Monday, March 9, 2015

WANANCHI WA JIMBO LA KILWA KASKAZINI WATAKIWA KUACHANA NA CCM

Akizungumza na wanakijiji wa Njianne huko Kilwa Kasimu Bingwe Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Mtwara na Kaimu mwenyekiti wa Kanda mpya ya Kusini inayojumuisha mikoa ya Lindi na Mtwara alisema Tanzania haipo huru kama tunavyoaminishwa, maana ya uhuru ni wananchi wananchi kufaidi matunda ya rasilimali zake. Bingwe aliwatahadharisha wananchi kutoikumbatia CCM kwani kwa kufanya hivyo hawatapata uhuru wa kweli. “Tusichukue nchi tukawa kama mabwana” alitoa kauli hiyo kwa kumnukuu baba wa Taifa.

Bingwe alionyesha masikitiko yake kwa uongozi uliopo madarakani unaotawala kwa mithiri ya utawala wa kikoloni. Alisema leo hii ni tofauti kabisa kwani pamoja na kuwa na viongozi watanzania, wenye ngozi nyeusi, utawala wao ni zaidi ya utawala wa wakoloni.

Sisi vyama vya upinzani tumesingiziwa mambo tofauti tofauti, ikiwa ni pamoja na kuitwa wahuni, sisi sio wahuni na wananchi wa Njianne msiyumbishwe kwa hilo kwani hata baba wa Taifa alipatwa kuitwa mhuni, lakini hao hao waliomuita muhuni ndio waliompokea kwa shangwe tulipopata uhuru.

Bingwe akitoa mfano alisema Chadema ni sawasawa na mti wa mwembe unopigwa mawe kwa sababu ya matunda yake.

Katika ziara hiyo alisikitika kuona watanzania wanaendelea kuikumbatia CCM, alihoji kwa nini waendelee kuipa CCM nafasi ya kuendelea kuwepo madarakani wakati wanafahamu wamegeuzwa ndondocha na misukule. Watanzania tusikubali kumilikiwa na CCM kwani haina haki miliki.

“Kupungukiwa akili unapozaliwa na hivyo kuwa na upungufu wa akili ni mpango wake Mungu, kupungukiwa na akili za kujitambua na hivyo kuendelea kuwa masikini kwa sababu za kuikumbatia CCM huo ni upumbavu wako mwenyewe, na wala sio mpango wa Mungu” alisema.

Kuishi Tanzania sio laana, nchi hii tumebarikiwa sana na ardhi mzuri yenye rutuba isiyohitaji mbolea, lakini maisha ya watu wetu ni magumu sana na hii yote imetokana na kuikumbatia CCM, isiyowakwamua na kuwawezesha wakulima.

Kiongozi huyo alisikitishwa na hali ya umeme kukatikakatika katika Wilaya ya Kilwa, alishangazwa inakuwaje umeme ukatike pamoja na kuwa na chanzo cha uhakika wa umeme wa gesi ya Songosongo. Ukatikaji huu wa umeme ni hatari sana hasa kwa hospitali kwani inaweza kupelekea mgonjwa kupoteza maisha endapo anahudumiwa kwa kutumia vifaa vinavyotumia umeme, pia ukatikaji huu wa umeme unaathari kubwa sana kiuchumi ikiwa ni pamoja na wawekezaji kusita kuwekeza katika maeneo hayo, alisema.

Juzi nilikuwa Kata ya Mitole, nimesikitishwa sana kwani pale pachani kuingia Mitole ukiacha barabara kuu inayotoka njinjo kwenda Nangurukuru nilikutana na mzee mmoja anayeonekana hana hata uhakika wa kesho yake itakuwaje, mzee huyu anaishi kwenye nyumba ambayo ameshindwa hata kuezeka nyasi kujikinga na jua na mvua, chakushangaza kwenye nyumba hiyo ametundika bendera ya CCM, chama kilichomfikisha kwenye hali aliyokuwa nayo.



Tusipumbazwe ni barabara iliyokamilika. Huu sio mwisho, kwani tuliowengi kwa vile hatujawahi kuona barabara ya lami kabla, tunafikiri kuwa serikali imetufanyia jambo kubwa sana na hivyo kuridhika na kutofikiri tulipaswa kufanyiwa mazuri na makubwa zaidi ya barabara.

Chadema haibahatishi, viongozi wa Chadema wana uzalendo wa kweli na leo tumekuja kwenu kuwaunganisha watanzania wote ili kuleta ukombozi wa kweli. Wote kwa pamoja naomba tulipiganie na tulitetee taifa letu. Naomba wanachi wote tujiunge na vyama vya upinzani vinavyounda UKAWA na tusiogope kuitwa wachochezi.

Akizungumza kuhusu wananchi wa Kilwa Kaskazini kutojitambua alisema, “ninasikitishwa sana kwa nini hamjitambui, kama Kinjeketile aliyewapa matumaini na kuwatia hamasa wapiganaji wa vita vya Majimaji vilivyoanzia kule Nandete Kipatimu alijitambua kwa kutumia uganga wake ili kuwaadabisha Wajerumani wakati hakuwa na elimu yoyote, iweje nyie ambao angalau mumesoma mpaka darasa la saba mmeshindwa kujitambua?”

Naomba mjiunge na Chadema, tunahitaji wenye dhamira ya dhati kujiunga na chama chetu. Chama hiki kimefika hapa kilipo kwa utayari na utendaji wa wanachama na wapenzi wake bila ya kutafuta maslahi yao binafsi, ndani ya Chadema hakuna fedha bali kuna fikra. Binafsi nimeacha mambo yangu binafsi, nimeacha biashara zangu na kuamua kujitoa muanga ili kuitetea Nchi yangu kupitia Chadema, unapojiunga na chama hiki unapaswa kukubali kujitoa, kutumia muda wako, kukubali kuteseka kwa manufaa ya Taifa letu na vizazi vyetu.

