Wednesday, July 1, 2015

TAMKO KUHUSU KUAHIRISHWA KWA MUDA WA UBORESHAJI WA DAFTARI LA KUDUMU LA WAPIGA KURA KWA KUTUMIA TEKNOLOJIA YA “BIOMETRIC VOTERS REGISTRATION” (BVR) KATIKA JIJI LA DAR ES SALAAM NA MKOA WA PWANI

Kufuatia Tume ya Taifa ya Uchaguzi kuutangazia umma kuwa zoezi la uboreshaji wa Daftari la kudumu la wapiga kura liliokuwa lianze tarehe 04/07/2015 kwa Jiji la Dares Salaam na tarehe 25/06/2015 kwa mkoa wa Pwani kwamba limeahirishwa hadi tarehe itakayotangazwa tena; Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA)
Kanda Pwani (Mikoa ya Temeke, Kinondoni, Ilala na Pwani) kinaitaka Tume ifanye yafuatayo:

1. Tume ya Uchaguzi itangaze tarehe ya kuanza zoezi la uboreshaji wa Daftari la kudumu la wapiga kura katika Jiji la Dar es Salaam na mkoa wa Pwani baada ya
kuahirishwa ili kuwasaidia wananchi kujipanga kwa zoezi zima la uandikishaji.

2. Tume ya Taifa ya Uchaguzi izingatie mfumo wa kiuchumi na kimazingira uliopo katika mikoa hii unaowafanya watu wengi muda wa mchana kuwepo makazini/katika shughuli za kiuchumi. Na kupanga muda wakutosha kwa kuzingatia idadi ya wakazi. Hii ni pamoja na kuzingatia kuwa Jiji la Dar es Salaam na mkoa wa Pwani pekee, kwa takwimu za serikali, vina wapiga kura wapatao asilimia 15 ya wapiga kura wote nchini.

3. Tume ya Taifa ya Uchaguzi ihakikishe changamoto zote zilizotokea sehemu mbalimbali zinapatiwe ufumbuzi kabla ya zoezi halijaanza Dar es Salaam na Pwani. Changamoto hizi ni pamoja na; mashine kuwa mbovu, idadi ya mashinekutokukidhi mahitaji, idadi ya vituo kwenye kata kutoendana na idadi yawanaotakiwa kujiandikisha, utaratibu wa kuchukua majina bila kuzingatia waliopanga mistari, na waandikishaji kutokuwa na uwezo thabiti wa kutumia mashine za uandikishaji. Uzoefu umeonyesha kuwa, changamoto hizi zimeendelea kujirudiarudia katika sehemu nyingi bila kutolewa ufumbuzi wa uhakika na Tume ya Uchaguzi.

4. Tunaitaka Tume ya Taifa ya Uchaguzi kuweka wazi mbele ya umma kuwa Jeshi la Polisi halihusiki katika kupanga utaratibu wa BVR hali inayosababisha vurugu na ukosefu wa amani vituoni. Uzoefu uliopatikana wakati wa ziara zaviongozi wakuu wa chama kukagua zoezi la BVR katika maeneo mbalimbali unaonesha kuwa maeneo yote ambayo polisi hawakuwepo vituoni wakati wa uandikishaji, utaratibu ulikwenda kwa utulivu lakini hali imekuwa tofauti kabisa kote ambako jeshi hilo limehusika kusimamia uandikishaji. Mf; Arusha Tunapeda kusisitiza kuwa; CHADEMA haitofumbia macho mikakati yoyote itakayoonekana ina dhamira ya kudhoofisha zoezi la uandikishaji ambayo itasababisha kuwanyima wananchi haki ya kikatiba ya kupiga kura, maana bila kujiandikisha mtu hawezi kupiga kura.

Mwisho, CHADEMA inapenda kuwahamasishwa wananchi kujitokeza kwa wingi wakati wa zoezi la uandikishaji litakapoanza katika Jiji la Dar es Salaam na Mkoa waPwani.

Asanteni!

IMETOLEWA NA
Mhe. MABAERE N. MARANDO
MWENYEKITI WA CHADEMA KANDA YA PWANI

No comments:

Post a Comment