Tuesday, March 17, 2015

Mkakati wa Chadema kuingia Ikulu

Siku moja baada ya katibu mkuu wa Chadema, Dk Willbrod Slaa kuwataka Watanzania wajiandae kwa “Serikali Mpya” aliyodai itapatikana Oktoba 31 baada ya Uchaguzi Mkuu, gazeti la Mwananchi limebaini mkakati wa ushindi unaopangwa na chama hicho cha upinzani.

Hadi sasa, Chadema ndio chama kinachoongoza kwa upande wa upinzani kulingana na matokeo ya Uchaguzi Mkuu uliopita na wa Serikali za Mitaa uliofanyika mwishoni mwa mwaka jana, na inaonekana kujipanga kupaka mafanikio makubwa zaidi mwezi Oktoba.

Katika Uchaguzi Mkuu wa 2010, mgombea wa CCM, Jakaya Kikwete alishinda kwa kupata asilimia 61.17, ikiwa ni pungufu ya asilimia 20 ya kura alizopata mwaka 2005, wakati Chadema ilimsimamisha Dk Willbroad Slaa aliyepata asilimia 26.34 akiwa anasimama kwa mara ya kwanza.

Huku CCM ikiwa katika mchakato mgumu wa kumpata mrithi wa Kikwete uliogubikwa na adhabu dhidi ya makada wanaotajwa kutaka nafasi hiyo, Chadema iliweka mkakati wake katika kikao cha Kamati Kuu kilichofanyika Januari mwaka huu.

Kwa mujibu wa habari ambazo Mwananchi imezipata, chama hicho kimelenga pamoja na mambo mengine kupeleka madaraka kwenye ngazi ya kanda badala ya mambo yote kutegemewa yafanywe na makao makuu.

Chadema, habari hizo zinasema, imeunda kanda 10 ambazo ni Kanda ya Serengeti, inayoundwa na mikoa ya Simiyu, Shinyanga na Mara, Ziwa Victoria (Geita, Mwanza, Kagera), Nyanda za Juu Kusini (Rukwa, Mbeya, Njombe, Ruvuma, Iringa), Kanda ya Kusini (Lindi na Mtwara).

Nyingine ni Kanda ya Kati (Singida, Dodoma na Morogoro), Kanda ya Kaskazini (Tanga, Kilimanjaro, Arusha na Manyara), Kanda ya Magharibi (Tabora, Katavi na Kigoma), Kanda ya Pwani (Temeke, Ilala na Kinondoni), Kanda ya Unguja(Kusini Unguja, Kaskazini Unguja na Mjini ) na Kanda ya Pemba (Kusini Pemba na Kaskazini Pemba).

Kanda hizo zitawezeshwa kwa mafunzo na kiuchumi ili kuzijengea uwezo wa kushughulikia mambo yake, hasa wakati wa uchaguzi bila ya kutegemea ofisi kuu.

Kwa mujibu wa habari hizo, kanda hizo pia zinazindua vikundi vyake vya ulinzi, ambavyo kazi kubwa inaonekana itakuwa ya kulinda kura ili kukabiliana na tatizo kubwa la upungufu wa rasilimali watu wakati wa Uchaguzi Mkuu.

Pia kuundwa kwa Mabaraza ya Uongozi ya Kanda kutawezesha mashauri mengi kwenye ngazi ya mikoa kutatuliwa bila ya kutegemea ofisi kuu.

Tayari mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe ameshafanya ziara kwenye baadhi ya kanda na kufanya vikao na Mabaraza ya Uongozi ya Kanda kuyashirikisha mikakati hiyo, sambamba na kuzindua vikundi vya ulinzi.

Lakini alipoulizwa kuhusu mpango huo, Mbowe hakutaka kuwa bayana.

“Sasa nikiweka wazi mikakati yetu, si itakuwa kama nimewauzia wengine. Hapana siwezi kuiweka wazi ila tunajipanga kuelekea Uchaguzi Mkuu,” alisema Mbowe, ambaye pia aligombea urais mwaka 2005 wakati Kikwete akiingia Ikulu kwa mara ya kwanza.

Lakini mtu aliye karibu na uongozi huo wa Chadema alikiri kuwapo kwa mkakati huo.

“Unajua mkakati huo unakwenda sambamba na kutoa mafunzo kwa viongozi mbalimbali wa chama kuanzia ngazi ya chini kabisa,” alisema akiomba jina lake lisitiriwe.

“Tunataka kanda hizi ziwe na uwezo wa kupambana na si kusubiri kila jambo kutoka makao makuu.” Taarifa zaidi zinaeleza kuwa ziara hizo za Mbowe pia zinalenga kufanya maboresho ya kiutendaji ikiwa ni pamoja na viongozi wa chama hicho kupewa mafunzo maalum na mbinu mbalimbali. “Chama kimebaini kuwa ili kushinda, hakiwezi kupambana na adui kutoka sehemu moja tu, ni lazima kiwe nchi nzima.

Hilo tumeliona katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa,” alisema mtoaji habari huyo. “Kinachofanywa sasa ni kuhakikisha kuwa kila kanda inakuwa na nguvu ya kufanya mambo yake yenyewe.

Yaani kila kanda itaweka mkakati wake wa kukiimarisha chama na kukabiliana na misukosuko yote ya kisiasa. Makao makuu ya chama yatakuwa yakitoa maelekezo tu.” Jumamosi iliyopita, Dk Slaa alisema katika mkutano wa hadhara uliofanyika Isaka wilayani Kahama kuwa nchi haina budi kujiandaa kwa serikali mpya.

Alisema Chadema itashika nchi kwa kuwa wananchi wamechoshwa na serikali iliyopo sasa ya CCM, kwamba ili kuongeza nguvu za kuking’oa chama hicho kikongwe, wananchi wanapaswa kuunga mkono juhudi za Ukawa.

Dk Slaa, ambaye aliwahi kuwa mbunge wa Karatu kabla ya kugombea urais mwaka 2010, anatazamiwa kuteuliwa tena na chama chake kuwania urais na ni mmoja wa watu wanaopewa nafasi kubwa ya kupitishwa na Ukawa kupeperusha bendera ya upinzani dhidi ya mgombea wa CCM, kwenye mbio za Ikulu.

Mbali na kufanya vizuri mwaka 2010, Chadema ilipiga hatua kubwa zaidi kwenye Uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliofanyika mwishoni mwa mwaka jana baada ya kunyakua viti vingi vilivyokuwa vinashikiliwa na CCM na vyama vingine vya upinzani.

Chadema ilifanya vyema zaidi katika Kanda ya Serengeti kwa kupata kura nyingi katika vijiji, vitongoji na mitaa, kura ambazo hazijafikiwa na kanda yoyote.
Kanda nyingine zilizofuatia kwa kufanya vizuri katika uchaguzi huo ni Kanda ya Ziwa Victoria na Kanda za Kaskazini.

No comments:

Post a Comment