Tuesday, June 17, 2014

HOTUBA YA MSEMAJI MKUU WA KAMBI RASMI YA UPINZANI BUNGENI MHE. ESTHER NICHOLAS MATIKO (MB), AKIWASILISHA BUNGENI TAARIFA YA KAMBI RASMI YA UPINZANI BUNGENI KUHUSU MPANGO WA MAENDELEO WA TAIFA MWAKA 2014/2015 (Inatolewa chini ya Kanuni ya 105 (8) ya kanuni za Bunge Toleo la mwaka 2013)

1.    UTANGULIZI:
Mheshimiwa Spika, napenda kumshukuru mwenyezi mungu kwa kunijalia afya njema na kuniwezesha kusimama mbele ya bunge hili kutoa maoni ya kambi Rasmi ya Upinzani kuhusu Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2014/15.
Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii pia kutoa shukrani kwa Kiongozi wa Upinzani Bungeni Mheshimiwa Freeman Mbowe kwa kuniamini na kuniteua kuwa Msemaji Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani katika Ofisi ya Rais- Mahusiano na Uratibu. Kipekee naishukuru familia yangu (Mume wangu na watoto wangu wapendwa) kwa kinitia moyo katika kazi zangu za kibunge na kichama. Aidha wananchi wote wa Mkoa wa Mara hususani wa Wilaya ya Tarime kwa ushirikiano wanaonipa katika kutekeleza majukumu yangu.
Mheshimiwa Spika,Mpango huu wa maendeleo wa mwaka 2014/15 ni sehemu ya nne ya Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2011/12-2015/16) kama ulivyopitishwa na Bunge hili, na pia ni sehemu ya kwanza ya utekelezaji wa Dira ya maendeleo ya Taifa ya 2025. Dira 2025 imeundwa na nguzo kuu tano ambazo ni: (i)Kuboresha hali ya maisha ya Watanzania (ii) Kuwepo kwa mazingira ya amani,usalama na umoja (iii) Kujenga utawala bora (iv) Kuwepo jamii iliyoelimika vyema na inayojifunza, na (v) Kujenga uchumi imara unaoweza kukabiliana na ushindani kutoka nchi nyingine.

Mheshimiwa Spika, Hoja ya msingi ni kwa kiasi gani Serikali ya CCM imefanikisha utekelezaji wa nguzo ya kwanza ya Dira 2025, ambayo ni kuboresha hali ya maisha ya Watanzania?

Mheshimiwa Spika, Mpango wa maendeleo wa miaka mitano unasema wazi kuwa sera ya matumizi haioneshi msisitizo maalum wa kupunguza matumizi ili yaendane na makusanyo ya ndani. Aidha lile lengo la kutumia asilimia 22 ya makusanyo ya ndani kwa matumizi ya kawaida limeshindikana kabisa[1]. Kwa sasa mwaka wa fedha 2014/15 makusanyo ya ndani ni shilingi trilioni 12.178 na matumizi ya kawaida ni shilingi trilioni 13.408. Aidha, hili linajidhihirisha wazi katika taarifa za Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali.
Mheshimiwa Spika, njia ya kubana matumizi kwa kuondoa udhaifu wa kukarabati barabara mara kwa mara, kuwa na kipindi maalum cha kukarabati barabara mara baada ya kukabidhiwa kwa Serikali nalo nitatizo kubwa linalotumia mabilioni ya fedha za walipa kodi. Taarifa ya Mpango wa miaka mitano inaonesha kwamba kwa mujibu wa makadirio ya benki ya dunia kiasi cha dola za kimarekani bilioni 2.4 kwa mwaka zinatumika kukarabati barabara katika bara la Afrika. Na hili kwa ushauri wao lingeweza kuepukwa kama kungekuwa na kipindi maalum cha ukaratabati “timely preventive maintenance”   na pia kuna mapungufu kadhaa yanayoendana na udhaifu wa Serikali kushindwa kuwa makini. Kama vile kushindwa kukusanya kodi, kuwa na watumishi wengi wasiokuwa na tija[2] n.k

Mheshimiwa Spika, Kama kweli Serikali inataka kufikia malengo ya millenia, Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kuzingatia matakwa ya mpango katika matumizi kwenye miradi ya maendeleo.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inapenda wananchi wafahamu kwamba Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa ya 2014/15 yaliyoletwa na Serikali ili yajadiliwe na Bunge hili  ni ya nne katika mfululizo wa mipango ya kila mwaka ya kutekeleza Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2011/12 – 2015/16). Kwa maneno mengine ni kwamba imebaki miaka miwili tu kukamilisha utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa  Miaka Mitano  (2011/12 – 2015/16)
Mheshimiwa Spika,  Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inapenda pia kuwajulisha wananchi kwamba wakati imebaki miaka miwili tu kwa Serikali kukamilisha utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano, umebaki mwaka mmoja tu kwa upande wa Chama cha Mapinduzi kukamilisha utekelezaji wa   Mpango huo.
Mheshimiwa Spika, Ilani ya CCM ya mwaka 2005 inasema nanukuu “Kukuza uchumi kwa kiwango cha zaidi ya asilimia kumi (10%) kwa mwaka ifikapo 2010 kutoka ukuaji wa sasa wa asilimia sita nukta saba (6.7%) PiaKuanza kupunguza umaskini wa watu wetu kwa namna iliyo dhahiri”, haya yalikuwa ni malengo ya kufikia mwaka 2010, ambapo hadi sasa uchumi haujafikia asilimia 10, pia Asilimia 28.1 ya Watazania wote wanaishi chini ya mstari wa umaskini (below poverty line kwa takwimu za Benki ya Dunia za mwaka 2012), hii ni sawa na Watanzania milioni 12.
 Endelea....


 Mheshimiwa Spika,Kwa kipindi chote cha utekelezaji wa bajeti serikali haijafanikiwa kuwa na bajeti yenye uhalisia wa kupunguza umaskini wa watanzania, kwani Bajeti inayolenga kupunguza umaskini ni ile ambayo inalenga kupunguza mzigo wa kodi kwa wananchi, ni ile ambayo inatengeneza ajira nyingi, ni ile ambayo inakuza uwekezaji hasa wa ndani, ni ile inayomfanya Mtanzania aweze kuweka akiba (savings), ni ile ambayo inalenga kuinua maisha ya walio wengi ambao wako vijijini, ile inayolenga uchumi umilikiwe na Watanzania, ile inayolenga kukuza ujasiriamali na ile inayokuza ulaji (increased consumption).

