Wednesday, February 5, 2014

Mbowe amlipua JK

MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo  (CHADEMA), Freeman Mbowe, amemvaa Rais Jakaya Kikwete, akimtaka kuacha kutafuta huruma ya Watanzania juu ya suala la Katiba na badala yake atumie nafasi hiyo kuwataka wabunge wake kuheshimu maoni ya wananchi.
Mbowe ambaye pia ni Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, alisema kuwa hotuba ya Rais Kikwete juzi kwamba Katiba haiwezi kupatikana kwa ngumi imejaa upotoshaji kwa wananchi.
Katika hotuba yake ya maadhimisho ya miaka 37 ya kuzaliwa kwa CCM, yaliyofanyika mkoani Mbeya, Rais Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM, alimshangaa Mbowe kwa kauli yake kwamba mfumo wa serikali tatu ukikataliwa katika Bunge hilo nchi haitatawalika.
“Huku ni kuwadanganya wananchi, pale hakuna ngumi wala vurugu yoyote, kila ibara iliyopo katika rasimu itajadiliwa ili upatikane mwafaka. Huku ni kukosa ukomavu wa kisiasa,” alisema.
Akizungumza na Tanzania Daima jana, Mbowe alisema ni vema Rais Kikwete akaacha kuhangaika na wapinzani, badala yake awe tayari kuheshimu mawazo ya wananchi waliyotoa wakati wa kutoa maoni ya Katiba.
Mbowe alisema kuwa Rais Kikwete ni mwanasiasa na mtu anayejaribu kupotosha hoja, kwani CHADEMA waliposema watapambana, hawakumaanisha kupigana ngumi kama alivyosema kiongozi huyo.
Alisema kuwa viongozi wa CCM wamekuwa wakilazimisha ajenda ya Katiba mpya kuonekana kama sera yao, jambo ambalo CHADEMA haiwezi kuafiki.
“Katiba ni ya wananchi, si ya chama chochote cha siasa, ndiyo maana hatukubali kuona mawazo ya wananchi yakishindwa kuheshimiwa,” alisema.
Mwenyekiti huyo alisema Tume ya Mabadiliko ya Katiba inayoongozwa na Jaji Joseph Warioba imefanya kazi nzuri ambapo Rais Kikwete na wabunge wake wanapaswa kuheshimu mchango huo.
Alisema kuwa CHADEMA itahakikisha inashindana kwa hoja katika Bunge la Katiba litakaloketi hivi karibuni na iwapo hilo litashindikana watarudi kwa wananchi ambao ndio wenye uamuzi wa mwisho juu ya suala hilo.
“Wajumbe watakaoshiriki Bunge la Katiba ni 640 ambao hao si waamuzi wa mwisho na kama tutaona kuna suala lolote linaloenda kinyume, sisi tutakachokifanya ni kurudi kwa wananchi kuwaeleza juu ya kilichotokea na hao ndio wenye maamuzi ya mwisho katika kura ya maoni,” alisema.
Mbowe alisema kuwa hata katika kushindana kwa hoja CCM wanapaswa wasiweke hila, maana wataweza kuchangia mchakato huo kushindwa kufanikiwa.
Alisema kuwa nia ya CHADEMA ni kuhakikisha Katiba nzuri, bora na iliyo ya wananchi inapatikana na si kusababisha vurugu kama ambavyo Rais Kikwete amejaribu kupotosha.
“Hila hiyo imeonekana wazi maana kuna hali ya kutaka kupuuza mawazo ya wananchi na CCM kulazimisha mawazo yao, hilo hatutalikubali na tutapambana…hiyo si mara ya kwanza kupambana katika suala hilo,” alisema.
Mbowe alisema kuwa kuhusu serikali tatu ni muhimu Rais Kikwete akaheshimu mawazo hayo na CHADEMA itashindana kwa hoja juu ya suala hilo ili kuhakikisha mawazo hayo yaliyowasilishwa na Jaji Warioba yanaheshimiwa.
Katika ziara ya mikutano ya hadhara ya CHADEMA iliyopewa jina la Operesheni M4C Pamoja Daima, Mbowe na viongozi wengine waliionya Serikali ya CCM kutochakachua mchakato wa Katiba, kwani Watanzania hawako tayari kurudi kwenye Katiba ya sasa ambayo alidai imekosa uhalali wa kuongoza nchi.
Alisema CCM kwa kutumia wabunge wake wakiamua kuhujumu mchakato huo bungeni, yeye na viongozi wenzake watapita nchi nzima kuwataka wananchi wasishiriki kura za maoni na yuko tayari kufunguliwa kesi kwa kudai Katiba mpya.

No comments:

Post a Comment