Wednesday, January 8, 2014

Zitto ajilipua - PROFESA BAREGU

ALIYEKUWA Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe, ametoa kauli nzito, baada ya kusema viongozi wa vyama vya siasa wanaopekua mawasiliano ya raia ni hatari kwa nchi na kwamba wakishika dola, raia wao hawatapona.

Kauli ya Zitto imekuja siku moja tu baada ya Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk. Wilbrod Slaa, kuutangazia umma kuwa wamenasa mawasiliano ya siri yanayodaiwa kufanywa na Zitto. Zitto aliliambia MTANZANIA jana kwa njia ya ujumbe mfupi wa simu kwamba sheria za nchi zinazuia mtu kupekuliwa mawasiliano yake.

“Sheria za nchi zinazuia mtu kupekuliwa pekuliwa mawasiliano, haki ya faragha ni haki yangu ya msingi.

“Kama viongozi wa chama cha siasa cha upinzani wanafanya kazi ya kupekua mawasiliano ya raia na kujiona wanafanya sahihi, watu hao ni hatari kwa nchi, maana wakishika dola raia hawatapona. Mimi siwajali watu hawa, nawadharau,” alisema Zitto.

Akizungumzia uamuzi wa kuvuliwa uanachama kwa aliyekuwa Mwenyekiti wa CHADEMA Mkoa wa Arusha, Samson Mwigamba na Mjumbe wa Kamati Kuu, Dk. Kitila Mkumbo, Zitto alisema chama kimefanya uamuzi wake.

“Chama kimefanya uamuzi wake na ni wajibu wao akina Kitila na Mwigamba kuona kama wanapaswa kukata rufaa au hapana,” aliongeza Zitto.

Aidha amesikitishwa na kauli ya Dk. Slaa kuzuia wanachama wake kushiriki mikutano yake ya kisiasa, kwani kufanya hivyo ni kukosa busara.

“Kwangu mimi, uamuzi wa Katibu Mkuu kuzuia viongozi na wanachama kushiriki mikutano yangu nadhani ni kukosa busara na hekima, suala langu bado liko mahakamani, likitoka litarudi kwenye chama.

“Nasisitiza, kutangaza namna hii si sawa kabisa kwa mujibu wa misingi yote ya demokrasia,” alisema Zitto.


PROFESA BAREGU
Naye Mjumbe wa Kamati Kuu ya chama hicho, Profesa Mwesiga Baregu, alisema viongozi wa chama hicho wanapaswa kulinda kauli zao ili kuepuka mvuragano unaoweza kutokea wakati huu.

“Wakati huu ambao chama kimekuwa na mambo mengi, nawasihi viongozi kuchunga kauli zao ili kuepuka matatizo ambayo yanaweza kujitokeza.

“Nimekuwa msuluhishi ndani ya chama, nakwambia ndani ya chama haiwezekani fikra moja ikaendelea kudumu, kwa msingi huo lazima watu watofautiane mtazamo, si kila jambo kupinga.

“Katika hali hii, msimamo wangu ni kwamba changamoto inayotukabili tupunguze makali ya maamuzi, kwa sababu Watanzania wengi wanakitegemea chama hiki.

“Hivi sasa Watanzania wanajiandaa kukikabidhi CHADEMA dola, ni wakati mzuri wa viongozi kufikiria maisha ya chama kwanza na baadaye ukweli wa mambo utajulikana,” alisema.

No comments:

Post a Comment