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa bajeti zote tangu tuanze utekelezaji wa mpango wa taifa, pia utekelezaji wa ilani ya CCM,  na kwa kuwa sisi sote tunayo nia ya kuwaondoa watanzania katika umaskini, ni kwa vipi sasa serikali imejipanga kuhakiki mipango yetu inaendana na sera zetu za bajeti ili tuweze kuoanisha mipango na utekelzaji wake? Kama wataalamu tunao, rasilimali tunazo, nia tunayo, ni kwa vipi tunashindwa?

Mheshimiwa Spika, Ni vema sasa serikali iliambie bunge lako nini kikwazo cha kutekeleza mpango wa maendeleo? Au ni hila za CCM kuwafanya watanzania waendelee kuwa maskini kwa maslahi ya kisiasa? Vema bila kujali itikadi zetu tuungane pamoja kwa nia ya kuwatoa watanzania katika umasikini mkubwa kwani ni ukweli kwamba hawatakiwi kuwa huko kutokana na utajiri wa nchi hii ulivyokuwa mkubwa. Hali hii haikubaliki kabisa. Inabidi tutanzue kitendawili hiki cha kuwa nchi tajiri sana kwa wingi wa rasilimali ila watu wake ni masikini.

Aidha, Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sura ya Tisa (9) Ibara ya 212 ya Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2010 inasema kwamba:
 “Chama Cha Mapinduzi katika miaka mitano ijayo,(yaani 2010 - 2015) kinaelekeza nguvu kubwa katikakutimiza lengo la msingi la Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2025 kwa kuendeleza jitihada za ujenzi wa uchumi wa kisasa na taifa linalojitegemea. Katika kuzingatia jukumu hilo Ilani hii ya CCM ya 2010 hadi 2015 inatangaza nia ya modenaizesheni ya uchumi. Modenaizesheni ya uchumi ndiyo njia ya uhakika itakayobadili na kuleta mapinduzi katika uchumi wa nchi, kujenga msingi wauchumi wa kati unaoongozwa na viwanda, kuondoa umasikini wa wananchi wetu kwa kiwango kikubwa na hivyo kuwezesha nchi yetu kujitegemea…………...”
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inataka wananchi wapime na kufanya tathmini wenyewe juu ya mambo yafuatayo:
                                  i.             Miaka mitatu ya utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano kwa Upande wa Serikali na Miaka Minne ya Utekelezaji wa Mpango huo huo kwa upande wa CCM imeleta mabadiliko katika maisha yao kama ilivyokusudiwa na mpango huu?
                                 ii.            Je, ni kweli kwamba Mkakati wa CCM wa kufanya mapinduzi ya Uchumi (Modenizationi ya uchumi) uliotangazwa na ilani ya uchaguzi ya CCM ya 2010 umefanikiwa?
                               iii.            Je, ni kweli kwamba msingi wa uchumi wa Tanzania unaongozwa na viwanda kama CCM ilivyoahidi kwenye ilani yake ya uchaguzi ya 2010?
                              iv.            Je, ni kweli kwamba umasikini wa wananchi umepungua zaidi kuliko miaka mitatu au minne iliyopita kama CCM ilivyoahidi kupunguza umasikini kwa wananchi na kuleta maisha bora kwa kila Mtanzania?
                               v.            Je, ni kweli kwamba sasa hivi Tanzania ina uwezo zaidi wa kujitegemea kuliko miaka mitatu au minne iliyopita kama ambavyo CCM iliahidi kwamba kabla ya 2015 Tanzania itakuwa na uchumi imara na hivyo kujitegemea?
                              vi.            Je ni kweli kwamba hali ya ajira hasa kwa vijana ni bora zaidi kuliko miaka mitatu au minne iliyopita kama ambavyo Serikali ya CCM ilivyoahidi kutoa ajira ili kupunguza umasikini wa kipato?
                            vii.            Je, ni kweli kwamba ugumu wa maisha umepungua zaidi kuliko miaka mitatu au minne iliyopita kama ambavyo Serikali ya CCM ilivyoahidi kuleta maisha bora kwa kila Mtanzania?
                           viii.            Je, bajeti za Serikali kwa miaka minne iliyopita zimeweza kuondoa tatizo la  umasikini kwa watanzania?

Mheshimiwa Spika, Mpango wa maendeleo wa mwaka 2014/15 ni sehemu ya Mpango wa Maendeleo wa miaka mitano ambao nao ni sehemu ya Kwanza kati ya sehemu tatu za mipango ya nchi ili kufikia dira ya maendeleo ya mwaka 2025. Lengo la ujumla la sehemu ya kwanza ya dira ya 2025 ni “kutoa fursa ili hazina ya raslimali za nchi zitumike ipasavyo kwa kuweka mazingira wezeshi na kutanua wigo wa ukuaji wa uchumi ili watu maskini waweze kukua kiuchumi”.
Mheshimiwa Spika,Kambi Rasmi ya Upinzani inapenda kurudia kauli ambayo tumekuwa tukiieleza Serikali kuwa Mpango mzuri haupimwi kwa vigezo vya jinsi Kitabu cha Hotuba ya Bajeti kilivyopangwa vizuri, maneno mazuri yaliyomo katika hotuba hiyo, au nadharia ya malengo ya kisiasa yanavyonyumbuliwa katika hotuba hiyo.
Mheshimiwa Spika, utengaji wa asilimia kati ya 25 na 30 ya bajeti kuanzia mwaka 2012 hadi sasa kwa matumizi ya maendeleo ni kwenda kinyume cha Mpango wa maendeleo[3] ambao umeeleza vyema kwamba kwa utekelezaji wa sehemu ya kwanza ya mpango wa miaka mitano Serikali itenge si chini ya asilimia 35 kila mwaka kwa ajili ya miradi ya maendeleo. 
Mheshimiwa Spika, Mpango mzuri wa Maendeleo kimsingi ni takwimu ya jinsi tarakimu za mapato na matumizi zilivyopangwa na utekelezaji wake. Kinyume na hapo mpango uliowekwa vizuri kwenye hotuba bila ya kuwepo kwa mkakati wa utekelezaji wa mpango huo ni kazi bure. Kwa sababu hiyo hotuba ya Kambi Rasmi kwa  mwaka huu, inajikita katika uchambuzi wa  takwimu mbalimbali zilizomo katika mpango uliopita na mpango wa mwaka huu wa fedha ili kuonyesha kwa jinsi gani Mpango unaoletwa na Serikali usivyokuwa na mashiko katika utekelezaji wake. Kwani fedha za utekelezaji ndio kigezo kikuu cha kutuonesha tutokako, tulipo na wapi tunakokwenda kama nchi.
Aidha Kigezo hiki ndicho pia kinaonyesha kama vipaumbele vyetu viko sahihi, kama tunasimamia fedha na rasilimali zetu vizuri, kama tunachukua hatua wakati mwafaka ili kudhibiti ubadhirifu, wizi na ufisadi au ni business as usual?

