Monday, August 6, 2012

Walimu watishia kuing’oa CCM


WASEMA HAKUNA MAISHA BORA CHINI YA CCM
WAKATI walimu wakikubali kurejea kazini na kuendelea kutafakari amri ya mahakama, mkakati mzito unapangwa kuhakikisha hawakiungi mkono Chama cha Mapinduzi (CCM) kwenye Uchaguzi Mkuu mwaka 2015.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili, umebaini kuwa tangu kutolewa kwa kauli ya Rais Jakaya Kikwete kwamba mgomo huo si sahihi na serikali yake haina uwezo kutimiza madai yao na kufuatiwa na uamuzi wa mahakama, walimu wamekuwa wakiangalia namna nyingine ya kuibana serikali.
Mwishoni mwa wiki, walimu katika wilaya ya Ukerewe, mkoani Mwanza, walikuwa na kikao kizito ambapo pamoja na mambo mengine, walipendekeza kuiangusha CCM kwenye uchaguzi mkuu mwaka 2015.
Katika mkutano huo ulioitishwa na uongozi wa Chama cha Walimu (CWT) na kufanyika katika ukumbi wa Afro Berch mjini Nansio Ukerewe, baadhi ya walimu ambao waliomba majina yao yahifadhiwe, waliwataka wenzao waungane kuing’oa CCM kwa madai kuwa serikali inayoiongoza imeshindwa kusimamia maslai yao.
“Ndugu zangu walimu, walimu tusitarajie kupata maslai bora kama CCM itaendelea kushika dola. Hebu angalieni tangu tulipoanza mvutano na serikali chama hicho kimebaki kimya huku kikitambua matatizo makubwa yanayotukabili. Tuungane tufanye maamuzi magumu mwaka 2015,” alisema mwalimu huyo.
Huku akiungwa mkono na walimu wengi, mwalimu huyo bila kumung’unya maneno, alisema ingawa maadili ya utumishi wa umma yanazuia watumishi kushiliki siasa, lakini muda umefika kwa walimu kutumia ushawishi wao kuhakikisha mwaka 2015, CCM inang’oka madarakani.

Mwalimu huyo alisema, walimu wakiamua kwa wingi wao wanaweza kwani ndio wanaotumika na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) wakati wa uchaguzi.
Mwalimu mwingine aliungana na mwenzake kuishambulia CCM kwamba inalinda kundi dogo la wanasiasa wanaoneemeka na rasilimali za taifa huku Watanzania wengi wakikabiliwa na umaskini.
Mwalimu huyo pia aliushambulia mfumo wa mahakama kwamba hauko huru kwenye kutoa maamuzi, akitolea mfano uamuzi wa kesi yao kuwa ulikuwa na mkono wa serikali.
Kwa upande wake, Katibu wa CWT wilayani humo, John Kafimbi, alimlalamikia Rais Kikwete kuzungumzia kesi yao huku akijua fika kwamba suala hilo liko mahakamani.
Aliwataka walimu wajipongeze kwani katika kipindi cha mgomo, wamedhihirisha kwamba wakiamu wanaweza kupigania haki zao.
Jijini Dar es Salaam, Chama cha Wananchi (CUF), kimesema Rais Kikwete ameudanganya umma kwamba serikali inahitaji asilimia 75 ya bajeti yake kuboresha maslahi ya walimu tu wakati kiasi hicho ni kwa ajili ya watumishi wote.
Mbali ya hilo, CUF imeitaka serikali kuacha kutumia mahakama kuzima madai ya msingi ya walimu bila kutafuta njia sahihi ya kutatua.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mwenyekiti wa CUF Taifa, Profesa Ibrahim Lipumba, alisema katika mazungumzo yake na wahariri wa vyombo vya habari yaliyofanyika Ikulu jijini Da es Salaam Agosti mosi, Rais Kikwete alichukulia madai ya walimu na kulinganisha na nyongeza ya wafanyakazi wote serikalini badala ya kuja na tamko la kushughulikia matataizo ya walimu.
“Rais anaposema tutatumia asilimia 75 ya bajeti kama tukitekeleza madai ya walimu hawatendei haki Watanzania waliomsikiliza kwani alitumia takwimu za wafanyakazi wote serikalini kama wataongezewa mishahaya kwa kiwango hicho na kuyafanya ndiyo madai ya walimu,” alisema Prof. Lipumba.
Alisema, ingawa CUF haiamini kama migomo ya wafanyakazi ndio suluhu la matatizo, inaamini walimu wana madai ya msingi na ya haki yanayopaswa kushughulikiwa na kupewa kipaumbele.
Mwenyekiti huyo wa CUF alimshangaa Rais Kikwete kushindwa kueleza mikakati ya kutekeleza madai ya walimu ili kuwanusuru na hali ngumu ya maisha.
“Serikali isiyo na mipango kwa vyovyote vile haina uhalali wa kuwatumikia wakulima na wafanyakazi, na hali hiyo inaitia aibu serikali inayoamua kuwahadaa walimu kwa mambo yaliyo wazi,” alisema Prof. Lipumba.
Alisema kuna fursa nyingi ambazo serikali ya CCM imeshindwa kuzitumia na kama zingetumiwa ipasavyo, leo kusingekuwa na madai ya walimu wala wafanyakazi wa kada nyingine.
“Kwa kweli elimu ya Tanzania itaendelea kuwa duni ikiwa mchezo huu wa kuwapiga danadana walimu utaendelea….vigogo wa CCM ambao watoto wao wanasoma katika shule za kimataifa na za kimombo, katu hawawezi kuwafikiria watoto wa maskini wasio na mbele wala nyuma,” alisema Prof. Lipumba.
Alibainisha kuwa lazima walimu watambue CCM haiko madarakani kutatua matatizo yao, hivyo ni vema wakaungana kuhakikisha chama hicho kinaondoka madarakani.
Hivi karibuni Mahakama Kuu divisheni ya kazi ilisitisha mgomo wa walimu kwa madai kuwa ni batili.
Mahakama hiyo iliamuru pande zote zinazotofautiana kurudi katika meza ya majadiliano kwa ajili ya kusaka suluhu.

No comments:

Post a Comment