Sunday, December 20, 2015

Kauli ya Mbowe baada ya MCC kuzuia Trilioni 1 kwa serikali ya Tanzania

Muda mfupi baada ya Bodi ya MCC kutoa taarifa inayoonesha Tanzania haitapata msaada kutoka shirika hilo kama ilivyotarajiwa kwa ajili ya mwaka 2016, Mwenyekiti wa Chama Chadema, Freema Mbowe ametoa kauli nzito juu ya suala hilo akisema kuwa kuchelewa kupatikana kwa fedha za MCC si tu kunachafua jina la nchi na hadhi yake katika medani za kimataifa, bali kutaathiri kwa kiasi kikubwa miradi yote iliyo chini ya ufadhili wa MCC.

MCC imeahirisha msada huo wa USD Mil. 472.8 ambazo ni takriban trilioni moja kwa fedha za Tanzania zilizolengwa kusaidia sekta ya nishati ya umeme hususan ule wa vijijini, katika kuunganisha wateja wapya, mabadiliko ya kimuundo ya Shirika la Umeme nchini (TANESCO) ili lifanye kazi na kutoa huduma kwa ufanisi katika sehemu za uzalishaji, usafirishaji na usambazaji.

Fedha hizo pia zilikusudiwa kusaidia kuanza kwa mpango mkubwa wa kuboresha sekta ya umeme nchini.2014-2024.

Mbowe amemtaka Rais John Magufuli kuchukua hatua za haraka za kiuongozi kumaliza mtanziko wa kisiasa Zanzibar kwa mshindi wa nafasi ya urais kutangazwa kutokana na uchaguzi uliofanyika mwezi Oktoba, mwaka huu.

Aidha amesema kuwa Sheria ya makosa ya mtandao (Cyber Crime Act 2015) ambayo ni mojawapo ya sababu zilizotumiwa na MCC kuahirisha msaada huo kwa Tanzania hadi itakapokuwa imefanyiwa kazi, ni sheria mbaya sana inayokinzana na kukua kwa technologia ya habari na mawasiliano na kuzuia upashanaji wa habari miongoni mwa jamii ambayo ililenga kuweka makosa ya kijinai ili kudhibiti wapinzani wa CCM katika uchaguzi mkuu na kukipatia mazingira ya ushindi chama hicho.
“Sasa imethibitika kuwa Bodi ya MCC iliyokaa tarehe 16 Dec 2015 imeahirisha rasmi kuidhinisha msaada wa Millenium Challenge uliokuwa umekusudiwa kwa Tanzania kwa mwaka wa fedha 2016. Sababu kuu mbili zilizosababisha uamuzi huo ni:

1. Mkwamo wa Uchaguzi wa Rais na Wawakilishi Zanzibar na

2.Matumizi mabaya ya she ria ya makosa ya mtandao hususan kuhusiana na uchaguzi Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa 2015.”

“Ubabe wa baadhi ya viongozi wa CCM ni janga la Taifa. Kuchelewa kupatikana kwa fedha za MCC si tu kunachafua jina la nchi na hadhi yake katika medani za kimataifa, bali kutaathiri kwa kiasi kikubwa miradi yote iliyo chini ya ufadhili wa MCC,” amesema Mwenyekiti Mbowe na kuongeza;
“Sheria ya makosa ya mtandao (Cyber Crime Act 2015) ni sheria mbaya sana inayokinzana na kukua kwa technologia ya habari na mawasiliano. Aidha, kwa makusudi kabisa inafifisha uhuru wa kupashana habari na ni dhahiri ilitungwa kwa nia mbaya ya kuthibiti kijinai uchaguzi mkuu.

“Tuliipinga sheria hii Bungeni na ikapitishwa usiku wa manane kwa ubabe wa wabunge wa CCM na hata tulipomtaka rais Kikwete asiisaini aliisaini kibabe akijua anaandaa mazingira gani ya “kihalifu”, “ amesema Mwenyekiti Mbowe.
Ameongeza kusema kuwa sheria hiyo ilitumika kuvamia vituo vya CHADEMA vilivyokuwa vikitumika kukusanya matokeo ya kura za rais na wabunge na hadi leo vijana zaidi ya 161, wakiwemo wanafunzi, wana kesi za “kubumba” mahakamani.

Mwenyekiti Mbowe amesema kuwa Sheria hiyo hiyo ilitumika kuficha dhana ovu iliyotumika kuhalalisha kuvamia Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kilichokuwa kikiratibu watazamaji wa uchaguzi wa ndani kwa kibali cha Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC).

“Vile vile Sheria hii imetumika kuwakamata na kuwaweka ndani na hata kuwanyima dhamana vijana wetu ambao walituunga mkono katika uchaguzi mkuu.

“Namtaka rais Magufuli achukue hatua za kiuongozi na kiutawala kwa kufanya yafuatayo:

“Kwanza aumalize mgogoro wa kisiasa Zanzibar kwa kuhakikisha kuwa mshindi halali anatangazwa.

“Pili achukue hatua ya kuifanyia marekebisho makubwa Sheria ya makosa ya mtandao katika bunge lijalo. Aidha wale wote waliobambikiwa kesi amuamuru DPP kuzifuta kesi hizo mara moja,” amesema.

Mwenyekiti Mbowe amesisitiza kuwa Rais Magufuli hana budi kuchukua hatua hizo za haraka ili kulinusuru taifa na hasara ya kupoteza mabilioni hayo ya MCC na zaidi kuepusha kuporomoka zaidi kwa biashara ya utalii nchini Zanzibar.

Amesema katika taifa ambalo sekta ya umeme inakabiliwa na matatizo makubwa katika uzalishaji, usambazaji na usafirishaji huku wananchi wa kipato cha chini wakibebeshwa mzigo mkubwa wa kumudu nishati hiyo na wengine wakilazimika kutumia nishati mbadala kama mkaa unaotokana na miti hivyo kusababisha uharibifu wa mazingira, serikali inayojua wajibu wake yenye viongozi wanaothamini uwajibikaji, haikupaswa kushindwa kuchukua hatua stahiki kutimiza vigezo vya msaada huo ambao umeshaisaidia Tanzania katika miradi mingine kadhaa.

Imetolewa Ijumaa, Desemba 18, 2015 na;

Tumaini Makene
Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano

CHADEMA

No comments:

Post a Comment