2.    HALI YA UCHUMI WA TAIFA
Mheshimiwa Spika, taarifa ya hali ya uchumi inaonesha kuwa Pato la Taifa katika mwaka 2013 lilikua kwa asilimia 7.0 ikilinganishwa na ukuaji wa asilimia 6.9 kwa mwaka 2012. Shughuli ndogo ambazo zilikua kwa kasi kubwa katika mwaka 2013 ni pamoja na mawasiliano asilimia 22.8; ujenzi asilimia 8.6; biashara ya jumla na rejareja asilimia 8.3; na hoteli na migahawa asilimia 6.3. Kwa upande mwingine ukuaji wa sekta ya kilimo ulibaki kama ilivyokuwa mwaka 2012 wa asilimia 4.3. Hii ilitokana na kupungua kwa kasi ya ukuaji wa shughuli ndogo za mazao kutoka asilimia 4.7 mwaka 2012 hadi asilimia 4.5 mwaka 2013.

Aidha, Mheshimiwa Spika, kuongezeka kwa kasi ndogo ya ukuaji wa sekta ndogo ya mifugo na uwindaji ya asilimia 3.1 hadi 3.8 na misitu kutoka asilimia 2.4 hadi 3.3. Pia shughuli zingine ambazo ukuaji wake ulipungua katika mwaka 2013 ni bidhaa za viwandani asilimia 8.2 hadi 7.7; umeme na gesi asilimia 6.0 hadi 4.4; uchukuzi asilimia 7.1 hadi 6.2; na uvuvi asilimia 2.9 hadi 2.2.
Mheshimiwa Spika, Matokeo ya Utafiti wa Mapato na Matumizi ya Kaya Binafsi wa Tanzania Bara kwa Mwaka 2011/12 unaonesha kuwa “Kiwango cha Umaskini wa Mahitaji ya Msingi kwa mtu mmoja kwa mwezi ni Shilingi za Tanzania 36,482/= na Kiwango cha Umaskini wa Chakula kwa mwezi kwa mtu mzima ni Shilingi za Tanzania 26,085/=. Kwa kutumia takwimu hizi, matokeo yanaonesha kuwa zaidi ya robo (asilimia 28.2) ya watu wote waishio Tanzania Bara wako chini ya mstari wa kiwango cha umaskini wa mahitaji ya msingi na asilimia 9.7 ya watu wote wapo chini ya mstari wa umaskini wa chakula[4]”.
2.1.       MWENENDO WA VIWANGO VYA RIBA
Mheshimiwa Spika, Wizara ya Fedha kupitia Benki Kuu, inayo wajibu wa kusimamia utekelezaji wa sera za fedha na sheria zinazohusu mashirika ya fedha na benki. Jukumu hili huambatana na wajibu wa kudhibiti mfumuko wa bei (inflation), ambalo wizara imejitahidi kulitekeleza.
Hata hivyo, Wizara imeshindwa kusimamia viwango vya riba vinavyotozwa na mabenki pamoja na taasisi za fedha.  Wakati mfumuko wa bei umeshuka toka   asilimia 19.8  Disemba 2011 na kufikia asilimia 6 mwezi Machi 2014, viwango vya riba katika mabenki na asasi za fedha vimeendelea kuwa vya juu.
Mheshimiwa Spika, riba halisi ‘(real interest rate)’ ambayo inakadiriwa kama tofauti ya ‘nominal interest rate’ na ‘inflation rate’ hivi sasa ni kati ya asilimia 12 – 18. Hakuna shughuli ya kiuchumi ya kawaida unayoweza kuifanya na kuweza kulipa riba za juu kiasi hiki.
Mwananchi wa kawaida akiweka akiba yake analipwa riba ‘(saving deposit rate)’ ya asilimia 3 wakati mfumko wa bei wa sasa ni asilimia 6. Hata wakati mfumko wa bei ulipokuwa asilimia 19.8 riba aliyolipwa mwananchi wa kawaida anayeweka akiba ilikuwa asilimia 2.9. Mabenki yetu hayampi mwananchi wa kawaida motisha wa kuweka akiba bali yanambana mjasiriamali kwa kumtoza riba kubwa.
Mheshimiwa Spika, Riba katika benki na asasi za fedha imeendelea kuwa juu, mojawapo ya sababu ya kiwango hiki kuwa juu ni  Serikali kuwa mmoja wa wakopaji wakubwa kutoka katika mabenki na asasi za fedha za hapa nchini. Ripoti ya Benki Kuu ya Tanzania iliyotolewa mwezi Machi 2014 imeainisha kuwa Serikali imekopa kutoka kwenye vyanzo vya ndani zaidi ya shilingi Trilioni moja katika kipindi cha Mwezi Machi 2013 hadi Machi 2014. Hali hii imesababisha ushindani usio wa haki  baina ya serikali na wananchi wanaokopa katika mabenki  hayo (crowding effect). Anayeumia kwa hali hii ya ushindani na serikali ni mkopaji mdogo.

 Mheshimiwa Spika, ukopaji wa serikali kama ulivyoelezwa hapo juu unachangia kufanya riba ziwe za juu. Riba inayolipwa na serikali kwa ’Treasury Bills’ ya mwaka mmoja  mpaka mwezi Disemba 2013 ilikuwa asilimia 15.63. Kwa mabenki mengi kuwekeza kwenye hatifungani za serikali ‘(treasury bills and bonds)’ kuna faida kubwa ya uhakika ambapo kumkopesha mjasiriamali wa kawaida kuna ‘risk’ kubwa ya kutolipwa.

Mheshimiwa Spika, Pamoja na kuwepo na mabenki mengi mfumo wetu wa fedha haufanyi  kazi ya kukusanya akiba kwa wingi na kuiwekeza kwa wajasiriamali wandani ili kukuza uchumi na kuongeza ajira. (Mfumo wa riba upo kwenye Quarterly Economic Report of March 2014 ya Benki Kuu Table 3.13).

