Saturday, January 24, 2015

Ukawa kuhamasisha wananchi wasipige kura ya maoni Katiba mpya

Dar es Salaam.
Vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) vimetangaza rasmi kutoshiriki katika mchakato wa kura ya maoni ya katiba na kwamba kuanzia sasa vitahamasisha wananchi kuunga mkono.
Uamuzi huo umetolewa leo na wenyeviti wa vyama wanaounda umoja huo wa ukawa ambao ni Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba, Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia na Mwenyekiti wa NLD, Makaidi.

Akizungumza wakati wa kutoa msimamo huo Profesa Lipumba amesema wamefikia uamuzi wa kutoshiriki katika zoezi hilo kwa sababu mchakato mzima haukuwa na maridhiano ya kitaifa.

“Vyama vya siasa ikiwemo CCM vilikubaliana mwaka jana kwamba zoezi la kura za maoni lifanyike mwaka 2016 baada ya uchaguzi mkuu, tulisaini wote na Rais Jakaya Kikwete alikubali, kwa nini mabadiliko yafanyike ghafla” amehoji Profesa Lipumba.

Amesema jambo la kushangaza, Rais Kikwete aligeuka na kutangaza kwamba Aprili 30, mwaka huu kuwa siku ya kupiga kura ya maoni kuhusu Katiba Mpya.

Amesema pamoja na kutangaza siku ya kupiga kura, bado uandikishaji katika daftari la wapiga kura haujaanza kwa sababu wanasubiri vifaa.

“Hadi sasa vifaa vya Biometric Voter Registration (BVR) vilivyopo ni seti 250 wakati vinavyohitajika ni seti 7500, tume inasubiri hadi sasa, zoezi hili litafanyika kweli?,” alihoji Lipumba.

“Mbinu hiyo inafanywa na Serikali kwa sababu Wazanzibari ndiyo wanaona kikwazo kwao,” alisema Makaidi.

Aprili 16 mwaka jana, Wabunge wa Bunge Maalum la Katiba kutoka vyama vya Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi na NLD walitoka nje wakidai bunge hilo lilikuwa halijadili maoni ya wananchi yaliyowasilishwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.

No comments:

Post a Comment