Saturday, May 30, 2015

ZIARA YA KATIBU MKUU DK. WILLIBROAD SLAA


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
ZIARA YA KATIBU MKUU DK. WILLIBROAD SLAA
Kupitia taarifa hii kwa vyombo vya habari Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kinapenda kuujulisha umma wa Watanzania kuwa Katibu Mkuu, Dk. Willibroad Slaa atafanya ziara ya kikazi katika maeneo mbalimbali ya mikoa ya Mbeya, Rukwa na Katavi, ambapo atakuwa na shughuli kadhaa, ikiwemo kukagua mwenendo wa uandikishaji wa wapiga kura unaofanyika kwa mfumo wa Biometric Voters Registration (BVR).
Katika ziara hiyo ya siku 6 kuanzia Jumamosi ya Mei 30, 2015, Katibu Mkuu Dk. Slaa mbali ya kujionea zoezi hilo la BVR katika vituo vya uandikishaji, atafanya mikutano ya hadhara kwenye maeneo yote atakayozuru ambapo atazungumza na wananchi juu ya masuala yanayowahusu katika maeneo yao pamoja na mengine ya kitaifa.
Kupitia shughuli hizo atakazofanya, Katibu Mkuu ataendelea kuwahamasisha Watanzania wenye sifa za kupiga kura, kujiandikisha kwa wingi katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura (DKWK) linalofanyika maeneo mbalimbali nchini kwa kutumia mfumo wa BVR.
Aidha, Katibu Mkuu Dk. Slaa atatumia fursa hiyo kukagua shughuli mbalimbali za chama zinazofanywa na viongozi na watendaji wa CHADEMA katika kanda za chama; Kanda ya Nyanda za Juu Kusini ambayo inajumuisha mikoa ya Mbeya, Iringa, Njombe, Ruvuma Rukwa pia Kanda ya Magharibi yenye mikoa ya Kigoma, Tabora na Katavi.
Katibu Mkuu pia atapata fursa ya kukutana na viongozi na watendaji wa chama wa ngazi za chini katika kanda hizo na kusikia kutoka kwao namna wanavyoendelea kutekeleza programu na mikakati waliyojipangia katika maeneo yao au kuelekezwa na vikao vya chama, ikiwa ni sehemu ya kuzidi kukiandaa chama na UKAWA yaani vyama vinne (NLD, NCCR-Mageuzi, CUF na CHADEMA), kushinda uchaguzi mkuu wa mwaka huu.
Ratiba ya ziara ya Katibu Mkuu Dk. Slaa itakuwa kama ifuatavyo;
1.      Jumamosi Mei 30, 2015 - Mbozi (Vwawa) atafanya mkutano wa hadhara Uwanja wa Ichenjezya.

2.      Jumapili Mei 31, 2015 – Tunduma- Mbeya, atafanya mkutano wa hadhara katika Uwanja wa Shule ya Msingi Tunduma.

3.      Jumatatu Juni 1, 2015 – Sumbawanga- Rukwa, atafanya mkutano wa hadhara Uwanja wa Stendi ya Chanji, mjini Sumbawanga.

4.      Jumanne Juni 2, 2015 – Mpanda Mjini- Katavi, atafanya mkutano katika Uwanja wa Kashaulili.
Itakumbukwa kuwa Katibu Mkuu Dk. Slaa alifanya ziara ya siku 3 hivi karibuni katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Kagera ambako alishuhudia udhaifu na mapungufu makubwa katika uandikishaji wa BVR, ikiwemo wananchi kutishwa, kupigwa, kuzuiwa kujiandikisha na viongozi wa CCM wakiwa vituoni, mashine kutofanya kazi, siku za kuandikishwa kutojulikana na uandikishaji kufanyika ‘electronically na manually’ bila maelezo yoyote kutoka Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC).
Imetolewa leo Ijumaa, Mei 29, 2015 na;
Tumaini Makene
Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano
CHADEMA


No comments:

Post a Comment