Mheshimiwa Spika, kupungua kwa riba za benki kutaongeza fursa za kukopa na kusaidia wananchi kukuza mitaji. Hali hii itasaidia ongezeko la ajira ambalo ni tatizo kubwa sana nchini, kukua kwa uchumi wa taifa, idadi ya walipa kodi itaongezeka na ustawi wa wananchi utaimarika.
3.    UTEKELEZAJI WA MPANGO WA MWAKA 2013/14
Mheshimiwa Spika, kitendo cha kutenga asilimia 30 ya bajeti toka mwaka 2012 hadi mwaka huu kama fedha za maendeleo, na hili ni kwenda kinyume na matakwa ya mpango wa maendeleo wa  miaka mitano, kifungu cha 4.5.1 ambacho kinasisitiza kutenga si chini ya asilimia 35 ya bajeti kuu. Mapungufu haya maana yake ni kwamba tuko nyuma sana katika kufikia malengo ya millenia.

Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kwa mara nyingine kukusanya mitaji ya ndani kutoka kwa watanzania wenyewe kwani miradi mingi ni kwa ajili ya maendeleo yetu na hili linaondoa dhana nzima ya uchumi inayoitwa “tragedy of the common”

Mheshimiwa Spika, Mpango wa Serikali wa Maendeleo kwa mwaka 2013/14 ulikuwa ni kuzingatia vipaumbele vile vile vya mpango wa miaka mitano ambavyo ni:
a.    Miundombinu, b. Kilimo, c. Viwanda vinavyotumia malighafi za ndani, d. Maendeleo ya rasilimali watu na ujuzi, na mwisho ni e. Uendelezaji wa huduma za utalii, biashara na fedha.

Mheshimiwa Spika, Taarifa za Serikali zinaonesha kuwa kumekuwepo na mafanikio makubwa katika utekelezaji wa mpango kwa mwaka wa fedha unaoishia mwezi juni, lakini jambo la ajabu ni kwamba takwimu za wizara ya fedha zinaonesha kwamba utekeleza wa bajeti kwa fedha za maendeleo kwa fedha za ndani hadi mwezi Mei fedha zilizotolewa ni asilimia 52.2 na fedha za nje ni asilimia 39.6 tu. Na hivyo kufanya jumla ya fedha za maendeleo zilizopatikana kuwa asilimia 46.2 tu.

Mheshimiwa Spika,  Hoja ya msingi hapa kama sekta za kipaumbele kwa mujibu wa mpango zimepewa fedha ambayo haikidhi kuleta matokeo ambayo yalitarajiwa katika mpango wa miaka mitano pamoja na dira ya maendeleo ya mwaka 2025. Ufuatao ni mgawo wa fedha za maendeleo kama zilivyotolewa na Hazina.
Na.
Jina la Sekta
Asilimia ya fedha za maendeleo zilizotolewa hadi Mei 2014
1.       
Sekta ya Kilimo
73
2.       
Sekta ya Maji
26.4
3.       
Sekta Nishati
49.1
4.       
Sekta ya Ujenzi
56.7
5.       
Sekta ya Uchukuzi
42.8
6.       
Sekta ya Viwanda
52.1
7.       
Sekta ya Maliasili na Utalii
15.6
8.       
Sekta Elimu
39.8
9.       
Sekta ya Afya
28.3
10.  
Sekta ya Ardhi
21.8
Chanzo: Taarifa ya Waziri wa Fedha-

Mheshimiwa Spika, Inasikitisha kuona taarifa za serikali zinajaa hadaa kwa wananchi kwa kuwasilisha takwimu na tathmini zisizo halisi na zenye kudanganya umma. Kwa ujumla taarifa hizi ama zinalenga kuonyesha mafanikio makubwa yamefikiwa na serikali katika kutoa huduma kwa jamii au kuonesha kukamilisha miradi ya maendeleo kwa kiasi kikubwa huku uhalisia ukiwa ni tofauti kabisa na yanayoandikwa.
Mheshimiwa Spika, Katika taarifa ya utekelezaji miradi ya maendeleo ya mwaka 2013/14 (uk.8) inaonekana kuwa katika sekta ya kilimo mafanikio mengi yamepatikana kwa kutaja mambo yasiyopimika na haswa yasiyo na uhusiano na vipimo vya mafanikio.
a.   KILIMO
Mheshimiwa Spika, Mafanikio ya sekta ya kilimo hupimwa kwa kuangalia mambo yafuatayo:
·         Uzalishaji katika mazao ya kilimo na mchango wa uzalishaji huo wa kilimo kwenye pato la Taifa
·         Upatikanaji wa masoko kwa mazao ya kilimo, bei ya mazao kulingana na faida kwa wakulima na kufikika kwa masoko;
·         Lishe na uhakika wa chakula kwa familia na Taifa unaotokana na mafanikio ya uzalishaji; na
·         Maboresho ya mbinu na pembejeo za uzalishaji katika sekta.

Mheshimiwa Spika, Lakini ukiangalia taarifa za serikali zinaongelea mambo tofauti na ambayo yanawahadaa wananchi kufikiria kuna mafanikio ambayo kwenye uhalisia hayapo. Hivi sasa tunashuhudia kuendelea kudorola mchango wa kilimo kwenye pato la Taifa ambapo sasa ni 4.3 ikilinganishwa na 4.6 mwaka 2008. Ieleweke kwamba licha ya kilimo kuwa nguzo muhimu katika uchumi wetu na kwamba watanzania takribani asilimia 80 wanategemea kilimo katika kuendesha shughuli zao za maendeleo, sekta hii ndio inachangia mchango mdogo zaidi kwa sekta zote zilizobakia ukiachia Uvuvi unaohujumiwa, ambapo viwanda na Ujenzi  vinachangia 7.5% huku sekta ya Huduma ikichangia 8.2%.
Mheshimiwa Spika, sehemu kubwa ya bajeti ya maendeleo kwenye sekta ya kilimo kwa miaka kati ya 2010/11 hadi 2013/14 imekuwa inakwenda kwenye idara ya maendeleo ya mazao na kufuatiwa iliyokuwa idara ya Umwagiliaji na huduma za ufundi. Ni kweli kwamba idara zote hizi ni muhimu, lakini Kambi Rasmi ya Upinzani inaona kama fedha hizo zingelikuwa zinaingizwa moja kwa moja kwenye benki ya kilimo na wakulima kukopa ni dhahiri kilimo kingekuwa na tija zaidi kuliko ilivyosasa kwani thamani ya fedha hizo kwenye kilimo haionekani.

