jambo nyeti linaloamua hatma ya maisha ya mwananchi mmoja mmoja, makundi, jamii na hatimae taifa kwa ujumla. Tume itambue kuwa wadau mbalimbali wa uchaguzi, hususan wapiga kura, wanafuatilia kwa ukaribu umakini, uwezo na utayari wa NEC kusimamia uchaguzi nchini na kipekee Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020.

Imetolewa leo, Jumatatu Juni 10, 2019 na;

Tumaini Makene

Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano
CHADEMA

Saturday, June 8, 2019

HALIMA MDEE AFANYIWA UPASUAJI, AENDELEA VIZURI

Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama, Halima Mdee (Mb) anaendelea vyema na matibabu katika Hospitali ya Aga Khan baada ya kufanyiwa upasuaji siku ya Ijumaa, Juni 7, mwaka huu akiwa amelazwa hospitalini hapo tangu Alhamis, wiki hii.

Mhe. Mdee ambaye ni Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake (BAWACHA) Taifa na Mbunge wa Jimbo la Kawe, alilazimika kufanyiwa upasuaji baada ya kushauriwa na madaktari wake kwa ajili ya kutibu ugonjwa uliokuwa unamsumbua.

Baada ya upasuaji huo uliochukua takriban muda wa saa 4.30, Mhe. Mdee bado yuko chini ya uangalizi wa madaktari, akiendelea kuimarika na kupata nguvu, ambapo madaktari wameshauri apate muda wa kupumzika kabla hajaruhusiwa kutoka hospitalini hapo.

Imetolewa leo Jumamosi, Juni 8, 2019 na;

Tumaini Makene
Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano
CHADEMA

Thursday, May 16, 2019

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI NA UMMA

CHAMA CHA DEMOKRASIA NA MAENDELEO (CHADEMA)

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI NA UMMA

Kumekuwa na taarifa zinazosambaa katika njia mbalimbali za upashanaji habari mitandaoni na baadae kwenye vyombo vya habari tangu asubuhi ya leo kuhusu kile kinachoonekana kuwa ni sintofahamu kubwa inayoendelea katika Bunge la Afrika (PAP) ambako taarifa zimedai kuwa Rais wa PAP,  Roger Nkodo Dang anakabiliwa na tuhuma nzito ikiwa ni pamoja na matumizi mabaya ya madaraka, unyanyasaji wa kingono, upendeleo na unyanyasaji kwa wafanyakazi wa Ofisi za Makao Makuu ya Bunge hilo, nchini Afrika Kusini.

Taarifa hizo za maneno zilizokuwa zikisambaa  zilipewa nguvu na video fupi iliyorekodiwa ikimuonesha Makamu wa Rais wa PAP, Stepehen Maselle (ambaye ni mmoja wa wawakilishi wanne wa Tanzania katika PAP) akizungumza wakati akiongoza mojawapo ya vikao vya Bunge hilo vinavyoendelea nchini Afrika Kusini kwa sasa, ambapo amesikika (tafsiri yetu ya Kiswahili) akimlalamikia Rais wa PAP kuwa amemwandikia barua Spika wa Bunge la Tanzania ili amrejeshe Stephen Masele nchini (recalling) ili ikiwa ni namna ya Rais huyo kupambana kuzuia agenda au taarifa ya Kamati Maalum iliyoundwa kuchunguza tuhuma zake isisomwe, kujadiliwa au kufanyiwa kazi na Bunge hilo. Katika video hiyo Mbunge huyo amesikika akisema anayo ruhusa kutoka kwa Waziri Mkuu (Serikalini) hivyo hataondoka nchini Afrika Kusini kama ambavyo Rais huyo wa PAP anataka iwe, katikati ya mapambano yake ya kujisafisha na tuhuma hizo nzito zinazomkabili.

