Sunday, August 2, 2015

Lowassa aliipenda CCM Isiyompenda.

Na Bryceson Mathias
‘Je Tuseme Jiwe walilolikataa waashi, limekuwa Jiwe Kuu la Pembeni?’

KATIKA Gazeti hili (Tanzania Daima), Toleo Na.3729 Jumatano, Februari 18, 2015 kwenye Ukurasa wa Saba, lenye kichwa cha Habari ‘Kinana ana Upendeleo kwa Wagombea Urais CCM’!.

Kwenye Makala hiyo, niliandika nikionesha kuwa, hata Mteule wa Chama cha Mapinduzi (CCM), John Pombe Maghufuli, naye alianza Kampeni kabla ya wakati kama ilivyo kwa waliotuhumiwa akiwemo, Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Ngoyai Lowassa.

Baada ya Malalamiko ya Wananchi na Wadau kuhusu Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba, kudaiwa ameanza Kampeni akijificha kwenye Pazia la nafasi yake ya Kazi serikalini na Chama chake, CCM kupitia kwa Katibu, Abdulahman Kinana, alimwandikia, Nchemba, kusimamisha Ziara zake za CCM mikoani.

Hali hiyo haikulalamikiwa kwa Nchemba peke yake, lakini pia ilionesha Watia Nia wengi wa Urais ndani ya CCM ambao kwa ujumla walikuwa nyadhifa kubwa serikalini (Uwaziri), kwa namna moja au nyingine walitumia sana nafasi zao kufanya Kampeni zinazodaiwa.

Katikati ya Januari 18, 2015, kwenye Mitandao ya Kijamii, kuliwekwa Barua yenye Kumb. Na. CCM/OND/4 iliyokuwa ikienda kwa Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Mwigulu Nchemba, iliyokuwa na kichwa cha habari ‘KUSITISHWA ZIARA’ Iliyosomeka hivi;
“Umekuwa ukifanya ziara nyingi katika Mikoa na Wilaya bila ya ushirikishwaji kamili na Makao Makuu, Mikoa na Wilaya, na hasa Kamati za Siasa.
“Wewe pia umeonyesha kwa Kauli na Mienendo yako kujiandaa kugombea nafasi ya Urais kupitia CCM. Ziara hizi zina mwelekeo wa kampeni, jambo ambalo ni kinyume na maadili ya Chama.

“Nakuagiza kuzisitisha ziara zote. Iwapo utataka kufanya ziara yoyote ya kichama, itabidi kwanza uniarifu na upate kibali changu. Nakuagiza kutekeleza agzo hili mara moja” mwisho wa Nukuu.

Katika ziara hizo, Mwigulu alipoulizwa alijitetea akisema, kama Naibu Katibu Mkuu wa CCM, alikuwa akikagua Uhai wa Chama, na kutatua Kero Lukuki zinazowakabili watendaji, kutokana na Malalamiko mbalimbali yaliyokuwa yakitolewa na wananchi katika maeneo yao.

Mbali ya Watia Nia Sita wa Urais CCM akiwemo Lowassa, kupewa adhabu ya Kufungiwa Miezi Sita kwa madai walianza Kampeni kabla, kwa mujibu wa Sheria, hata Magufuli naye alikuwa ameanza harakati hizo kama walivyofanya wengine.

Ingawa, baadhi ya watetezi wanadai alikuwa hajatia Nia lakini tayari alikwisha tajwa kuwa mmoja wao, ingawa hakutaka kujionesha, lakini yeye aliachwa aendelee kutumia Nafasi yake ya kukagua Miradi ya Barabara, Kuzifungua, ikiwemo Mikutano na Semina za Watalaam, akihutubia wananchi nchi nzima.

Kama mtakumbuka vizuri, Machi 16, 2015 Makamu wa Rais Dk.Mohamed Bilal, alipokagua Mzani mpya na wa Kisasa kabisa Vigwaza, ambapo gari lisilozidisha litapima kwa sekunde thelathini badala ya dakika mbili akiwa na Magufuli akitoa taarifa, ilikuwa ni moja ya Turufu zake.
Kati ya 17-18 Mei, mwaka huu kwenye Semina za Watalaam wa Ujenzi (CPD) Mlimani City, Magufuli pia alikuwa na Fursa ya kuwa na Makandarasi, Wahandisi, Wasanifu Majengo nchini, ambapo semina hiyo iliyokuwa ifanyike Tanga, yeye kama Mkuu wa Wizara, aliibadilisha ikafanyika Tanga. Hivyo nakataa mtu anaposema wengine hawakufanya Kampeni mapema, tutoe haki, wote walifanya.

