Tuesday, January 21, 2014

Mnyika: Wananchi mwandikieni barua JK

MBUNGE wa Ubungo, John Mnyika (CHADEMA), amewashauri wananchi wanaoishi kandokando mwa hifadhi ya Barabara ya Morogoro kumwandikia Rais Jakaya Kikwete barua  kuhusu mgogoro uliopo katika barabara hiyo.
Mnyika alitoa ushauri huo katika mkutano uliofanyika Luguruni Park, Dar es Salaam ambao ulihudhuriwa na wawakilishi wa  wananchi  zaidi ya 5,000 wanaoishi  kandokando mwa barabara hiyo ambao nyumba zao zimewekewa alama za ‘X’ na Wakala wa Barabara (Tanroads)  kwa ajili ya ubomoaji.
Alisema haoni haja ya kupanua barabara kutoka Kibaha hadi Dar es Salaam wakati maeneo mengine ya nchi hayana barabara zinazopitika kwa kirahisi.
Alisema upanuaji wa barabara hiyo unakiuka amri halali ya mahakama iliyoamuru Tanroads kusitisha zoezi hilo, kwa mujibu wa hukumu iliyotolewa mwaka jana na Mahakama Kuu Kitengo cha Ardhi.
Mwenyekiti wa  Kamati  ya waathirika hao, Chrizant Kibogoyo, alisema wamemiliki ardhi hiyo kihalali zaidi ya miaka 30 hadi kufikia mwaka 2000 ambapo Waziri John Magufuli aliagiza Tanroads kuingia katika ardhi na makazi yao hadi mita 120 toka katikati ya Barabara ya Morogoro pande zote mbili kuanzia Kibaha hadi Tamco.
Kibogoyo alisema uingiaji huo si halali, kwani  haukuheshimu hatimiliki zilizotolewa na Wizara ya Ardhi yenye dhamana kwa mujibu wa sheria za nchi kuthibitisha umilika wa ardhi.

No comments:

Post a Comment