Mheshimiwa Spika, Kilimo ndiyo sekta kiongozi katika kuliingizia taifa fedha za kigeni na kubwa zaidi ndiyo sekta inayoongoza kwa kutoa ajira. Hivyo basi ili kukifanya kilimo kuwa na tija zaidi badala ya kuweka motisha za kikodi kuwaleta wawekezaji kutoka nje ili kuwekeza kwenye kilimo. Kambi Rasmi ya Upinzani inaona lingekuwa ni jambo bora kwa kuweka mpango wa kutoa mikopo kwa kuiwezesha benki ya kilimo kufanya kazi na kuwafikia wakulima wengi zaidi na hivyo uwekezaji katika kilimo ukafanywa na wananchi wenyewe na faida itakayopatikana itarudi humu nchini tofauti na kama uwekezaji utafanywa na wageni. Hili ni muhimu sana kwani kutakuwa na  “multiplier effect”kama uwekezaji katika kilimo utajikita hapa hapa.

Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani kama ambavyo imesema hapo awali kuwa fedha nyingi zinazowekwa kwenye sekta ya mazao kama zitawekwa kwenye benki ya kilimo ni dhahiri fedha hizo zitatumika kwa tija zaidi na nzuri zaidi zitarudi na kuingia tena kwenye mzunguko wa kukopesha. Aidha, kwa njia hii ni dhahiri ajira zitaongezeka mara dufu na itapunguza wimbi la vijana kuhamia mijini.
Mheshimiwa Spika, Aidha, mkakati wowote ambao unahusu uwekezaji katika kilimo ambao hauhusu wakulima wadogo na wa kati maana yake ni kwamba bado wakulima wadogo wataendelea kuwa ni manamba katika mashamba makubwa ya wawekezaji ambao ndio mpango wa Serikali ya CCM. Kambi Rasmi ya Upinzani inaona kwamba mpango huu utaendeleza mtindo wa kuwapora ardhi wananchi na kuwamilikisha wageni. Jambo hili siyo haki na linapingwa kwa nguvu zote.

b.   ELIMU
Mheshimiwa Spika, Vivyo hivyo kwenye sekta ya elimu ambako vigezo vya ukuaji na mafanikio ya elimu vimeachwa huku serikali ikizungumzia mambo ya utekelezaji tu. Vigezo vya mafanikio ya elimu ni pamoja na Ubora wa Elimu, Ufaulu wa Wanafunzi ikiwa ni pamoja na kuwa na ujuzi wa kumudu matakwa ya kiwango walichofikia, idadi ya wahitimu ikilinganishwa na mahitaji ya soko, watoto waliopo, walioandikishwa na waliomaliza mafunzo. Hata hivyo tungeliweza kuongelea mafanikio kwa kuondoa kero, lakini taarifa hii hata kero za walimu na ukosefu wa madawati hazizungumzwi. Hii ni kuwahadaa wananchi na kulidanganya bunge.
Mheshimiwa Spika, Elimu yetu hasa inayotolewa kwenye shule za Serikali itaendelea kuwa duni sababu ya uwekezaji mdogo unaofanyika kutokana na ukweli kwamba, sera, sheria na kanuni zilizowekwa ili kuiendeleza elimu serikali haizifuati, badala yake vigezo hivyo vinawekwa kwenye shule binafsi. Mfano mzuri ni pale sera inaposema kuwa shule haitasajliwa hadi iwe na vyoo, viwanja vya michezo, maabara n.k
Mheshimiwa Spika, Ni shule ngapi za kata zinaanzishwa bila ya kuwepo kwa matakwa hayo ya kisheria? Huu ni udhaifu unaotokana na ukweli kwamba, Serikali inamiliki shule, inasimamia shule inatunga mitaala, inatunga mitihani ni kwa vipi serikali iwe kama mchezaji, mchezeshaji na msimamizi wa mchezo. Ni lazima serikali ikubali kubakia na jukumu la kusimamia ubora wa elimu na kuruhusu uendeshaji wa elimu kuchukuliwa na chombo kingine, vinginevyo tutabaki kulalamika miaka yote kuwaout put ya elimu ailingani na in put inayowekwa katika elimu”
Mheshimiwa Spika, Ni muda mwafaka sasa Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kubadili usimamizi wa Sekta ya elimu kwa serikali kuwa msimamiaji wa ubora wa elimu na sio mtoaji wa elimu, kwani kufanya hivyo inaua dhana ya ushindani baina ya watoaji wa elimu. Huu ni upofu wa wataalam wetu au washauri wetu katika sekta ya elimu.
Mheshimiwa Spika, kumekuwepo na mjadala mkubwa kwamba mashule na vyuo binafsi zinatoza karo kubwa kiasi kwamba wananchi wenye kipato cha chini hawawezi kusomesha watoto wao kwenye shule hizo. Hoja ya msingi ni kwanini inakuwa hivyo?
Mheshimiwa Spika, shule hizo binafsi zinakumbwa na ubaguzi ule ule wa Serikali ambapo shule hizo zinatakiwa kulipa kodi kadhaa na ili shule hizo ziendelee kuwepo ni lazima wapandishe karo kwa wanafunzi, na hapo ndipo ughali unapoonekana wazi. Kodi hizo ni zifuatao:
1.      Corporation tax
2.      Value Added TAX
3.      Skills & Development Levy
4.      Land Rent
5.      Local Government taxes:
a.     Property tax
b.     City Service levies
c.     Tax for sign board
6.      Fire brigade Inspection fees
7.      Work permit fee for teachers (Wanaotoka nje kwa ajili ya masomo ya sayansi).

