Wednesday, February 12, 2014

Chadema kuvamia majimbo ya Maghembe, Kilango, Mwanri

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) mkoa wa Kilimanjaro,   kitatumia helikopta na magari tisa kuanzia leo kushinikiza wananchi wa majimbo ya Same na Siha yanayoongozwa na Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu,Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Aggrey Mwanri kuwakataa wabunge hao katika uchaguzi mkuu ujao kwa madai wameshindwa kuwajibika.

Mwenyekiti wa Chadema mkoani hapa ambaye pia ni Mbunge wa  Moshi Mjini, Philemon Ndesamburo, aliyasema jana kuhusu operesheni hiyo itakayoongozwa na makada wa kitaifa wa chama hicho akiwamo Mnadhimu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni,Tundu Lissu.

”Tutaweka kambi ya siku sita katika jimbo la Siha, Same, Mwanga na Moshi Vijijini, lakini nguvu kubwa ni kwa mawaziri wawili ambao tumeweka mkakati wa kuwang’oa kwa kuhakikisha hawarejei tena madarakani na halmashauri hizo zitaongozwa na Chadema.

Ushindi tulioupata Kiborilonitutaupeleka kesho(leo) kwa helkopta na magari tisa ya Operesheni Pamoja
Daima ya M4C,” alisema Ndesamburo.

 Operesheni hiyo itayahusu majimbo ya Same Magharibi, Same Mashariki, Mwanga, Vunjo Moshi Vijijini na  Siha. Alisema lengo la operesheni hiyo ni kukiimarisha chama kuanzia ngazi ya shina pamoja na kufanya chaguzi za viongozi katika maeneo hayo.

Ndesamburo alisema lengo jingine ni kuendelea kuwafumbua wananchi kuhusu mchakato wa katiba mpya ambao kwa sasa umefikia katika hatua yakuanza kwa mjadala wa rasimu ya pili ya katiba Bungeni pamoja na umuhimu wa kujiandikisha katika daftari la kudumu la wapigakura.

Chadema kimefanikiwa kutetea Kata ya Kiboriloni katika uchaguzi mdogo uliofanyka juzi baada ya kupata  kura 1,019 dhidi ya kura 255 alizopata mgombea wa CCM, Willy Tulli na Adon Mzava wa UDP aliyeambulia kura mbili.

No comments:

Post a Comment