Saturday, November 15, 2014

Chadema chawataka wananchi kuwachagua Ukawa

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimewataka wananchi wa Kigoma kuwachagua viongozi wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) katika uchaguzi wa serikali za mitaa ili waweze kuwaletea maendeleo .
Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe, alisema hayo jana katika ziara yake ya "Operesheni Delete CCM" alipokuwa akihutubia mkutano Jimbo la Kasulu na Kibondo mkoani hapa.

Katika kuhitimisha ziara yake Kigoma, alisema kuwa umefika wakati muafaka kuipumzisha CCM na kuwapa wapinzani ili kuwaletea maendeleo.

Alisema huduma za jamii zimekuwa duni kutokana na uongozi mbovu wa chama tawala huku mahospitalini kukiwa hamna dawa, pia upande wa elimu kukiwa na matabaka ya watoto wa wakubwa wakisoma shule za kimataifa na wale wa maskini wakisoma katika shule za taka ambazo hazina maabara, vitabu wala walimu wa kutosha.

Operesheni hiyo ilianza mkoani Tabora, Katavi, Kigoma na sasa itaendelea mkoani Morogoro lengo likiwa ni kuwaelimisha wananchi kuhusiana na uchaguzi wa serikali za mitaa na kuwachagua wapinzani na kuikataa katiba iliyopendekezwa.

“Inabidi wana Kigoma kuikataa CCM kuanzia chaguzi za serikali za mitaa na uchaguzi mkuu ujao kwa kuwachagua viongozi wa Ukawa ili kuwaletea maendeleo," alisema Mbowe.

No comments:

Post a Comment