Saturday, November 14, 2015

MAALIM SEIF AZUGUMZA NA BALOZI WA EU NA VIONGOZI WA UKAWA

Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif Sharif Hamad, akiwa pamoja na viongozi wa UKAWA baada ya kikao cha mashauriano kilichofanyika Mikocheni jijini Dar es Salaam.

Na Hassan Hamad, OMKR

Katibu Mkuu wa Chama Cha Wananchi CUF Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, amerejea kauli yake ya kutotambua kufutwa kwa uchaguzi mkuu wa Zanzibar uliofanyika tarehe 25 mwezi uliopita.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam mara baada ya kikao cha mashauriano na viongozi wa Umoja wa Katiba ya Wananchi UKAWA, Maalim Seif amesema Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar Bw Jecha Salim Jecha hana mamlaka ya kufuta uchaguzi huo, na kinachohitajika na kuendelea na mchakato wa kuhakiki kura zilizobakia na mshindi kutangazwa.

Kuhusu tamko lililotolewa na serikali juu ya kufutwa rasmi kwa uchaguzi huo kupitia tangazo lililochapishwa kwenye gazeti rasmi la serikali tarehe sita mwezi huu, Maalim Seif amesema tamko hilo limekosa uhalali tangu lilipotolewa na Mwenyekiti wa ZEC.

Maalim Seif ambaye pia ni Mgombea Urais wa Zanzibar kupitia CUF amesema Chama chake hakijalizingatia tamko hilo na wala hakijadili uwezekano wa kurejewa kwa uchaguzi huo, kwa madai kuwa uchaguzi ulikamilika bila ya kuwepo malalamiko kutoka chama chochote cha siasa na wala Tume ya Uchaguzi.

Mapema akizungumza baada ya kikao hicho cha mashauriano, aliyekuwa mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chadema Mhe. Edward Lowassa amesema kikao hicho kilichojadili Mkwamo wa kisiasa Zanzibar kimekwenda vizuri.

Hata hivyo amesema ufafanuzi zaidi utatolewa Jumapili ijayo ambapo viongozi hao wanakusudia kuzungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.

Kabla ya kikao hicho Maalim Seif alifanya mazungumzo na Balozi wa Umoja wa Ulaya (EU) Bw. Filberto Seregondi katika hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam na kuelezea hatua zinazochukuliwa kukwamua mkwamo wa kisiasa Zanzibar.

Balozi Seregondi ambaye anamaliza muda wake wa utumishi hapa nchini,aliambatana na ujumbe wa waangalizi wa uchaguzi mkuu wa Tanzania kutoka Umoja huo.

Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif Sharif Hamad alipokutana na Balozi wa EU nchini Tanzania Bw.Filberto Seregondi pamoja na ujumbe wa waangalizi wa uchaguzi mkuu wa Tanzania kutoka EU huko hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam

No comments:

Post a Comment