Kabla Watanzania hawajaelewa hasa kinachoendelea, kutokana na mkanganyiko huo ambao umeanza kushika kasi kwenye vyombo vya habari vya kitaifa na kimataifa, Spika wa Bunge Ndugu Job Ndugai ametoa taarifa ya Bunge akithibitisha maneno yaliyokuwa yakisambaa mitandaoni kuwa Bunge limemuagiza Stephen Maselle arejee nyumbani haraka kuja kujibu tuhuma za ukosefu wa maadili zinazomkabili mbele ya Kamati ya Bunge ya Maadili, Kinga na Madaraka ya Bunge pamoja na Kamati ya Maadili ya Chama chake.

Katikati ya mkanganyiko huu, CHADEMA inapenda kuweka msimamo wake wazi kuwa jina la nchi yetu Tanzania lisitumike vibaya wala kuwekewa taswira hasi na kuendelea kuharibu sura yetu kidiplomasia na katika mahusiano ya kimataifa.

Tunasema hivyo tukiwa na taarifa za uhakika kuwa PAP ililazimika kuunda Kamati Maalum kuchunguza tuhuma hizo nzito zinazomkabili Rais wake, Roger Nkodo Dang, za unyanyasi wa kingono kwa watumishi wa kike walioko Makao Makuu ya PAP (imedaiwa takriban wanawake 10 wamejitokeza mbele ya kamati kuthibitisha walivyonyanyaswa kingono bila ridhaa yao), matumizi mabaya ya madaraka, upendeleo ndani ya bunge hilo na unyanyasaji kwa watumishi wa ofisi hiyo hali iliyosababisha kuwepo kwa mgomo wa watumishi kwa takriban wiki nzima.

Taarifa tulizozipata kutoka ndani ya Bunge hilo zimedai kuwa Rais Roger Nkodo Dang anatumia njia mbalimbali kupambana kujisafisha na tuhuma hizo kwa sababu mbali ya kupoteza nafasi yake hiyo kwenye Bunge la PAP, iwapo zikithibitika kuwa ni kweli, pia zitamuondolea kinga za kidiplomasia alizonazo, huku ikijulikana wazi kuwa tuhuma hizo zinazomkabili ni mojawapo ya makosa makubwa ya kijinai yanayochukuliwa kwa uzito mkubwa nchini Afrika Kusini.

Katika mazingira hayo, kitendo cha Bunge kumrejesha nyumbani kwa haraka Makamu wa Rais wa PAP, Stephen Masele ambaye kiutaratibu ndiye aliyetakiwa kuongoza vikao vya Bunge hilo vinapojadili taarifa ya Kamati Maalum kuhusu tuhuma za Rais na kusimamia utekelezaji wa maazimio, inaibua shaka kubwa na kujenga taswira hasi kwa nchi yetu kuwa inatumika au inataka kutumika kumuokoa Rais Roger Nkodo Dang dhidi ya tuhuma hizo au haitaki kuonekana kuwa imesimamia na kuongoza taratibu zinazotakiwa katika suala linalomsibu na pengine kitakachofuatia. 

Hivyo basi ili kuiweka nchi yetu katika mahusiano mazuri ya kimataifa na kuendeleza sifa yetu iliyojengwa kwa miaka mingi huko nyuma kuwa Tanzania inasimamia misingi na taratibu na kuondoa kadhia itakayoijengea nchi yetu picha mbaya, si ndani ya nchi pekee bali kimataifa pia, tunalitaka Bunge (lililomrejesha nyumbani Stephen Masele) na Serikali ya Tanzania ambayo imedaiwa kumwagiza Stephen Masele aendelee kubaki huko hadi amalize majukumu yake, kutoa kauli ya msimamo wetu Tanzania kuhusu tuhuma zinazomkabili Rais wa PAP. Je ni kweli tunaunga mkono unyanyasaji wa kingono? Je tunaunga mkono matumizi mabaya ya madaraka ikiwemo rushwa? Je tunaunga mkono unyanyasaji? Je tunaunga mkono upendeleo katika taasisi hiyo ya kimataifa?

Ni msimamo huo pekee utaweza kuiokoa Tanzania katika jambo hilo ambalo limeanza kuchukua mkondo mbaya kuwa nchi yetu inatumika kulinda tuhuma za uhalifu wa kijinai.

