Friday, June 26, 2015

KINABO WA CHADEMA TISHIO KIBAHA VIJIJINI; Arudisha rasmi ya fomu ya ubunge leo!

Na Mwandishi Wetu, Kibaha
HATIMAYE, Mjumbe wa Baraza Kuu Mstaafu na kada maarufu wa Chadema katika jimbo la Kibaha Vijijini, Kinabo Edward Kinabo, amerudisha fomu leo katika Ofisi za Chadema Jimbo la Kibaha Vijijini mjini Mlandizi, akiomba ridhaa ya chama chake ya kuwania ubunge wa Jimbo hilo katika uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba 25 mwaka huu.

Kinabo, mzaliwa wa kijiji cha Ruvu Stesheni na mwenyeji wa jimbo hilo, ni mwanaharakati wa maendeleo ya vijana na wanawake akiwa na uzoefu wa kufanya kazi na mashirika mbalimbali yasiyo ya kiserikali yenye hadhi ya kitaifa na kimataifa kwa muda mrefu.

Mwanasiasa huyo aliyesomea siasa na uongozi Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, amewahi kufanya kazi za kusaidia wabunge wa kambi ya upinzani Dodoma katika uandaaji wa hoja,maswali na hotuba za mawaziri vivuli wa upinzani mara kadhaa.

Pia amewahi kuwa mwanahabari mwandamizi na mchambuzi wa masuala ya kisiasa katika gazeti la Tanzania Daima

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kukabidhi fomu ya ubunge, mwanasiasa huyo kijana (34) aliyekuwa moja ya nguzo muhimu katika kufanikisha ushindi wa mbunge wa sasa wa Ubungo, John Mnyika, alisema dhamira yake ni kuleta uwakilishi mpya wenye kujali matakwa na maslahi ya watu wa jimbo hilo na kuhakikisha anakwenda kuishauri na kuibana vizuri serikali katika kutenga na kusimamia fedha nyingi za miradi ya maendeleo ambazo zimekuwa hazitumiki vizuri kufanya kazi iliyokusudiwa.

Aidha, alisema amedhamiria kuwatetea wananchi wengi wa jimbo hilo wenye kilio cha ardhi, kwani jimbo hilo limegeuzwa kuwa shamba la Bibi kwa vigogo wa CCM na matajiri wachache wenye uswahiba mkubwa na chama hicho kujitwalia kiholela sehemu kubwa ya ardhi na kuibakisha bila kuiendeleza, huku wananchi maskini wa jimbo hilo wakipungukiwa maeneo ya makazi na kilimo.

Aliongeza kuwa kwa miaka mingi wabunge na madiwani wa CCM wameshindwa kuboresha huduma za kijamii, hasa kutokujenga zahanati, kutoboresha miundombinu ya kielimu mashuleni na kushindwa kusukuma miradi ya maji na umeme vijijini, licha ya kuwepo bajeti ambayo ingetosha kuwapunguzia wananchi kero hizo.

"Kwa mfano, Mbunge wa sasa na madiwani wa CCM wakati wanaingia madarakani miaka mitano iliyopita, walikuta zaidi ya vijiji na vitongoji vya mamlaka ya mji mdogo 17 vikiwa havina zahanati, leo muda wao unakwisha wameshindwa kufanikisha ujenzi zahanati wa hata moja. Wananchi maskini wanateseka kusafiri umbali mrefu na kwa gharama kubwa kufuata tiba kwenye kituo kimoja cha afya cha hapa mjini Mlandizi, hali hii haivumiliki, wakati wa Kibaha Vijijini kupata mbunge makini, jasiri na mwenye uwezo wa kutosha kuwatetea na kusukuma maendeleo yao umefika, nimejitokeza kuwa mbunge wa aina hiyo, nataka kuwa faraja ya mama zangu wa jimbo hili, ya vijana wenzangu wa jimbo na wazee wa jimbo hili. Yote yalishindikana ndani ya jimbo hili chini ya wabunge na madiwani wa CCM,yanawezekana chini ya Kinabo wa Chadema na UKAWA. Nasubiria ridhaa ya chama changu", alisema mwanasiasa huyo.

Kinabo alitumia fursa hiyo kuitangaza kauli mbiu yake ya kampeni inayosema "Kinabo Atosha Kibaha Vijijini; Yaliyoshindikana, Yanawezekana"

Hali ya kisiasa ndani na nje ya Chadema jimboni hapa, inaonyesha kuwa Mwanasiasa huyo ndiye anayepewa nafasi kubwa ya kupita kwenye kinyang'anyiro cha kura ya maoni kutokana na kufanya kazi kubwa ya kukiimarisha chama hicho jimboni hapa na kuvuta hisia za wananchi wengi wa vijijini na ndani ya Mamlaka ya Mji Mdogo wa Mlandizi kwa kujenga hoja nzito katika hotuba zake na zinazoonekana kufanyiwa utafiti wa kina.

Wanachama wengine wa chama hicho waliojitokeza kuomba ridhaa ya kuwania ubunge wa chama hicho ni Dr Rose, Eli Achahofu, na Edita Babeiya.

2 comments:

  1. Anaweza, na kutufaa huyo, wana wa KIBAHA TUMPIGIE KURA JEMBE LETU HUYU..

    ReplyDelete
  2. Anaweza na kutufaa sana. Kibaha vijijini kama twaitaji mabadiliko ya kweli, yataletwa na mmoja tu nae si mwingine ni KAMANDA KINABO

    ReplyDelete