Saturday, March 14, 2015

Viongozi watatu wa Chadema mahakamani.

Viongozi watatu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) akiwemo Diwani wa kata ya Ubungo, Boniface Jacob, wamefikishwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na mashtaka mawili la kushambulia na kumteka mlinzi wa Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk. Wilibrod Slaa.

Wengine ni Afisa Usalama wa Chadema, Hemed Sabula (48), mkazi wa Tandale kwa Tumbo na Afisa Utawala Chadema Benson Mramba (30), Mkazi wa Tabata Kisukuru.

Watuhumiwa wote walisomewa mashtaka yao jana mbele ya Hakimu Mkazi, Waliarwande Lema, na upande wa mashtaka ukiongozwa na wakili wa serikali Janet Kitale.

Akisoma shitaka la kwanza, Kitale alieleza kuwa Machi 7, mwaka huu kwa pamoja wakiwa kwenye ofisi ya Chadema Makao Makuu walimshambulia Khalid Kagenzi katika maeneo mbalimbali ya mwili wake.

Kitale alidai katika shitaka la pili ambalo lilitokea Machi 7, wakiwa katika eneo hilo kwa pamoja walimteka Kagenzi na kumpeleka kwenye hotel ya River View iliyopo Sinza na kukusudia kumtisha na kumuweka mafichoni.

Watuhumiwa hao walikana mashtaka hayo na kupewa masharti ya dhamana ambapo kila mmoja alitakiwa kuwa na wadhamini wawili na kusaini hati ya dhamana ya Sh milioni 10. Viongozi hao walirudishwa rumande na kesi hiyo itatajwa Machi 26, mwaka huu na upelelezi haujakamilika.

Wakati huo huo, Kamishina wa Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam, Suleiman Kova akizungumza na waandishi wa habari jana alisema kuwa jeshi la polisi linaendelea na uchunguzi kuhusu malalamiko ya Dk. Slaa ambayo yaliwafikia Machi 8, mwaka huu.

Alisema tuhuma hizo ziliwasilishwa na wakili wa Chadema, John Mallya, ambapo walipokea maelezo yake pamoja na mtuhumiwa Kagenzi (48) ambaye ni mlinzi wa Dk. Slaa.

Alisema kuwa wakili Mallya alidai kuwa uongozi wa Chadema pamoja na kamati ya ulinzi na usalama wa chama hicho ulichukua hatua mbalimbali za kujiridhisha kwamba Kagenzi ana tuhuma za kuhatarisha maisha ya Dk. Slaa kwa kutumia mbinu mbali mbali ikiwa ni pamoja na kumwekea sumu.

Alisema ndiyo maana alitumwa kumpeleka kituo cha polisi kwa ajili ya uchunguzi zaidi. Kamanda Kova alisema polisi ilipomhoji mlinzi huyo alidai kuwa ana majeraha mwilini yaliyotokana na mateso aliyofanyiwa akiwa chini ya ulinzi wa maafisa wa usalama wa Chadema ambao walikaa naye na kumhoji kuanzia saa 5 asubuhi ya Machi 7, saa 11 jioni ya Machi 8, mwaka huu akiwa chini ya ulinzi mkali.

Alisema katika suala hilo kuna mashauri mawili ambayo yanachunguzwa likiwamo la awali la DK. Slaa na la pili dhidi ya watuhumiwa wanaodaiwa kumtesa kwa kumshambulia Kagenzi na kumsababishia majeraha mwilini.


Juzi Dk. Slaa alihojiwa kwa zaidi ya saa sita na jeshi la polisi kuhusiana na malalamiko aliyoyatoa mlinzi huyo ya kupanga mikakati ya kutaka kumuua.

No comments:

Post a Comment