Monday, April 13, 2015

Mbowe:Niko tayari kumkabili yoyote CCM kiti cha ubunge

Mwenyekiti wa Taifa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe, amesema yupo tayari kumkabili mwanachama yeyote wa Chama cha Mapinduzi (CCM), atakayejitokeza hadharani kupimana nae ‘ubavu’ kwenye kiti cha ubunge wa jimbo la Hai, mkoani Kilimanjaro katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu.

Mbowe, alitangaza nia hiyo juzi katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Mamlaka ya Mji mdogo wa Bomang’ombe uliopo wilayani hapa, muda mfupi baada ya kukabidhi magari mawili ya kubeba wagonjwa, aina ya Toyota Hiace, yenye thamani ya Sh. milioni 176.

“Kama anaweza kutokea mwanachama wa CCM, akasema anaweza kusaidia maisha ya wananchi, msimbeze, mpokeeni…Akija niachieni, nitashughulika nae; na wala siku ya kuomba kura, sitaomba kura kwa magari haya, ila nitaomba kwa mdomo.

Kama yupo anayefikiri nitatumia misaada hii kuomba kura katika uchaguzi ujao ni mwendawazimu peke yake,” alisema Mbowe.

Miongoni mwa makada wa CCM wanaotajwa kuwania kiti hicho ni pamoja na Mbunge wa zamani, Fuya Kimbita, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Meru, Danstun Malya na Katibu wa chama hicho Wilaya ya Monduli, mkoani Arusha Elisante Kimaro.

Mbowe aliwaeleza wananchi hao kwamba baada ya wiki mbili, atakabidhi tena kwa Halmashauri ya Wilaya ya Hai, lori aina ya Mercdez Benz lenye thamani ya Sh. milioni 100, lenye uwezo wa kubeba tani 25 za takataka.

Aliwaasa wakazi wa jimbo hilo, kutokubali kuingiza masuala ya siasa kwenye maisha ya watu; kwa vile alichokifanya yeye ni kutekeleza ahadi yake ya kutafuta magari ya kubeba wagonjwa katika Hospitali ya Wilaya ya Boma na Hospitali Teule ya Machame ya Nkwarungo.

“Kwa sababu tu ya itikadi za kisiasa, serikali imeyatoza kodi, magari haya ya kubeba wagonjwa pamoja na hilo lori la kubeba takataka ambalo linakwenda Halmashauri ya Wilaya.

Nimewaomba msamaha wa kodi kwa miezi mitatu wamekataa; ikanibidi nilipe shilingi milioni 27 za ushuru na Bima, kwa magari mawili ya wagonjwa na lori la taka; nimeambiwa niilipe Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), zaidi ya shilingi milioni 30,” alisisitiza Mbowe.

Akikabidhi magari hayo kwa Mkuu wa Jimbo la Hai la Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Kaskazini, inayoendesha Hospitali Teule ya Machame, Mchungaji, Asanterabi Swai na Mganga Mkuu wa Wilaya ya Hai (DMO), Dk. Paul Chawota, Mbowe alionya magari hayo yasitumike vibaya kutokana na maelekezo ya wanasiasa au kutelekezwa kwa makusudi badala ya kutoa huduma kwa walengwa kwa sababu ya itikadi zao.

No comments:

Post a Comment