Friday, December 18, 2015

TAARIFA YA JOHN MNYIKA KUHUSU KUTORIDHISHWA NA HATUA ZILIZOCHUKULIWA NA WAZIRI WA MAJI


TAARIFA KWA UMMA

Sijaridhishwa na hatua zilizochukuliwa na Waziri wa Maji alipofanya ziara juzi na kunukuliwa na vyombo vya habari jana. Hivyo, naomba Waziri Mkuu achukue hatua zifuatazo:

Mosi, atake Wizara ya Maji impatie nakala ya ripoti ya uchunguzi kuhusu kukatikakatika mara kwa mara kwa maji katika mitambo na maeneo ambayo yanahudumiwa na mitambo ya Ruvu juu. Baada ya kupata ripoti hiyo atembelee katika DAWASA/DAWASCO na ‘kutumbua majibu’ ya ufisadi na udhaifu uliopo.

Pili, atembelee ujenzi unaoendelea kwenye chanzo cha Ruvu juu ambao ulipaswa kukamilika toka 2013 lakini haijawa hivyo, na katika mkutano wa mwisho wa Bunge la Kumi Wizara ya Maji iliahidi ungekamilika Agosti 2015 na haijawa hivyo pia.

Tatu, atembelee eneo la ulazaji wa Bomba kubwa jipya kutoka Mlandizi mpaka Kimara na ujenzi wa matenki mapya ambao ulipaswa kukamilika 2013, lakini haijawa hivyo, na katika mkutano wa mwisho wa Bunge la Kumi Wizara ya Maji iliahidi ungekamilika Septemba 2015 na haijawa hivyo pia.

Nne, ulazaji wa mabomba ya kusambaza maji katika maeneo yasiyokuwa na “mabomba ya mchina” katika kata za Kibamba, Kwembe, Mbezi, Msigani, Saranga, Goba haujaanza kabisa. Naomba ufuatilie mchakato wake wa mkataba na vyanzo vyake vya rasilimali ili kazi hiyo ianze sanjari na bomba kuu linalolazwa ili yakamilike kwa pamoja wananchi wapate maji.

Achukue hatua zingine za ziada kwa kurejea hoja binafsi niliyoiwasilisha Bungeni tarehe 4 Februari 2013 (nimeambatanisha nakala) ambayo maelezo yake na mapendekezo yake bado ni muhimu yakafanyiwa kazi.


