Saturday, November 14, 2015

Polisi na Mahakama Kilwa watesa wafuasi wa UKAWA

VIJANA watano wafuasi wa UKAWA wilayani Kilwa kwa wiki tatu sasa wanasota mahabusu kwa sababu ya kunyimwa dhamana kutokana na tuhuma za kufanya kosa la uporaji kwa kutumia silaha.

Vijana hao ni Rifati Mnakatu (Katibu Chadema Kata ya Mitole), Ali Matumla (Mwenyekiti CDM Kata ya Mitole), Fadhili Mbopo (CDM), Chande Hemedi Nyayo (CUF) na Omari Mkonda (CUF).

Wengine walioshikiliwa ni Hassani Ukurwa na mzee aliyejulikana kwa jina moja la Mabruki wote wakiwa wanachama wa CCM.

Hata hivyo Ukurwa aliachiwa kwa hoja walizozitoa Polisi kuwa yeye ni CCM kwani nyumbani kwake walikuta mabango ya CCM na siku ya pili yake Mabruki pia aliachiwa kwa hoja kwamba yeye ni mwanachama wa CCM, hii inaonyesha kuwa Polisi hao walilenga kundi la vijana wanaounga mkono vyama vya UKAWA.

Kamanda wa Polisi wa Wilaya ya Kilwa, Jastin E. Josephy, akiongea na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu alikiri vijana hao kufikishwa polisi na kuwekwa mahabusu kwa siku kadhaa kabla ya kupelekwa mahakamani.

Alipoulizwa kwa nini vijana hao waliwanyima fursa ya kupatiwa dhamana ya kipolisi (police bail) kwa siku zote walipokuwa kituo cha polisi, alidai kuwa polisi walikuwa na kazi nyingi za uchaguzi.

Alipoulizwa kama vijana hao wamekwisha fikishwa mahakamani alikiri, lakini akasema hawakupewa dhamani. Kamanda huyo alidai kwamba dhamana ya vijana hao imezuiliwa na mwendesha mashtaka wa polisi kwa sababu vijana hao wanatuhumiwa kufanya kosa la uporaji kwa kutumia silaha, kosa ambalo, kwa mtazamo wa polisi, halina dhamana.

Mmoja wa vijana waliokamatwa anatuhumiwa kukutwa na kadi mbili za wapiga kura nyumbani kwake, kadi ambazo sasa vijana wote watano wanadaiwa kuziiba kutoka kwa wamiliki halali baada ya kutumia vitisho vya silaha. Cha kushangaza kadi hizo ni za ndugu zake anaoishi nao lakini ikaonekena ni moja ya kadi zilizoporwa.

Sakata hili lenye sura ya kisiasa, lilibuka baada ya mgombea Ubunge katika jimbo la Kilwa Kaskazini kwa tiketi ya CCM, Murtaza Mangungu, kutishia kuwaua wananchi kwa kutumia bastola kufuatia mabishano kuhusu uhalali wa Bango la UKAWA kuwepo mahali fulani.

Mabishano hayo yalitokea mnamo Alhamisi tarehe 22 Oktoba 2015, siku tatu kabla ya Uchaguzi Mkuu, katika Kijiji cha Mitole, Kata ya Mitole, Tarafa ya Njinjo katika Jimbo la Kilwa Kaskazini.

Zahama hiyo ilianza baada ya kumalizika kwa mkutano wa hadhara wa mheshimiwa Mangungu, pale msafara wa mgombea ubunge huyo ulipokuwa unaondoka kutoka katika kijiji cha Mitole na baadaye njiani kukutana na bango lililoninginizwa juu katikati ya barabara kwa kutumia kamba na kushauriana kulitoa.

Baada ya kufika hapo wapambe wa Mangungu walishauriana kulibandua bango hilo kinyume na sheria za uchaguzi. Bango hilo lilikuwa na picha ya mgombea wa udiwani wa Kata ya Mitole kupitia tiketi ya CUF, Said Mnakatu, aliyekuwa anaungwa mkono na vyama vya UKAWA.

Maamuzi ya wapambe wa Mangungu ya kuliondoa bango yalileta hasira kwa washabiki wa UKAWA na hivyo kuleta majibishano na mvutano huku wakizuiwa kulitoa.

Akiongea na wananchi walioshuhudia tukio hilo, Mwandishi wa habari hii aliambiwa kuwa wakati wa majibizano hayo, jiwe lilirushwa kutoka kusikojulikana na kuanguka kwenye Lori la wapambe wa Mangungu, na hivyo kuchochea majibizano, pamoja na kwamba jiwe hilo halikumgusa mtu yeyote.

Baada ya mvutano mkali, busara zilitawala na hatimaye wana CCM hao kuamua kutoliondoa bango hilo. Uamamuzi huu ulipelekea kivijana mmoja mfuasi wa UKAWA aliyekuwepo mahali hapo, Omari Mkonda, kushukuru kufikiwa kwa suluhisho hilo kwa kusema ”Alhamdulillah CCM hawajatoa bango letu.”

