Tuesday, May 28, 2013

Mdee awavaa wenye mashamba makubwa

Kambi ya Rasmi ya Upinzani Bungeni, imeorodhesha mashamba 36 yenye ukubwa wa maelfu ya hekta za ardhi ambayo wananchi waliporwa kimabavu na Serikali kwa kutofuata sheria na kisha kupewa wawekezaji. 

“Naamini taarifa hii itapelekea Bunge lako tukufu, kutoa au kufanya maamuzi yenye busara kwa manufaa ya taifa na wananchi wake,” alisema Msemaji wa Kambi ya Upinzani, Halima Mdee, alipokuwa akisoma hotuba ya kambi hiyo kuhusu Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa mwaka 2013/14. 

Pia Mdee alisema kuna mashamba sita ambayo taarifa za wawekezaji haziko wazi ama hazieleweki. 

Alitaja mashamba hayo kuwa ni Chawangwa ambalo lina  hekta 200 za ardhi ya Kijiji (1), lipo Kisarawe. Lilikuwa ni kwa ajili ya kilimo cha Jatropha lakini  halijaendelezwa, Euro Mine Export  Ltd ambayo shamba lake lipo Mikese mkoani Morogoro kwa ajili ya kilimo cha Jatropha.  

Mashamba mengine ni yaliyopewa ni kampuni ya Oxman Tanzania Ltd lililopewa Rufiji kwa ajili ya Kilimo cha Mpunga na lile lililopewa Kampuni ya Rubana ambalo lipo Mwanza kwa ajili ya kilimo cha Jatropha ambalo hata hivyo  halijulikani kwa maafisa kilimo wa  ardhi wa Wilaya. 

Makampuni mengine yaliyopewa mashamba na kushindwa kuendeleza ni Kampuni ya Synergy Tanzania Ltd iliyopewa shamba la hekta 20,000 huko Rufiji kwa ajili ya kilimo cha Mpunga, Tanzania Biodiesel Plant ambalo lina hekta 16,000 za shamba, ambalo lipo Bagamoyo. 
 
VIGOGO WA CCM
Mdee alisema Mwenyekiti wa CCM wa Wilaya ya Simanjiro, Brown Oleseya, ambaye amemilikishwa kiujanja ujanja hekta za kijiji 3425. 

Alisema licha ya kujipatia kiwanja hicho kiujanja ujanja, Oleseya amewafungia wananchi njia zote za chemchem za maji ya malisho ya mifugo. 

Alisema Agosti 31 mwaka 2009, Oleseya kwa kushirikiana na watumishi wasio waaminifu walibadilisha matumizi ya shamba kutoka kilimo na ufugaji kuwa hifadhi ya kitalii. 
Alisema nyaraka zote anazozitumia kama ushahidi mwenyekiti huo, hazina uhalali wowote kisheria.

Mdee alihoji iwapo serikali kueleza kama iko tayari kuvunja majumba makubwa ya wenye fedha waliouziwa maeneo ya wazi kinyume na utaratibu nma kupewa hati na maofisa wasiowaamifu. 

“Serikali inatoa tamko gani juu ya kiwanja namba 856 cha Msasani Beach ambalo kwa mujibu wa ramani ya upimaji iliuosajiliwa namba 29331 ilikuwa ni kwa matumizi ya wazi?,”alihoji.
 
Alisema hali hiyo ilifanya njia ya mkondo wa maji kuelekea baharini imezibwa na mvua ikinyesha maeneo ya Warioba yanajaa maji.

No comments:

Post a Comment