c.   SEKTA YA NISHATI
Mheshimiwa Spika, Katika sekta ya nishati serikali ilikuwa na lengo la kuwafikishia umeme asilimia 30 ya wananchi kwa kuwaunganishia umeme watumiaji 150,000 ifikapo Julai 2014. Huku wizara ikiripoti kuwaunganishia umeme wananchi 70,002 tu, taarifa ya serikali zinazopigiwa chapuo na Katibu Mkuu wa CCM zinadai kuwafikia asilimia 36 ya wananchi kabla hata ya Julai 2014. Na ili kuona kwamba serikali imepanga kwa makusudi kabisa kuwahadaa wananchi kupitia takwimu ni pale mhe Steven Wassira katika taarifa yake ya mpango mwezi Aprili aliainisha wananchi 70,002 tu ndio waliounganishiwa umeme kati ya July 2013 na Aprili 2014( nah ii ni kwa kipindi cha miezi 9),lakini kwenye hotuba yake ya 12 Juni 2014 ameainisha kuwa ni wananchi 138,931 wameunganishiwa umeme, hii inaonyesha ongezeko la wananchi 68,931 ndani ya miezi miwili tu? Huu ni uongo wa wazi kwa wananchi na Bunge hili huku wakijua kuwa taarifa hizi hazina ukweli wowote. Zaidi ya hapo ni kuwa hali halisi iliyopo kwa wananchi ni vilio kwa vijiji kutofikiwa na nishati hiyo huku baadhi ya vijiji vikiwa wameunganishiwa wakaazi wachache tu.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa taarifa ya utafiti wa bajeti ya Kaya iliyotolewa mwaka huu inasema, “Matokeo yameonesha kuwa mwaka 2011/12 asilimia 18 ya kaya za Tanzania Bara zinaishi katika nyumba zilizounganishwa na umeme wa gridi ya Taifa. Hili ni ongezeko la asilimia 6 ukilinganisha na matokeo ya mwaka 2007. Nyumba nyingi Maeneo Mengine ya Mjini zimeunganishwa katika umeme wa gridi ya Taifa kuliko Maeneo ya Vijijini. Utafiti huu pia umebaini asilimia 68 ya kaya zilizopo Dar es Salaam na asilimia 36 katika Maeneo Mengine ya Mjini zimeunganishwa katika gridi ya Taifa. Aidha, takribani asilimia 4 ya kaya za Maeneo ya Vijijini ndizo zilizounganishwa katika umeme wa gridi ya Taifa[5]”.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi inaitaka Serikali ilieleze Bunge na wananchi, kama ni ukweli kwamba asilimia zaidi ya 75 ya watanzania wanaishi vijijini na kwa mujibu wa tafiti hizo za idara ya taifa ya takwimu kuwa ni asilimia 4 tu ya wananchi waishio vijijini ndio waliounganishwa kwa gridi ya Taifa. Je hizo asilimia 36 za maeneo ya mijini ndio zinazoongelewa na waheshimiwa wanaowakilisha wananchi waishio vijijini?

Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani itakuwa haijatenda haki kama haitaomba kupatiwa majibu katika sakata zima la IPTL, PAP na ESCROW akaunti. Hivyo basi kwa niaba ya wananchi inahoji yafuatayo:
1.          Kosa la kwanza IPTL haikuweza kukamilisha mradi wake 1995 kwenye kipindi cha dharula na badala yake ikakamilisha  mwaka 1998. Baada ya kumaliza mwaka1998 IPTL ililalamikiwa na tanesco ICSID kwamba imekuza gharama za uwekezaji na hivyo kukuza gharama za umeme. Mwaka 2001 uamuzi wa ICSID ukatoka ikabainika ni kweli IPTL ilikuza gharama kwa kiasi cha dola 27milioni. Serikali ilikuwa na haki ya kupewa fedha zilizokuwa zimelipwa kama capacity charge.

2.     Mwaka 2002 IPTL ikaanza kuiuzia umeme Tanesco lakini mwaka 2004 Tanesco ikabaini kuwa IPTL ilidanganya kuhusu mtaji. IPTL ilisema 30% ya mtaji ilikuwa nao kama equity sawa na dola 36milion ambayo ni shilingi bilioni 36 na kwamba 70% ilikopa. Lakini baada ya ukaguzi ikabainika kuwa IPTL haikuweka dola 36milion kama equity bali dola 50 ambapo kwa exchange rate ya wakati huo ya 1:1000, dola50 ilikuwa sawa na Tsh elfu 50 ambazo hata fundi baiskeli angeweza kuwekeza.

3.     Kutokana na kasoro hiyo Tanesco ikataka gharama ya umeme (tarrif) ishuke kwa sababu bei ilizingatia equity ya tshs bilioni 36 kumbe ni tsh 50000. Mabishano yakaendelea mpaka 2006. Mwaka 2006 Serikali na Tanesco ikashinikiza ifunguliwe akaunt maalumu (escrow) ili malipo yawekwe huko mpaka mgogoro utapokwisha kuhusu bei sahihi ndipo pesa hiyo igawanywe kwa kuzingatia bei sahihi baina ya pande mbili ndio maana ilikuwa kosa kwa Waziri Mkuu, Mheshimiwa Pinda kusema pesa yote ya escrow eti ni ya IPTL kabla ya uamuzi kuhusu bei haujafikiwa.

4.    Mwaka 2008 IPTL iliposhindwa kujiendesha ikawekwa chini ya receivership chini ya RITA ambapo ni RITA ikawa inasimamia gharama za uendeshaji. Mwaka 2013 September ikatoka hukumu ya mahakama kuu chini ya Jaji Utamwa ilojichanganya baada ya VIP mwenye 30% kushtaki na kutaka IPTL iondolewe chini ya receivership na mali zote za IPTL ipewe kampuni ya PAP ya singasinga anaitwa Sethi.

Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali iwaeleze watanzania ni kwanini ilifungua ESCROW ACCOUNT kama ilikuwa ni haki kwa IPTL kulipwa capacity charge hiyo?Na kama kulikuwa na uhalali wa kufunguliwa kwa hiyo akaunti ni kwanini sasa fedha zote zimelipwa na Serikali kukosa hata shilingi?
Mheshimiwa Spika, Sekta ya nishati  hasa gesi imekuwa ndio tegemeo la kuitoa nchi yetu katika hali ya umasikini tuliyonayo kwa sasa na kutusukuma hatua kadhaa mbele. Jambo hili linawezekana ikiwa kutakuwepo na ubunifu wa mkakati makini na sio mkakati wa kutegemea wawekezaji toka nje kwani mind set za watawala zimelalia huko, na hawaamini kabisa kama watanzania wazawa wanaweza kuwekeza katika sekta hii ya gesi.
Mheshimiwa Spika, Kwa sasa gesi ya kupikia majumbani imekuwa inapanda kila kukicha na fedha za kigeni zinazotumika kuagiza gesi hiyo nje ya nchi ni nyingi sana. Kambi Rasmi ya Upinzani inaona lingekuwa ni jambo la busara kama gesi asili inachakatwa na kujazwa kwenye mitungi kwa ajili ya matumizi ya majumbani badala ya kutegemea mpango wa TPDC wa kusambaza gesi kwa njia ya mabomba kama mfumo wa maji ulivyo. Uwekezaji huu unaweza kutuchukua miaka 20 ijayo hadi wananchi kuona manufaa ya nchi kuwa na gesi.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inaamini kabisa jambo hili linawezekana kabisa na watanzania wanaweza kuwekeza katika viwanda vya ku-“compress gas” na kuiweka kwenye liquid form na kuijaza kwenye mitungi na kuisambaza kama ambavyo soda au bia zinasambazwa kwa watumiaji. Mfumo huu utaokoa mabilioni ya fedha za kigeni zinazotumika kuagiza gesi ya kutumia majumbani na pia utasaidia kuokoa mazingira yanayoharibika kutokana na ukataji wa mkaa unaotishia maeneo mengi ya nchi yetu kugeuka jangwa.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inaamini kabisa uwekezaji wa aina hii hauhitaji mtaji kutoka nje, bali wananchi kwa wingi wao wanaweza kutoa mtaji huu na wao wakawa ni wanahisa katika uwekezaji huu, kianachotakiwa ni ubunifu wa jinsi ya kuwashirikisha wananchi katika uwekezaji huu. Faida itabaki hapa hapa nchini kinyume na ilivyo sasa.

