Friday, July 3, 2015

Chadema yaibwaga CCM mahakamani

Kiteto. Chama cha Mapinduzi (CCM), Wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara imezidi kupata pigo baada ya Mahakama kutengua matokeo ya uchaguzi wa wenyeviti wa vitongoji 16 vya mji mdogo wa Mirerani, kwa maelezo kuwa ulikiuka sheria na utaratibu wa Uchaguzi wa Serikali za Mitaa.

Hii ni mara ya pili katika kipindi cha mwezi mmoja kwa Mahakama kutengua matokeo ya uchaguzi huo ambao uliwaweka madarakani makada wa CCM.

Awali, Mei 30 Mahakama ya Hakimu Mkazi Wilaya ya Kiteto ilitengua matokeo ya uchaguzi wa mwenyekiti wa Kijiji cha Lobosireti kwa kukiuka sheria na utaratibu.

Chadema ilifungua kesi kadhaa mahakamani hapo kupinga kitendo cha wagombea wa CCM kupewa ushindi bila kufanya uchaguzi Desemba 14, mwaka jana.

Hukumu hiyo ya jana, inatokana na kesi zilizofunguliwa na Chadema wilayani Simanjiro kwenye kata za Endiamtu na Mirerani, wakipinga wagombea wa CCM kupewa ushindi bila kupigiwa kura kwenye Uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliofanyika Desemba 14 mwaka jana.

Hakimu Mkazi Mfawidhi mahakama hiyo, Elimo Massawe aliagiza kurudiwa kwa uchaguzi wa viongozi wa vitongoji vya Zaire, Kisimani, Tenki la Maji, Endiamtu, Kairo na Kazamoyo vilivyoko Kata ya Ediamtu.

Hakimu Massawe alitaja vitongoji vingine kuwa ni Sekondari, Kilimahewa, Tanesco, Kazamoyo Juu, Mji mpya, Tupendane na vitongoji vya Kata ya Mirerani ambavyo ni Kangaroo, Songambele A, Getini na Songambele B.

Katika kesi hiyo, Chadema iliwakilishwa na mawakili James Millya, Shadrack Kimomogoro na Daudi Haraka na Mahakama iliamuru walipwe Sh160 milioni za gharama za kesi hiyo ambayo ilichukua takribani miezi sita hadi kutolewa hukumu.

Katibu Mwenezi wa Chadema mkoani Manyara, Ambrose Ndege alisema Mahakama imetenda haki kwa kutoa hukumu sahihi na wanajipanga ipasavyo kuhakikisha watashinda vitongoji vyote pindi uchaguzi huo utakaporudiwa.

“Tuliwaeleza tangu awali kuwa uchaguzi ukifanyika tutawashinda saa nne asubuhi hivyo tunawasubiri uwanjani na tutaongoza Mamlaka ya Mji wa Mirerani kwani wananchi wanatukubali,” alisema Ndege.


Hata hivyo, Katibu Mwenezi wa CCM wa Kata ya Endiamtu, Mashaka Jeroro alisema wanatarajia kukata rufaa kupinga hukumu hiyo akisema wagombea wa Chadema walikosea kujaza fomu ndiyo sababu wakawekewa pingamizi.

No comments:

Post a Comment