Wednesday, February 11, 2015

Mbowe: Hatutakubali kura zetu ziibwe Oktoba

Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema kimejipanga kuhakikisha katika uchaguzi Mkuu hawaibiwi kura.

Kauli hiyo ilitolewa jana na Mwenyekiti wa chama hicho, Freemon Mbowe wakati akizindua mafunzo ya Kikosi cha Ulinzi na Usalama cha chama hicho (Red Brigade), kwa vijana 200 wa Kanda ya Kati pamoja na Kikosi maalum cha Karate.

“Katika uchaguzi huu hatutaki kulalamika tena kwamba tumeibiwa kura na tutahakikisha tutaomba kura kwa wananchi na tutazilinda,” alisema Mbowe.

Alisema endapo watakubali kuibiwa kura maana yake hawapo tayari kuongoza.

Mbowe aliwataka vijana hao wa Brigade kutokukilinda chama peke yake bali pia kiwe chachu ya ulinzi kwa jamii inayowazunguka kwenye maeneo yao.

Alibainisha kuwa Chadema kitaendelea kutoa mafunzo ya ulinzi kwa vijana nchi nzima.

"Vijana hawa lazima wajenge moyo wa kujitolea, chama kilijengwa na watu wenye moyo huo ambao baadhi walipata madhara mbalimbali ikiwamo kupoteza maisha,” alisema Mbowe.

Alisema wajenge sifa ya kuwa wakombozi wa Taifa na malipo mengine siyo lazima walipwe hapa duniani bali watapata kwa Mungu.

No comments:

Post a Comment