Tunachowahubiria leo tunaomba mtusikilize na kutuelewa, ninasikitika watanzania wana macho lakini hawaoni, wanamasikio lakini hawasikii sijui kwanini. Kwanini msitambue kuwa CCM imeshindwa na hali halisi inajionyesha, huna haja ya kuambiwa tazama. Tufikie wakati tufanye maamuzi, kwa nini msijaribu kuiweka UKAWA madarakani, ni swala la kuamua tu unaiweka Chadema madarakani ikishindwa ‘unapiga chini’, safari nyingine unaweka CUF ikishindwa ‘unapiga chini’, safari nyingine unaweka CCM ikishindwa ‘unapiga chini’.

Huko kata ya Kinjumbi Bingwe alisema Kuna propaganda nyingi zinaenezwa dhidi ya Chadema na dhidi ya vyama vingine vya upinzani, kwamba endapo vitaingia madarakani basi vitasababisha vita. Huu ni uongo, na nyinyi wenyewe ni mashahidi kwani hapa mwenyekiti wenu wa Kijiji ni wa CUF naomba niulize kama kuna vita yeyote imewahi kutokea.



Tusiikumbatie CCM inayowapa rushwa wakati wa uchaguzi, wanapoleta fedha zao tusione dhambi kuzichukua lakini tuone dhambi kuwapigia kura.

Akizungumza kuhusu zoezi la kujiandikisha kwenye daftari la kudumu la wapigakura Bingwe aliwataka wananchi wa Kinjumbi kujitokeza kwenye zoezi hilo kwa kuwataka kuwa wa kwanza kujiandikisha.

Kuna uwezekano mkubwa wa kuwaondoa CCM endapo tutatumia umoja wetu, sioni sababu kwa nini historia isijirudie, kama tuliweza kuwaondoa Waarabu, Wajerumani, Waingereza ili kuwa na utawala wa wenyeji kwa nini tusiwaondoe CCM? Kama wakoloni tuliowaondoa wamebaki kwenye vitabu vya historia kama kumbukumbu kwa jinsi hiyo hiyo tunapaswa kuhakikisha CCM inabaki kwenye vitabu vya historia.

Naye Mfaume Ngajulage, Mwenyekiti wa Chadema (W) Kilwa, akihutubia huko Somanga alisema wananchi wasiyumbishwe kwa propaganda za CCM, alisema kuwa wao sio wapinzani bali ni wanaharakati, alisema hivyo kutokana na hoja inayosemwa na CCM kuwa vyama vya upinzani vinapinga kila kitu.

Mfaume mtoto wa aliyekuwa Mbunge wa Liwale 1995-2000 kupitia tiketi ya CCM aliwataka wananchi kutolala kwa kusema wasiridhike na kubweteka baada ya kula maboga na kukaa nyumbani, maisha ni zaidi ya kula maboga na kuridhika, maisha ni maji safi na salama, maisha ni huduma bora za afya, amani n.k. “CCM ni mzigo, naweza kuifananisha na mzigo wa mavi na mzigo wa misumari, Ukibeba gunia la misumari kichwani hata ukirekebisha vipi mzigo huo wa misumari utaendelea kukuchoma, pia ukibeba gunia la mavi hata ukigeuza vipi mavi yataendelea kukuchuruzikia” alisema.

Tumefika hapa tulipo kwa sababu ya CCM, huku akitumia lugha ya kiarabu “Laana tu-Llwah” akimaanisha CCM ilaaniwe, Ngajulage alisema. “Ninashangazwa na wananchi wanaoiunga CCM mkono, pamoja na kuwaambia madhambi ya CCM lakini kuna wenzetu wameendelea kuikumbatia, hii ni sawasawa na kuambiwa msichana X ana ukimwi na amemaliza kijiji kizima na wewe ukamfuata, huo ni upunguani. Alisisitiza pia umuhimu wa UKAWA kwa kusema kwamba ushirikiano uliopo sio wa kinafiki, endapo ndani ya ukawa kuna kiongozi hatawajibika na atatukwamisha tutamuondoa. Lengo letu ni kuhakikisha Halmashauri ya Kilwa inaongozwa na UKAWA kwenye uchaguzi mkuu ujao na sio vinginevyo.



Naye Mohammed Maadhi Katibu wa Chadema (M) wa Lindi alisikitishwa na ufisadi katika Halmashauri ya Kilwa, moja ya ufisadi huo ni pamoja na madeni inayodaiwa na TASAF, madeni yanayotokana na Halmashauri ya Kilwa kutotumia vizuri fedha ilizopewa kwa hizo hazikufanya kazi iliyokusudiwa hivyo TASAF kulazimika kuidai halmashauri kurudisha fedha hizo na kuifanya halmashauri kila inapopata fedha kulipa deni la TASAF.

Kamanda Benedict Kimbache​(Mlezi wa CDM -Jimbo la Kilwa Kaskazini)​na Kamanda Mohamed Maadhi(Katibu wa CDM (M) Lindi, ​wakiwa kwenye picha ya Pamoja
Kamanda Kimbache akiwahutubia wananchi wa Kinjumbi-Kilwa

Makamanda wakila kwa wenyeji huko Njinjo Kilwa, wakiwa kwenye Operesheni Tokomeza CCM Kilwa Kaskazini.

Picha ya Juu na Chini -Wananchi wa Njianne-Kilwa Kaskazini wakijipanga kusubiri card za uanachama wa Chadema


No comments:

Post a Comment