Thursday, April 16, 2015

Mwenyekiti wa Chadema akamatwa na Polisi.

Na Bryceson Mathias, Kilosa, Morogoro
MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Tawi la Mbigiri Wilaya ya Kilosa, mkoani Morogoro, Maftaha Hamisi Shabani, amekamatwa na Polisi Dumila, bila kuelezwa ana Kosa gani.

Akizungumza na Tanzania Daima, Katibu wa Tawi hilo Mohamed Ami, amethibitisha Mwenyekiti wake, Shabani, kukamatwa na Polisi akiwa Dumila, na kwamba, wengine waliokamatwa kabla yake ni Pamoja na Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji hicho, Hemed Salum (CCM).

“Ni kweli Mwenyekiti wa Chadema Mbigiri (Shabani) amekamatwa na Polisi akiwa matembezini Dumila, na wengine waliokamatwa naye ni Mtendaji wa Mbigiri, Jacb Mvungi, ambapo makosa yao bado hayajawekwa wazi, isipokuwa dhamana yao .

Imedaiwa mapema siku ya nyuma yake, Wafugaji wa Jamii ya Kimasai waliingiza Makundi ya Ng’ombe kwenye Mashamba ya Wakulima katika Kijiji cha Mbigiri, ambapo Wakulima wa Mbigiri walipoziswaga Ng’ombe hizo ili kuilalamikia Polisi kwa uharibifu, kibao kimewageukia.

Imeelezwa baada ya Wafugaji hao kukimbia na kuacha Ng’ombe, ghafla walitokea polisi na kuanza kuwakamata Viongozi wa Kijiji cha hicho wakiwemo Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji, (Salum na Mtendaji Mvungi), ambapo alifuatia Mwenyekiti wa Chadema Shabani.

Habari zingine zinadai, Viongozi na baadhi ya Wana Kijiji cha Mbigiri walipokwenda Polisi kutaka kuwawekea Dhamana ndugu zao, badala ya kutoa Dhamana, Polisi walikuwa wakiwakamata na kuwaweka ndani, jambo lililowafanya Wananchi kuogopa kwenda.

OCD wa Kituo cha Polisi cha Dumila, Jafari Rashid Kiyoga, alipoulizwa juu ya tukio hilo, alikataa kusema lolote akidai si Msemaji ila Kamanda wa Polisi mkoani Morogoro, Leonard Paul, ambapo hakupatikana kwa simu hadi tunakwenda mitamboni.



Wananchi na Viongozi wa Mbigiri bila kujali itikadi zao, wamelilalamikia Jeshi la Polisi wakidai, limekuwa Jeshi la Wafugaji wilani Kilosa na Mkoa, limekuwa na Upendeleo wa upande mmoja, ambapo Wafugaji wakilisha Ng’ombe mazao yao, wakiambiwa hawashughuliki, ila wanapochukua hatua za kuswaga Ng’ombe kama ushahidi ili wawashitaki, nguvu kubwa ya Polisi inatumika kwao.

No comments:

Post a Comment