Aidha, kwa sababu Spika wa Bunge ameshalizungumzia na kulitolea taarifa suala hilo hatua iliyomaliza utata wa iwapo taarifa zilizokuwa zikisambaa mitandaoni zilikuwa za kweli, tunalitaka Bunge kuweka wazi tuhuma zinazomkabili Mbunge Stephen Masele zilizosababisha arejeshwe nchini na uwakilishi wake (wa nchi) katika taasisi hiyo ya kimataifa kusitishwa.

Halikadhalika, CHADEMA inaitaka mihimili ya Serikali na Bunge kutoka hadharani na kutoa kauli kuueleza umma juu ya madai kuwa kuna hali ya mgongano wa kauli, misimamo na maamuzi baina ya mihimili hiyo miwili juu ya suala hilo, kiasi ambacho kimeanza kuleta athari katika uwakilishi wa nchi yetu kwenye PAP. Kauli ya mihimili hiyo itawasaidia wawakilishi watatu wa Tanzania waliosalia kwenye PAP kujua misingi ya hoja zao na masuala wanayotakiwa kusimamia katika mtanziko huu uliopo.

Imetolewa leo Alhamis, Mei 16, 2019 na;

Tumaini Makene
Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano
Chadema

Tuesday, May 14, 2019

BAADA YA HUKUMU YA MAHAKAMA KUU, MASUALA SABA YA MUHIMU; UCHAGUZI HURU NA HAKI NCHINI


CHAMA CHA DEMOKRASIA NA MAENDELEO (CHADEMA)

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI NA UMMA
                                  
 KUHUSU

BAADA YA HUKUMU YA MAHAKAMA KUU, MASUALA SABA YA MUHIMU; UCHAGUZI HURU NA HAKI NCHINI

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimepanua wigo wa mjadala wa uhitaji wa taasisi na mifumo itakayohakikisha nchi inafanya chaguzi huru na haki kwa kuitaka Serikali kufanyia kazi masuala 7 muhimu, wakati huu inapojiandaa kutekeleza amri ya Mahakama Kuu ya Tanzania ambayo imefuta vifungu 7(1) na 7(3), vya Sheria ya Taifa ya Uchaguzi namba 5 ya mwaka 1985, vilivyokuwa vikiwapatia mamlaka wakurugenzi wa halmashauri nchini kusimamia uchaguzi.

Aidha, CHADEMA kimetoa rai kwa wadau mbalimbali wa demokrasia na utawala bora ndani na nje ya nchi kupigania na kusaidia kwa kila njia inayowezekana kutekelezwa kwa masuala hayo 7, kwa sababu mfumo wa uchaguzi huru na haki ni mojawapo ya sifa kuu za demokrasia duniani zinazodhihirisha mamlaka ya wananchi katika kuamua namna wanavyotaka kujitawala na kuongozwa.

Pia, taasisi imara na mifumo thabiti ya chaguzi huru na haki, inaondoa uwezekano wa nchi kutumbukia katika machafuko kutokana na kutoridhishwa na mwenendo wa mchakato wa uchaguzi huku pia ikidhibiti mianya ya kuchaguliwa na kuwekwa madarakani mamlaka za kidikteta zenye kujali na kusimamia maslahi ya wachache badala ya maslahi ya taifa na matakwa ya wananchi.

 Akizungumza katika mkutano wa waandishi wa habari uliofanyika leo Makao Makuu ya CHADEMA, jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Uenezi, Itikadi, Mawasiliano na Mambo ya Nje, John Mrema ameyataja masuala hayo 7 ambayo CHADEMA kinaamini ni sehemu muhimu ya mjadala wa muda mrefu nchini kuhusu hitaji la chaguzi huru na za haki, kuwa ni pamoja na;

1.     Tume Huru ya Uchaguzi (Tanzania Independent Electoral Commission-TIEC)

2.     Matokeo ya uchaguzi wa rais kupingwa mahakamani

3.     Haki ya mgombea kukata rufaa (na kupata haki yake ya kugombea) anapokuwa amenyimwa fomu, fomu zake kukataliwa kupokelewa au kutoteuliwa na Msimamizi wa Uchaguzi.