Kutokana na kile kilichofanyika Dodoma wakati wa uteuzi wa Mgombea Urais wa kupeperusha Bendera ya CCM dhidi ya Lowassa, ambapo yeye mwenyewe anasema, hakuamini kama kilichofanywa na chama chake, kimefanywa na CMM iliyomlea, hapo ndipo naamini, Lowassa aliipenda CCM isiyompenda isipokuwa Wanachama walimpenda.

Katika hali hiyo, ndiyo maana wadau wanasema, huenda Lowassa aliipenda CCM isiyompenda, kwa sababu, Turufu aliyotumia Magufuli kwamba anafanya Ukaguzi wa Barabara na Miundo Mbinu, haikuishia hapo, pia alitumia Mikutano ya Watalaam wa Mambo ya Ujenzi kujinadi, hivyo naye alianza Kampeni mapema kama wengine.

Lowassa aliuenzi Upinzani au Laa?.
Wasomi na Wadau wa Siasa, wamekuwa wakijiuliza maswali; Je, Lowassa kufikia kujiunga na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), aliuenzi upinzani? Tunapotafuta majibu hayo, basi hebu tushirikiane kwa pamoja bila kudhani alifanya hivyo kwa kuksa nafasi CCM.

Pamoja na Lowassa kutajwa kwenye Orodha ya Aibu ya Mafisadi kule Temeke Mwembe Yanga, hatukuwahi kusikia akilipiza Kisasi au kufanya Majibishano akipinga au kulumbana na taarifa za Shutuma zilizoelekezwa kwake.

Licha ya kuwepo majibishano mbalimbali Makali ndani ya Bunge kuwahusu Wapinzani, hatukuwahi kusikia akisimama na kuwaponda Wapinzani kuburuzana kwa ubishi, akiwararua au kuwagandamiza akikataa hoja zao.

Kwa muda wote, Lowassa tangu ajiuzulu Uwaziri Mkuu, alikaa kimya kama Mtu anayetunga Sheria, na kwa nyakati tofauti vyombo vya habari na Wananchi walishangaa sana na ukimya wake huo, na kutafsirika kwa mambo mengi dhidi yake.

Kwa mtazamo huo, ndipo ninapohitimisha Mjala wa Swali la Lowassa aliuenzi Upinzani au Laa? Mimi nasema aliuenzi, maana kwa maelezo machache ya awali hapo juu, inaonesha hata siku moja hakuwahi, kuwasema vibaya wapinzani wala kuwang’ong’a au kuharibu mipango yao, hivyo aliuenzi upinzani! .

Na kwa namna hiyo, sioni kama kuna mikwaruzo yoyote ambayo, Lowassa inaweza kumsumbua atakapokuwa ndani ya Chadema, ingawa kuna baadhi ya watu wanaweza kupata taabu kutokana na walivyomtafsiri au kumsema, jambo ambalo wanaweza kusameheana tu aana ni katika vita ya siasa!.

Sasa hivi kumetokea maneno na minong’ono mingi kwamba, Katibu Mkuu wa Chadema, Dkt. Wallboard Slaa, amejiuzulu nafasi yake na amekabidhi Kadi ya Chama hicho, na kwamba eti anakwenda Chama cha ACT-Wazalendo akiwemo, John Mnyika, kwa kuwa hawaridhiki kupokewa kwa Lowassa.

Bado sipingani wala kukubali Taarifa za vyombo vya habari hivyo kwenye gazeti lake la kila siku la Ijumaa na Jumamosi hivi karibuni, ila nakubali kutokukubaliana. Nasema hivyo kwa sababu, yote yanaweza kutokea kama vile Lowassa ilivyotokea kuhamia Chadema.

Ninachofahamu mimi, Slaa na Mnyika waliipenda Chadema na Wanachama wake, ambao nao waliwapenda, kama kweli, Slaa na Mnyika wanaipenda Tanzania, na wanaumizwa na Adha wanayopata Watanzania kila kukicha, kiasi wanakosa hata Mulo wa siku moja, kwa busara zao hawezi kushindwa kujitokezaw auambie Umma ukweli, maana wao ni wa kweli!

Akifika mahali penye hisia za namna hiyo, huo ni Mshindo na Mwanguko wa Tembo kisimani ambapo, Samaki wadogo na Wakubwa, Chura na wanyama wengine majini, watakufa kutokana na Uzito wa Mnyama huyo.

Ninachosema, ‘Mungu Ibariki Tanzania………………………”

0715933308

1 comment:

  1. Umesema kweli, Makamanda hawa wajitokeze na kuuambia umma kulikoni, Dr. Slaa na John Mnyika, jitokezeni ili ukweli uwe wazi.

    ReplyDelete