Shukrani hiyo ya sauti ilijenga tena chuki ya ghafla kati ya Mangungu na vijana wa UKAWA, kiasi kwamba, Mangungu aliamua kuchomoa Bastola yake kutoka mfukoni na kuanza kumtishia kifo Omari Mkonda. Wakati wa sakata hilo, Mangungu alisikika akitamba kwa kusema, ”Mimi sijapewa bastola kwaajili ya kuulia Nguruwe bali nimepewa kuulia watu watukutu.”

Hatimaye, Mangungu akisaidiana na wenzake walimshika Omari Mkonda na kumuingiza kwenye gari la Mangungu na kisha kumpeleka kusikojulikana. Taarifa zilizopatikana baadaye, zilionyesha kwamba, Omari Mkonda alishikiliwa kwa muda na watekaji hao kabla ya kupelekwa kituo cha polisi.

Siku ya pili baada ya tukio la kushikiliwa kwa Mkonda, yaani tarehe 23 Oktoba 2015 saa tatu usiku kijiji cha Mitole kilivamiwa na jeshi la Polisi wapatao 8 kutoka Wilayani.

Mapolisi hao walikwenda kwa Afisa Mtendaji wa Kijiji cha Mitole, Kimbwembwe, wakamtaka awaonyeshe wanakoishi vijana waliokuwepo kwenye orodha waliyokuja nayo polisi, orodha hiyo ikiwa na majina ya watu wapatao 50.

Vijana waliokamatwa siku hiyo ni Rifati Mnakatu (Katibu Chadema-Kata ya Mitole), Ali Matumla (Mwenyekiti Chadema -Kata ya Mitole), Fadhili Mbopo (mwanachama wa Chadema), Chande Hemedi Nyayo (mwanachama wa CUF).

Tangu siku hiyo, vijana hawa wamekuwa wakishikiliwa mahabusu na jeshi la Polisi huko Kilwa Masoko, makao makuu ya wilaya ya Kilwa. Kwa muda wa wiki mbili hawakupelekwa mahakamani.

Juhudi za kuwawekea dhamana zimefanyika mara kadhaa na viongozi wao wa vyama na ndugu zao bila mafanikio, huku polisi wakiwapiga danadana kwa madai kwamba jeshi la polisi limetingwa na shughuli za uchaguzi.

Kwa mujibu wa taarifa tulizozipata wakati gazeti hili linakwenda mitamboni, siku ya Ijumaa tarehe 6 Novemba 2015 vijana hao ndipo walipelekwa mahakamani kwa mara ya kwanza. Hata hivyo kesi haikusikilizwa. Shitaka dhidi yao ni Uporaji kwa kutumia silaha, shitaka ambalo liliwanyima haki ya kuwekewa dhamana.

Kamanda wa Polisi wa Wilaya ya Kilwa, Jastin E. Josephy, akiongea na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu alikiri kufikishwa kwa vijana hao polisi.

Alipoulizwa kwa nini waliwanyima vijana hao fursa ya kupatiwa dhamana ya kipolisi (police bail) kwa siku zote walipokuwa kituo cha polisi, alidai kuwa polisi walikuwa na kazi ngingi za uchaguzi.

Alipoulizwa kama vijana hao wamekwishafikishwa mahakamani alikiri, lakini akasema hawajapewa dhamani. Kamanda wa Polisi wa Wilaya ya Kilwa anadai dhamana ya vijana hao imezuiliwa kwa sababu “vijaa hao wanatuhumiwa kufanya kosa la uporaji kwa kutumia silaha,” kosa ambalo halina dhamana. Lakini, alikanusha madai kwamba, kushikiliwa kwa vijana hao ni suala la kisiasa.

Naye Murtaza Mangungu aliyekuwa mgombea kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM) ambaye anatuhumiwa kuwatishia wananchi bastola na kumteka nyara kijana Mkonda, akiongea na mwandishi wa gazeti hili kwa njia ya simu alidai kuwa vijana hao walikuwa wamevamia mkutano wake.

“Niliwaeleza vijana wale waliokuwa wamevamia mkutano wa kampeni kuwa wao wanarusha mawe nasi tukirusha risasi itakuwaje,” alisema Mangungu. Hata hivyo, alikanusha kuhusika katika kumteka nyara kijana Mkonda na kumtishia kifo kwa kutumia bastola.

Murtaza Mangungu ni Mbunge aliyemaliza muda wake katika Jimbo la Kilwa Kaskazini kupitia CCM. Katika uchaguzi mkuu uliomalizika hivi karibuni, Mangungu alishindwa kutetea kiti chake kwa kupata kura 16,503 huku mpinzani wake Vedasto Ngombale (CUF) akiibuka mshindi kwa kupata kura 16,724.

Wananchi wa Kilwa walioongea na gazeti hili wanamwomba Rais Magufuli kuingilia kati kwa kuwastaafisha kwa manufaa ya umma mapolisi wote walioshiriki katika kesi hii ya kubumba.
Benedict Kimbache

No comments:

Post a Comment