John Mnyika

Mbunge wa Kibamba

16/12/2015





HOJA BINAFSI YA JOHN MNYIKA KUHUSU SUALA LA MAJI



MABADILIKO KATIKA HOJA  KUHUSU HATUA ZA HARAKA ZA KUBORESHA UPATIKANAJI WA MAJI SAFI NA USHUGHULIKIAJI WA MAJI TAKA KATIKA JIJI LA DAR ES SALAAM
(Kwa mujibu wa Kanuni 55 (10) ya  Kanuni za Kudumu za Bunge)
Kwa kuingiza maneno:
“KWA KUWA, Programu ya Maji Safi na Mazingira Vijijini ikiwemo katika Manispaa za Jiji la Dar es Salaam ilipaswa kutekelezwa kuanzia mwaka 2005/2006 na kukamilika mwaka 2010/2011 kwa kugharimu dola za kimarekani milioni 292 hata hivyo tathmini ya miaka miwili na nusu ya utekelezaji (mid term review) imebanisha kasoro nyingi katika utekelezaji.
KWA KUWA, Kati ya mwaka 2003 mpaka 2010 Serikali ilitekeleza Mradi wa ukarabati na upanuzi wa miundombinu ya Majisafi na Majitaka Jijini Dar es salaam na maeneo ya Bagamoyo na Kibaha (Dar es salaam Water Supply and Sanitation Project-DWSSP) uliotumia dola milioni 164.6 hata hivyo mpaka sasa katika maeneo mengi mtandao wake maarufu kama mabomba ya wachina hautoi maji huku kukiwa na upungufu katika uzalishaji, upotevu wakati wa usafirishaji, udhaifu katika usambazaji na tuhuma za ufisadi katika matumizi.
NA KWA KUWA, Wizara ya Maji iliandaa waraka maalum wa kuiomba Serikali kutenga kiasi cha shilingi bilioni 653.85 Mpango Maalum 2011-2013 wa kuboresha huduma za majisafi na uondaji wa majitaka katika Jiji la Dar es salaam na kupitishwa na Baraza la Mawaziri mwezi Machi 2011 lakini utekelezaji wake unaelekea kucheleweshwa mpaka mwaka 2016.
NA KWA KUWA , katika mwaka wa fedha 2011/2012 na 2012/13 Serikali haikutenga kiwango kamili cha fedha kwa kuzingatia Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano ulioidhinishwa na Bunge na kwa kuzingatia mgawanyo wa Mpango Maalum wa Maji Safi na Maji Taka katika Jiji la Dar Es Salaam na kauli ya Serikali ya tarehe 7 Novemba 2012.
NA KWA KUWA, kwa mujibu wa ibara ya 62 (2)  na (3) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 , Bunge ndicho chombo kikuu chenye madaraka, kwa niaba ya wananchi, kuisimamia na kuishauri Serikali na vyombo vyake vyote katika utekelezaji wa majukumu.
NA KWA KUWA, kwa mujibu wa ibara ya 63(3) katika utekelezaji wa madaraka yake bunge laweza kujadili na kuidhinisha mpango wowote wa muda mrefu au wa muda mfupi unaokusudiwa kutekelezwa katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kutunga sheria pale utekelezaji unapohitaji kuwapo sheria.
NA KWA KUWA, Malengo ya Kitaifa yalikuwa ni kuwapatia wakazi wa Mjini maji kwa asilimia 90 ifikapo mwaka 2010 na kwamba malengo hayo kwa Jiji la Dar es Salaam yamesogezwa mbele na kuwekwa malengo mapya ya upatikanaji wa huduma ya maji safi kufikia asilimia 90 na uondoaji wa maji taka kufikia asilimia 30 ifikapo mwaka 2015.
KWA HIYO BASI, Bunge linaazimia kwamba Serikali ichukue hatua za haraka zaidi za kuboresha upatikanaji wa maji safi na ushughulikiaji wa maji taka katika Jiji la Dar es salaam:
NA KWAMBA, Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) afanye ukaguzi  maalum wa matumuzi ya fedha matumizi ya bilioni 96.4 za mradi wa maji safi na mazingira vijijini katika Jiji la Dar es salaam na Halmashauri zingine na kuwezesha hatua za ziada kuchukuliwa.
NA KWAMBA, Kufuatia kauli iliyotolewa bungeni tarehe 7 Novemba 2012 kuhusu Mpango Maalum wa kutatua tatizo la maji katika Jiji la Dar es salaam uliopitishwa mwezi Machi 2011 Serikali izingatie makisio ya awali ya gharama za mpango huo na kuingiza mahitaji yaliyobaki kwenye Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Mwaka 2013/2014 na Bajeti ya mwaka 2013/2014.
NA KWAMBA, Mpango wa dharura wa kupunguza kero ya maji ulionza kutekelezwa na Wizara ya Maji kwa kushirikiana na DAWASA kuanzia Juni 2010 unaohusisha uchimbaji wa visima 29 uliopaswa kukamilika Oktoba 2011 uwekewe muda wa ukomo wa kukamilika kwa dharura katika maeneo ambayo miradi haijakamilika mpaka hivi sasa ikiwemo iliyozinduliwa Oktoba 2012 yenye kuhitaji miundombinu ya ziada kufikia wananchi zaidi.
NA KWAMBA, Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) afanye ukaguzi wa thamani ukilinganisha na ufanisi (Value for Money) wa Mradi wa ukarabati na upanuzi wa miundombinu ya Majisafi na Majitaka Jijini Dar es salaam na maeneo ya Bagamoyo na Kibaha (Dar es salaam Water Supply and Sanitation Project-DWSSP) kwa kurejea ukaguzi wa kiufundi (technical Audit) uliofanywa na kampuni ya Howard Humphreys.
NA KWAMBA, EWURA ifanye ukaguzi wa kiufanisi (performance audit) wa miradi ya visima vya maji takribani 200 ambavyo vilichimbwa na serikali na kukabidhiwa kwa DAWASCO, jumuiya za wananchi na taasisi mbalimbali lakini haitoi huduma inavyostahili kwa kadiri ya malengo ya awali.
NA KWAMBA, EWURA iharakishe kukamilisha mchakato ulioanza wa kutunga kanuni za udhibiti wa ubora na bei ya huduma ya maji kwa upande wa sekta binafsi katika Jiji la Dar es salaam.
NA KWAMBA, Kamati husika ya Bunge ijadili taarifa ya ukaguzi wa ufanisi kuhusu usimamizi wa usambazaji wa maji katika maeneo ya mijini (performance audit report on the management of water distribution in urban areas) ya Januari 2012 ili maoni na mapendekezo yazingatiwe wakati wa kujadili na kushauri kuhusu mapendekezo ya mpango wa taifa na bajeti ya nchi.
NA KWAMBA, Serikali iwasilishe bungeni haraka iwezekanavyo muswada wa sheria ya marekebisho ya sheria mbalimbali za majisafi na majitaka (Water Supply and Sanitation Miscellaneous Amendment Bill) ili kushughulikia upungufu uliojitokeza katika utekelezaji wa sheria zilizopo na kuweka mfumo thabiti wa usimamizi wa sekta ya maji nchini.”
Naomba kuwasilisha.
…………………
John John Mnyika(Mb)
Jimbo la Uchaguzi-Ubungo
04/02/2013

No comments:

Post a Comment