Thursday, July 2, 2015

Mnyika aibana serikali kuhusu uhaba wa mafuta.

Mbunge wa Ubungo, John Mnyika (Chadema) ameibana serikali kuhusu uhaba wa dizeli na petroli, kwa madai kuwa wamiliki wa vituo vya mafuta hayo wanayaficha kusubiri bei mpya.

Mnyika aliibua suala hilo jana bungeni, akitaka kusitishwa shughuli za Bunge ili suala hilo lijadiliwe kama jambo la dharula.
Alisema katika safari yake ya juzi kutoka jijini Dar es Salaam kwenda Dodoma, alitembelea vituo vya mafuta zaidi ya nane na kukuta huduma ya mafuta haitolewi kwa wateja.

Mnyika ambaye pia ni Waziri Kivuli wa Nishati na Madini, alisema kauli ya serikali iliyotolewa bungeni kukanusha kuwapo mgomo wa wauza mafuta si ya kweli.

"Kuna vituo vimegoma na vichache vimepandisha bei kupindukia, kwa kuwa kuna waliyoyahodhi mafuta, shughuli za Bunge zisitishwe tujadili,"alisema.

Hata hivyo, Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Charles Mwijage, alisema jukumu la wizara ni kuhakikisha sekta hiyo inatulia kwa kuwapo upatikanaji mafuta ambayo wananchi wanamudu na yenye viwango.

"Kuna ujumbe ulipitishwa juu ya uhaba wa mafuta, kabla ya taarifa hizo tulishafanyia kazi kuhakikisha tuna mafuta ya hifadhi ya kutosha siku 12 hadi 40,” alisema.

Alisema hivi sasa jitihada zinafanywa kwa kushirikisha Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (Tcra) kuwatafuta waliosambaza ujumbe huo.

Mwijage alisema maofisa wa wizara yake walitembelea vituo nane na kukuta hawauzi mafuta, lakini ilibainika kuwa ni kwa sababu hayakuwapo.

Alisema ikibainika kuwapo mfanyabiashara anayehifadhi mafuta pasipo kuyauza, adhabu itakayomkabili ni faini ya Shilingi milioni 20 au kufungiwa.

“Nimekuwa mkaguzi kwa zaidi ya miaka 30 hivyo naijua industry (sekta) hii vizuri, Watanzania wawe na amani mafuta yapo aliyesambaza ujumbe atakamatwa," alisema.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Fedha, Adam Malima, alisema kama kuna watu amehodhi mafuta, kuna sheria zinazowabana.

"Pale tulipo na uhakika wanafanya hujuma, serikali itachukua hatua kali kwa aliye na mafuta, kuna vituo tumeenda hana mafuta, hii ni serikali lazima ifanye kazi yake ipasavyo,” alisema.

Naye Naibu Spika, Job Ndugai, alisema anatambua lipo tatizo na kwamba ifikapo kesho litakuwa limeisha hivyo haoni sababu ya kusitisha shughuli za Bunge.

No comments:

Post a Comment