Mheshimiwa Spika, Katika sekta ya maji, taarifa ya utekelezaji miradi ya maendeleo inaonesha kuwa serikali imefanikiwa kuongeza kasi ya kuwafikishia huduma za maji safi wananchi  kutoka 300,000 hadi 500,000 hadi watu 2,390,000 kwa miezi sita tu ya utekelezaji bajeti ya 2013/14. Hii haijalishi kuwa wizara hii hadi kufikia Juni 2014 ilipowasilisha taarifa yake ya utekelezaji bajeti na kuomba bajeti ya 2014/15 ilikuwa imepatiwa jumla ya 27% tu ya bajeti. Hii maana yake ni kwamba kwa kipindi cha miaka zaidi ya hamsini ya uhuru watu waliopatiwa maji  safi na salama vijijini ni 500,000 lakini kwa miezi sita tu idadi hiyo imeongezeka kwa takriban asilimia 260 na kufikia watu 2,390,000. Kwa hali ya kawaida ni nani anaweza amini miujiza hii?

Mheshimiwa Spika, Kuhusu utekelezaji wa jumla wa miradi ya maendeleo kulingana na Mpango wa Maendeleo wa Miaka 5, taarifa ya serikali inaonesha kati ya miradi 80 iliyopangwa kutekelezwa, hadi Aprili 2014 (huu ukiwa ni mwaka wanne wa utekelezaji mpango) HAKUNA hata mradi mmoja uliokamilika. Kati yake miradi 13 inaendelea vizuri huku minne mingine ikiwa ya kuridhisha, na iliyobaki 63 ikiwa katika hali isiyoridhisha na au imekwama. Iwapo utekelezaji huu ungewekwa kwenye GREDI za ufaulu wa kielimu ungekuwa kama ifuatavyo:
Division I = 0;
Division II = 13;
Division III = 4;
Division IV = 51; na
Division 0 = 12

Je malengo ya mpango ya 2025 yatafikiwa kwa utekelezaji wenye tathimini (evaluation) ya kufeli kama nilivyoinisha kwenye gredi za ufaulu.
Mheshimiwa Spika, Mwaka huu wa fedha wa 2014/15, mwaka wa mwisho wa utekelezaji Mpango huu, serikali imeomba jumla ya TShs 5.445 Trilioni kutekeleza ukamilishaji miradi hiyo huku kukiwa na uhakika kabisa kuwa haiwezi kukamilisha ahadi hizi hewa.
Eneo jengine la hadaa ni pale serikali inaposhindwa kuwaeleza wananchi na Bunge sababu za kushindwa kwake. Kwa mfano miradi wa Ujenzi ya barabara za Dumila – Kilosa na ule wa Dumila – Turiani imekwama kwa zaidi ya mwaka sasa huku matuta yake yakiota majani na wakandarasi kulalamikia malipo. Hakuna mahala popote kwenye taarifa hizi serikali inaelezea utekelezaji miradi hii. Miradi kama hii ipo mingi nchini ambayo hutekelezwa kimyakimya na au kutelekezwa kwa miaka kadhaa bila ukamilishaji na kuwaacha wananchi kwenye dhiki zaidi kuliko awali.

Mheshimiwa Spika, ardhi ni kichocheo kimojawapo cha kukuza uchumi na pia chanzo kikuu cha mapato kama kitatumika vyema. Serikali kwa makusudi imeshindwa kukusanya kodi ya ardhi kwa nyumba nyingi zilizopo maeneo ya mijini na badala yake imekuwa ikitumia fedha nyingi kwenda kupima maeneo ambayo wamiliki wake hata hawalipi kodi. Ina kadiriwa kwamba karibu asilimia kati ya 30 na 60 ya nyumba za mijini hazina hati jambo linalopelekea kupoteza mapato ya kodi ya ardhi.

Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi inaitaka Serikali kuondoa ukiritimba usiokuwa na maana na kupunguza gharama za utoaji wa hati za nyumba na viwanja na ikibidi hati zitolewe na wananchi walipie taratibu huku wakilipa kodi ya ardhi. Tunaamini jambo hili liko ndani ya uwezo wa mamlaka husika.
Mheshimiwa Spika, kwa kuangalia hali halisi iliyopo kwa wananchi na yale yaliyoandikwa kwenye nyaraka za Serikali, Kambi Rasmi ya Upinzani inaona kwamba, sababu zifuatazo ndizo zimepelekea hali hiyo:
  1. Tunapanga maendeleo yetu kwa kutegemea misaada au uwezeshaji toka kwa wahisani (Misaada na mikopo 30% +)
  2. Tunapanga mipango ambayo hatuwezi kuitekeleza. Miradi mingi inachukua muda zaidi ya muda pangwa na hivyo kuongeza gharama.
  3. Miradi mingi ya maendeleo haina uhalisia wa malengo/mahitaji ya jamii lengwa (Miradi inakuwa si shirikishi na hivyo utekelezaji wake hauhusishi wananchi).
  4. Serikali haijatekeleza vipaumbele ilivyoviweka (Yaani kupanga bajeti yake kulingana na maazimio iliyoridhia).
  5. Serikali kushindwa kutoa fedha za maendeleo hata zile zilizopangwa kwenye bajeti yake, kupeleka kiasi ambacho sicho kilichopangwa kwenye bajeti kwa ajili ya utekelezaji.
  6. Miradi mingi inayokamilika kutokidhi viwango, jambo linalosababisha ukarabati wa mara kwa mara kwa muda mfupi.