4. Mfumo usiruhusu mgombea kupita bila (kupingwa) kupigiwa kura.

5. Mfuko Maalum wa Fedha kwa ajili ya kuendesha shughuli za TIEC kusimamia uchaguzi.

6. Maamuzi ya Tume Huru ya Uchaguzi kuweza kupingwa mahakamani.

7. Kuwepo kwa mgombea binafsi.

CHADEMA inaweka bayana kuwa mapendekezo hayo ni kwa ajili ya maslahi ya nchi hasa Watanzania wanapojiandaa kuelekea kwenye chaguzi mbili muhimu, Uchaguzi wa Serikali za Mitaa (2019) na Uchaguzi Mkuu (Rais, Wabunge na Madiwani-2020), ambapo wapiga kura wanahitaji kuhakikishiwa kuwa karatasi za kura sio tu ziko salama, bali hazitaangaliwa kama karatasi zingine za kawaida.

"CHADEMA tunapendekeza iundwe Tume Huru ya Uchaguzi kwa maana ya TIEC, Tanzania Independent Electoral Commission) ambayo itawekewa utaratibu mpya wa uteuzi kuwapata wajumbe wake, mathalani katika nchi za Kenya, South Africa, Malawi au Ghana watu hao wanapatikana kwa kutuma maombi ya kazi na kufanyiwa vetting (uchambuzi) na mamlaka husika kabla ya uteuzi. Uteuzi uwe huru usiwe chini ya mtu mmoja ambaye naye anakuwa na maslahi binafsi au ya chama chake wakati wa uchaguzi. Tunataka wajumbe wa Tume wawe na uhakika wa usalama wanapotimiza majukumu yao. Muhula wao kazini ujulikane na ulindwe. Masharti yao ya kazi yajulikane. Mnakumbuka wakati wa uchaguzi mkuu uliopita, kuna watumishi waliondolewa kazini katikati ya uchaguzi kinyume cha utaratibu."

"Tunataka TIEC hiyo iwe na mfuko wake maalum kwa ajili ya kuendeshea shughuli zake badala ya kupiga magoti kuombaomba Serikali Kuu. Hii inapunguza uhuru wa Tume kwa sababu inaomba fedha kwa watu ambao inatakiwa kuwasimamia. Mfano mzuri ni huu wa sasa ambapo Tume ya Uchaguzi haijaandikisha daftari la wapiga kura, kinyume na maelekezo ya kisheria ambayo yanataka daftari liandikwe mara mbili. Hii ni kwa sababu tume haina mfuko wake wa fedha zake yenyewe, inasubiri hadi ipewe," amesema Mrema.

Aidha, CHADEMA inasisitiza kuwa hakuna haja ya kuendelea kuwepo na zuio la kutoruhusu maamuzi ya Tume ya Uchaguzi kuhojiwa mahakamani, kwa sababu iwapo makamishna na watendaji wa Tume watajua kuwa tume inaweza kushtakiwa na kuhojiwa mahakamani watafanya maamuzi yao kwa kuzingatia haki ili wasifikishwe mahakamani. "Lakini pia kama tume ni huru kunakuwa na hofu gani ya kuzuia maamuzi yake kuhojiwa mahakamani? Maana yake basi hiyo tume isiyohojiwa mahakamani haiko huru."

Huku ikitambua na kuunga mkono juhudi ambazo zimechukuliwa tayari na wadau wengine kwa kufungua kesi Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu, ambayo tayari imesajiliwa kwa namba 018/2018, kwa ajili ya kupinga Ibara ya 41(7) inayozuia kuchunguza au kuhoji matokeo ya uchaguzi Mahakamani, kwa sababu ibara hiyo inakiuka Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu, CHADEMA inaweka bayana kuwa ibara hiyo inapaswa kuondolewa ili mtu yeyote awe na haki ya kuhoji matokeo ya uchaguzi huo iwapo na ushahidi kuwa ulikuwa na makosa, kama inavyoruhusiwa kupinga mahakamani matokeo ya uchaguzi wa Wabunge na Madiwani.

