Saturday, February 28, 2015

Mbowe apanda kizimbani Hai, aiomba Mahakama iifute kesi yake

Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Freeman Mbowe ameiomba mahakama kutupilia mbali kesi inayomkabili kwakuwa ni kesi iliyotengenezwa kutokana na chuki za kisiasa na jazba za kushindwa katika uchaguzi mkuu uliopita wa mwaka 2010.


Akitoa ushahidi mbele ya Hakimu mkazi mfawidhi wa mahakama ya wilaya ya Hai, Denis Mpelembwa ,Mbowe ameiomba mahakama kutupilia mbali kesi hiyo yenye lengo la kumpotezea muda katika uwajibikaji wake katika Taifa.


Awali kabla ya kuanza kwa kesi hiyo eneo la mahakama lilijaa mamia ya wafuasi wa chama hicho kutoka jimbo la Hai wakiongozwa na vijana wa ulinzi wa chama hicho maarufu kwa jina la redbriged waliokuwa wamevalia sare na kuzingira eneo lote la mahakama .


Mbowe alifika mahakamani hapo majira ya saa 14:05 ambapo kesi hiyo ilipangwa kusikilizwa lakini ilishindikana na kuanza kusikilizwa majira ya saa 16:05 kutokana na uwepo wa kesi nyingine ya wananchi kuvamia shamba la mwekezaji wa kampuni ya Tanganyika Filim Safari.


Akiongozwa na wakili wake Albert Msando Mbowe ambae pia ni mbunge wa jimbo la Hai alidai mahakamani hapo kuwa haoni sababu za kumpiga kijana mwenye umri kama wa mtoto wake na kuiomba mahakama kuifutilia mbali kesi hiyo.


Mbowe anakabiliwa na kesi ya kumshambulia mwangalizi wa ndani wa uchaguzi mkuu wa mwaka 2010, Nasir Yamin, wa Jimbo la Hai


Awali Mbowe aliieleza mahakama kuwa siku ya tukio alipata taarifa kuwa kwenye kituo cha uchaguzi cha zahanati kilichopo kata ya Nshara kuwa kuna mtu aliyeko kwenye chumba cha kujiandikisha kinyume cha taratibu.

No comments:

Post a Comment