Saturday, March 29, 2014

Sasa kura mseto

Kamati ya maridhiano yakubaliana kura zote mbili zitumike
Ingawa wajumbe wengine walipinga kwa kura ya 'ndiyo' na 'hapana'

Hatimaye Bunge  Maalumu la Katiba limeridhia wajumbe kupiga kura ya wazi na siri katika kupitia mchakato wa rasimu ya katiba mpya.
 
Maamuzi hayo yalitolewa jana jioni baada ya Kamati ya Maridhiano iliyokutana kuanzia juzi usiku hadi jana mchana kukubaliana kuwa na kura za aina mbili,  kufuatia mvutano mkubwa ulioibuka baina ya wajumbe hao.
 
Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta, aliamua kuunda kamati hiyo baada ya mapendekezo kutokana na michango iliyotolewa na wajumbe katika mjadala wa juzi, ambapo Freeman Mbowe, alikuwa mmoja wa wajumbe waliotoa hoja hiyo.
 
Sitta aliunda kamati hiyo iliyokuwa na wajumbe Freeman Mbowe, Profesa Ibrahim LIpumba, Askofu (mstaafu) Donald Mtetemela na Vuai Ali Vuai.
 
Kabla ya kutolewa kwa uamuzi huo, Sitta aliwaruhusu wanakamati hiyo kila mmoja kutoa yale waliyoamua. 
 
Akiongea kwa niaba ya Mbowe,  Johna Mnyika  alisema mazungumzo yamesaidia kupiga hatua moja mbele ingawa ya kukubaliana kutokubaliana.
 
“Sisi tulikuwa na mtazamo kuwa kura iwe ya siri lakini wengine walitaka kura ya wazi. Pamoja na majadiliano yote wenzetu waliona wana uhuru wa kupiga kura ya wazi, ilibidi tufike hatua ya kuamua kulivusha taifa ili lisonge mbele.” 
 
Alisema walipendekeza maamuzi haya yafanywe kwa kura ya wazi lakini wao  waliamua yafanyike kwa siri.
 
Alisema wameamua anayetaka kupiga kura ya wazi apige ya wazi na atakayeamua ya siri iwe ya siri. Matokeo yatakayopatikana kwa minajili ya kupiga hatua moja mbele na kulisogeza taifa mbele.
 
“Wenye kukubaliana na kura ya wazi watakuwa wengi, na wanaotaka kura ya siri watasema hapana na kwa vyovyote walio wengi watashinda,”
 
Alisema utaratibu huu wa mashauriano ni vizuri utumike hata pale ambapo hawakubaliani ili kupiga hatua mbele.
 
“Sisi hatuna njama zozote za kuvuruga bunge hili kwa sababu tumepigania sana jambo hili na kutaka Watanzania wapate Katiba iliyo bora,” alisema.
 
Alisema wapinzani hawana dhamira ya kukwamisha mchakato wa Katiba. “Kwa sababu kuna magazeti yamemnukuu Mheshimiwa Rais …
 
PROFESA  IBRAHIM LIPUMBA
Alisema unapofanya mchanganyiko wa kura ya wazi na siri ni kuwafanya wale wanaotaka kura ya siri kutopata haki yao lakini Ili tusonge mbele na kuanza kujadili Rasimu ya Katiba, tupige kura ya wazi na siri tufanya maamuzi.
 
Lakini hii si kura nzuri ni kura itakayotupa vikwazo. “Mimi binafsi ntasema hapana kwa jambo ambalo limeletwa juu ya meza kulifanyia maamuzi. Lakini ili tusonge mbele tumeona tulifanyie maamuzi hayo.
 
“Natoa wito kwa CCM pamoja na kuwa wengi ni vyema kuheshimu mawazo ya wachache “, alisema na kuongeza kuwa  CCM wangekuwa na busara wangeweza kuongeza idadi ya kamati kwa kuweka mbele ya Watanzania.
 
VUAI ALI VUAI
Sisi kwa upande wetu tulikuwa na msimamo wa wazi na wenzetu walikuwa na msimamo wa siri. Sisi tuliotoka CCM tulikubali twende na mifumo yote miwili. Wale watakaokuwa tayari kupiga kura ya wazi wapewe haki yao ya wazi bila vikwazo na siri hivyo hivyo,
CCM itakuwa ya mwisho kusitisha mchakato wa Katiba, matakwa yetu ilikuwa ni kura ya wazi ili tufanye maamuzi tukiwa tunaonekana.
 
“Tulichotoka nacho kule ndani tunakwenda na kura ya siri kwa wanaotakana na kura ya wazi kwa wanaotaka,” alisema.
 
ASKOFU (mstaafu) DONALD MTETEMELA
Kila mmoja ana haki ya kuwa na msimamo au wazo lake ila wananapaswa kuheshimu jambo lililowaleta hapa ndani ya bunge na kukubali kutoa tofauti zao kwa mashauriano ili mchakato huo uendelee.
 
Wajumbe warudi kwenye azimio la kamati juu ya upigaji kura kwani tumekuwa tukijadili suala la kanuni hadi sasa ni siku 40 na hatujaanza kazi ambayo tulikuja kuifanya. Siku zimekwisha tusiongeze nyingine kwa kuleta hali ya kutofautiana. Tusinga’ng’anie kila kitu ni hapana na kung’ang’ania misimamo yetu. Tusonge mbele ili kutimiza lengo la kupata Katiba mpya.
 
KURA YAPIGWA KUPITISHA AZIMIO
 
Mwenyekiti wa Kamati ya Kanuni na Haki za Bunge, Pandu Ameir Kificho, alitangaza wajumbe hao kupiga kura ili kupitisha azimio hilo la kupiga kura ya wazi na siri.
 
Kura hizo ndizo zitakazotumika kwenye vikao vya kamati kwa ajili  ya kujadili rasimu ya katiba.
 
Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba, Sitta, alimtaka Katibu wa Bunge , Yahaya Khamis Hamad, kutangaza utaratibu wa wajumbe kupiga kura ambapo alisema kila mjumbe ataitwa jina  mmoja mmoja, kutamka “ndiyo” au “hapana” kwa wale waliamua kupiga kura ya wazi.
Aidha, kwa wale walioamua kupiga kura ya siri watakwenda mbele na kutumbukiza kura zao za siri kwenye masanduku ya kura.
 
Hadi tunakwenda mitamboni wajumbe walikuwa wanaendelea kupiga kura na baadhi walipiga ya wazi kukataa wakisema hapana. Wengine walipiga kura ya wazi kukubali wakisema ndiyo.
Hadi wakati huo wajumbe wote wa CCM walipiga kura ya  wazi kwa kusema ndiyo, wakati wajumbe wa Chadema na CUF walipiga kura ya wazi ya kukataa wakisema hapana  hali iliyoonyesha misimamo dhahiri ya kichama .
 
Miongoni mwa waliopiga kura ya wazi  ya hapana ni Waziri wa Sheria na Katiba wa Zanzibar, Abubakar Khamis, Profesa Ibrahim Lipumba, Juma Haji Duni  na kwa upande wa wajumbe wa CCM waliosema hapana kwa azimio hilo ni pamoja na Deo Filikunjombe, wakati mjumbe wa Chadema Godbless Lema , hakusema neno na hakupiga kura kwenye karatasi.

No comments:

Post a Comment