Sunday, December 20, 2015

Lowassa afurahia tuzo

Aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya CHADEMA na kuungwa mkono na vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) ameishutumu serikali kwa kuwakataza kufanya mikutano ya kuwashukuru wananchi na ameifananisha hatua hiyo sawa na uoga usio na msingi.

Akizungumza kupitia taarifa iliyotolewa na msemaji wake, Aboubakary Liongo, Lowassa alisema kuzuiwa kwake na upinzani kuzunguka nchi nzima kuwashukuru wapiga kura ni uoga wa CCM na serikali yake kwa kisingizio cha vurugu.

Lowassa amerusha makombora hayo wakati akishukuru tuzo ya amani duniani anayotarajiwa kupewa na taasisi 1,200 duniani kutokana na utulivu aliouonyesha kabla na baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu.

Aliitaka serikali kuacha mabavu na uonevu na badala yake ijenge nchi kwa kuheshimu Demokrasia na haki za binaadamu huku akisisitiza kwamba tuzo aliyopewa na taasisi hizo za dini ni uthibitisho wa kutosha kwa uongo wa CCM na serikali yake kuwa wapinzani ni watu wa vurugu.

"Wamekuwa wakitumia mabavu kutugandamiza kwa kisingizio cha kuwa sisi ni watu wa vurugu..angalia kule Mwanza wakati wa mazishi ya Mawazo jinsi walivyotumia mabavu kuyazuia..ujinga mtupu" alisema Lowassa.

Alisema yeye ni muungwana na ana hofu ya Mungu,hata siku moja hataweka mbele maslahi binafsi na ndiyo maana aliwatuliza wananchi waliokuwa wakimtaka kutoa tamko baada ya matokeo kutangazwa.

"Baada ya kuona jinsi walivyoporwa ushindi wao wananchi na baadhi ya viongozi wazito tu..walinitaka nitoe tamko la kutaka nguvu ya umma itumike kudai ushindi wao,lakini nilikataa sikuwa tayari kuona Watanzania wakipoteza maisha..siko tayari kuingia Ikulu huku mikono yangu ikibubujika damu,nashukuru taasisi hizo za kidini duniani, zimeliona hilo," alisisitiza Lowassa ambaye alikataa kuyatambua matokeo.

Alisema anapokea kwa unyenyekevu na furaha tuzo ya amani duniani anayotarajiwa kupewa na taasisi za kidini hizo.

Taasisi hizo katika Kikao chake huko Bukavu DR Congo, zilitangaza kumpa tuzo hiyo Edward Lowassa kutokana na utulivu aliyounesha kabla na baada ya uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu.

Taarifa ya Mwenyekiti wa kamati ya maadili, Amani na haki za binadamu kwa jamii Mchungaji, William Mwamalanga, ilisema kiasi wajumbe 1,400 wa mkutano huo kutoka kote duniani walikubaliana kumpa tuzo hiyo Lowassa kati ya wanasiasa 1,000 walioshindanishwa ili kumpata kiongozi bora wa amani mwaka 2015 ambaye anajali na kuangalia maslahi ya jamii badala ya madaraka.


Nipashe

No comments:

Post a Comment