Kuhusu uwepo wa vifungu vya Sheria ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, kifungu cha 45(2) na kifungu cha 44 cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, vinavyoruhusu mgombea kupita bila kupingwa ikitokea ameteuliwa peke yake, CHADEMA inapendekeza kuwa ikitokea mazingira (yasiyokiuka sheria) kuwa mgombea ameteuliwa peke yake, asihesabiwe au asitangazwe kuwa ameshinda kwa kupita kupingwa bali wananchi wapate fursa na kutumia haki yao kwa kumpigia kura ya NDIYO au HAPANA. Mbali ya kuwapatia wananchi haki hiyo na kuona iwapo mgombea anaungwa mkono na wananchi, pia itaondoa uwezekano wa wagombea wengine kuenguliwa kwa hila kwa kunyimwa fomu, fomu zao kukataliwa au kutopokelewa au kutoteuliwa kwa makusudi, ili kumsaidia mgombea fulani apite bila kupingwa kama ambavyo imetokea katika chaguzi kadhaa hivi karibuni.

CHADEMA pia inataka kuwepo kwa mfumo wa kisheria utakaohakikisha utekelezwaji wa Ibara ya 21 ya Katiba ya Nchi, ili kuondokana na vikwazo wanavyowekewa baadhi ya wagombea wa nafasi mbalimbali hasa wa vyama vya upinzani ambao wamekuwa ama wakinyimwa fomu za kugombea, fomu zao kutopokelewa (wasimamizi kukataa au kujificha) au kuenguliwa wakati wa uteuzi huku haki yao ya kugombea ikiishia hapo, bila kuwa na haki ya kukataa rufaa, kama ilivyotokea wakati wa uchaguzi wa marudio Jimbo la Korogwe vijijini mwaka jana. 

Katika hali ya kupinga ukiukwaji huo wa Katiba na haki za binadamu, aliyekuwa mgombea wa CHADEMA katika uchaguzi huo wa marudio Korogwe Vijijini, Bi. Aminata Suguti amefungua shauri Mahakama Kuu Kanda ya Tanga, kesi namba 7/2019 iliyoko mbele ya Jaji Mruma, tayari imetajwa mnamo tarehe 30 Aprili, mwaka huu na itaanza kusikilizwa Juni 4, mwaka huu. Upande wa mpeleka maombi unaiomba Mahakama kutoa amri kuwa iwapo mgombea hajateuliwa na msimamizi wa uchaguzi kwa sababu fomu zake hazikupokelewa, awe na haki ya kukata rufaa. Mahakama pia, iwe na mamlaka ya kumtangaza mgombea wa namna hiyo kuwa ni mgombea halali wa uchaguzi almuradi awe amepitia mchakato wa ndani wa chama chake.

Pia, CHADEMA imesema kuwa ni wakati mwafaka sasa kuwepo na Sheria inayoruhusu mgombea binafsi ili kutekeleza Katiba ya nchi, jambo ambalo pia litasaidia makundi mbalimbali katika jamii, ambayo hayahitaji kufungamana na itikadi za vyama vya siasa, kuwa na uwakilishi katika vyombo vya maamuzi. 

CHADEMA imetoa wito kwa Serikali pamoja na Chama kilichoko madarakani kutokuwa na hofu ya kuweka mazingira yanayoweka misingi ya taasisi na mifumo imara kwa ajili ya chaguzi huru na haki, kwa sababu kama chama au serikali iliyoko madarakani imefanya kazi kama inavyotakiwa itachaguliwa katika mazingira hayo na itakuwa na uhalali zaidi wa kuongoza wananchi badala ya mfumo wa sasa ambao unatia walakini chaguzi zinazofanyika nchini, hivyo viongozi wengi wanaochaguliwa wanakuwa na uhalali wa kisheria lakini si uhalali wa kisiasa (kukubalika au kuungwa mkono na watu).

Imetolewa leo Jumapili, Mei 12, 2019 na;

Tumaini Makene
Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano
CHADEMA