Friday, April 24, 2015

Mnyika awaasa wanachama Chadema kuacha makundi.

Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Tanzania Bara, John Mnyika (pichani), amewataka wanachama wa chama hicho wilayani Tarime kuachana na makundi yanayosababisha kukigawa Chama.

Akihutubia katika mkutano wa hadhara uliofanyika uwanja wa Sabasaba mjini Tarime na kuhudhuriwa na umati wa wananchi, Mnyika alisema kuwapo makundi kunasababisha Chama kugawanyika hivyo kudhoofisha nguvu zake.

Aidha, aliwapongeza wananchi wa wilaya hiyo kwa kufanikisha chama hicho kunyakua viti vingi katika uchaguzi wa serikali za mitaa uliofanyika Desemba 14, mwaka jana katika nafasi za uenyekiti wa mitaa, vijiji na vitongoji pamoja na wajumbe.

“Pamoja na kuwapongeza huko, lakini nawaomba wananchi mjitokeze kwa wingi kujiandikisha katika daftari la kudumu la wapigakura muda utakapowadia,” alisema Mnyika.

Naye Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (Nec), John Heche, aliwaasa wana-Tarime wawe na mshikamano wa kushirikiana kuleta maendeleo kwa kupiga vita maadui watatu ambao ni umaskini, ujinga na maradhi huku akichukua nafasi hiyo kujitangaza kuwania nafasi ya ubunge Jimbo la Tarime.

No comments:

Post a Comment