Tuesday, November 18, 2014

Mbowe amshauri Kombani ajiuzulu

Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe, amemtaka Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma), Celina Kombani, kujiuzulu kwa kuwa anaona ufisadi unaofanyika ndani ya serikali.

Aidha, alisema Kombani ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Ulanga Magharibi, hana tuhuma zozote kuhusu Kombani, lakini anaona wizi unaofanywa na baadhi ya mawaziri ili kulinda heshima yake ajiuzulu ili aendelee kuwa msafi.

“Celina anajua kuwa kuna wizi wa kutisha serikalini, sijamsema Celina kwa sababu sina tuhuma zake, nikiwa nazo nitasema ili kuendelea kulinda heshima yake anatakiwa ajiuzulu,” alisema Mbowe.

Mbowe alisema hayo wakati wa ziara yake ya operesheni ya “Delete CCM” kuelimisha wananchi kuhusiana na uchaguzi wa serikali za mitaa na kuikataa Katiba iliyopendekezwa katika Jimbo la Ulanga Magharibi, mkoani Morogoro alipokuwa akihutubia wakazi wa eneo hilo.

Katika mkutano huo uliofanyika Kijiji cha Mwaya Kata ya Mang’ula wilayani Kilombero, alisema kwa sasa kuna tabaka kubwa katika elimu tofauti na kipindi alipokuwapo Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, wanafunzi wote bila ubaguzi wa walikuwa wakisoma shule moja.

Alisema kwa sasa watoto wa mawaziri na viongozi wengine serikali wanasoma shule za kimataifa huku watoto wa maskini wakisoma shule za kata ambazo hazina maabara, walimu na vitabu.

Alisema serikali inaendelea kuwabebesha wananchi mzigo kwa kuwachangisha michango ya maabara huku mamilioni ya fedha yakiibiwa na viongozi badala ya kujenga maabara.

Aliwataka wakazi wa Kilombero katika uchaguzi wa serikali za mitaa kuwachagua wapinzani kupitia Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) ili walete uwazi katika mapato na matumizi ya fedha za serikali kila baada ya miezi mitatu tofauti na chama tawala.

No comments:

Post a Comment