4.    UWEKEZAJI WA PAMOJA KATI YA SERIKALI NA SEKTA BINAFSI
Mheshimiwa Spika, Serikali inakosa fedha za kuendesha miradi mikubwa ya maendeleo, aidha kwa kuwadharau wananchi inadhani wenye mitaji ni lazima watoke nje ya nchi. Hili ni kosa kubwa sana.
Mheshimiwa Spika, Kampuni ya Uwekezaji ya Taifa-NICOL iliundwa na wazawa kwa ubunifu wao wakazunguka nchi nzima kukusanya mtaji kwa watanzania na walifanikiwa mabilioni ya shilingi kwa ajili ya kufanya uwekezaji. Hoja ni kwanini Serikali inashindwa kuwaamini watanzania kuwa wawekezaji katika miradi mbalimbali ambayo ni dhahiri fedha za wananchi zinaweza kurudi haraka? Miradi kama ya reli ambayo mzigo wa kutoka na kurudi DRC ni wa uhakika, hivyo mtaji kurudi kwa wanahisa ni haraka. Miradi ya Umeme kwa kutumia maji ya mto Rufiji (Stiglers Gorge). Mtaji wa Kufufua shirika la Ndege la Tanzania, wakati tuna makampuni mengi ya wazawa yanayojihusisha na utalii (Tour Operators) na Taasisi zinazojihusisha na Utalii zilizo chini ya Serikali kama TANAPA, na NGORONGORO CONSERVATION AUTHORITY.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inasema Serikali imechoka kwa kukosa ubunifu wa jinsi ya kupata mtaji toka ndani ya nchi wakati kuna sheria ya PPP inayoruhusu uwekezaji wa pamoja na Sekta binafsi ambayo ni wananchi. Tunarudia tena WAZAWA WANA FEDHA ZA KUTOSHA KUENDESHA NCHI YAO BADALA YA KILA KUKICHA KUKIMBILIA NJE
5.    TAKWIMU
Mheshimiwa Spika, Takwimu ndio hitajio la kwanza katika kupanga mipango na katika kufanya tathmini ya mipango yako. Hivyo basi katika mkakati wa kukuza uchumi na kuondoa umasikini tumekuwa tukipatiwa takwimu zinazoonesha kuwa katika yale malengo mbalimbali ya kupunguza umasikini tuko katika hatua bora na ya kujivunia. Mfano taarifa ya Mkukuta ilikuwa inaonesha kuwa lile lengo la kuwapatia wananchi maji safi na salama kwa mwaka 2009 ilikwishafikia asilimia 57.8, lakini baada ya kupitia upya ikagundulika kwamba ni asilimia 40 tu. Hii maana yake nini? Hii ni hadaa kwa wananchi na wadau wa maendeleo kwa kutaka kuficha madhaifu au ni kutumia takwimu zisizo sahihi jambo ambalo linapelekea kupanga mipango ambayo haina uhalisia na kutunga sera ambazo haziwezi kututoa katika umasikini tulionao japokuwa fedha zipo lakini matumizi hayaendani na hali halisi.
6.    MICHEZO NA SANAA
Mheshimiwa Spika, kwa muda mrefu Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni imekuwa ikipendekeza uendelezaji wa sekta ya michezo kama mojawapo ya vyanzo vya mapato nchini. Umuhimu wa Serikali katika kuwekeza kwenye michezo, ni pamoja na kuongeza mapato, kutoa nafasi za ajira na pia katika kudumisha amani na utamaduni wa Mtanzania.
Shabaha kubwa ya uendelezaji wa viwanja vya michezo nchini ni katika kuijengea Serikali uwezo wa kukusanya mapato zaidi. Hii inawezekana kwa Serikali kuwekeza katika viwanja vya michezo vilivyopo ambavyo vimehodhiwa na chama tawala. Baadhi ya Viwanja vyenye uwezo wa kuliongezea taifa mapato makubwa ikiwa vitaendelezwa ni pamoja na uwanja wa Samora-Iringa, Sheikh Amri Abeid- Arusha, CCM Kirumba –Mwanza, Sokoine-Mbeya na Jamhuri-Dodoma. Kwa uchambuzi wa kina, viwanja hivyo vya michezo vimejengwa katika maeneo muhimu kishabaha, ambayo yana uwezo wa kuingizia taifa mapato kutokana na  mwamko wa wananchi hasa katika michezo.
Mheshimiwa Spika, uwanja wa kisasa wa Benjamin Mkapa maarufu kama uwanja wa Taifa ambao ulijengwa kwa kushirikiana na Serikali ya China kwa thamani ya Shilingi Bilioni 56.4, umeweza kuiongezea Serikali mapato kwa kiasi kikubwa kutokana na makusanyo yanayotokana na mechi za mpira wa miguu pekee. Kwa mujibu wa aliyekuwa Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Mhe. Amos Makalla wakati akijibu swali Bungeni Aprili 2013, alieleza kuwa tangu Uwanja wa Taifa uanze kutumika mwezi Agosti, 2007 hadi kufikia mwezi Februari mwaka 2013, ulikuwa umeingiza shilingi 1,533,697,666 kwa makusanyo yanayopitia Wizara ya Habari, Vijana, Tamaduni na Michezo ambazo hizo ni nje ya mapato yanayokusanywa kupitia kodi ya ongezeko la thamani (VAT) yanayowasilishwa na Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini (TFF).
Mheshimiwa Spika, pamoja na kuwa uwanja huu  wa kisasa umeendelea kutumika kwa ajili ya michezo na matamasha mbalimbali, ukusanyaji wake wa mapato haujaridhisha kutokana na kutokuwepo kwa mfumo wa kielektroniki wa ukusanyaji wa mapato hali inayochangia ukusanyaji hafifu wa mapato na mianya ya ubadhirifu unaotokana  na kutokuwepo kwa ufuatiliaji wa kiteknolojia.
Kambi rasmi ya Upinzani, inapendekeza yafuatayo yafanyike ili kuweza kutumia sekta ya michezo kwa kupitia ujenzi wa viwanja vya kisasa vya michezo nchini na kuongeza ukusanyaji wa mapato;
Mosi, kuvirejesha viwanja vyote vya michezo vilivyohodhiwa na Chama cha Mapinduzi kwa Serikali ili viwe mali ya umma kama ambavyo viliwahi kuwa chini ya Baba wa Taifa,
Pili, kuviendeleza viwanja hivi kwa kuingia ubia na makampuni makubwa ya uwekezaji ama na nchi wahisani ili kurejesha hadhi ya viwanja vitakavyoendana na mahitaji ya kisasa ya viwango na ubora wa viwanja vya michezo
Tatu, kuhakikisha kuwa uwanja wa Taifa hautumiki katika michezo ya aina yoyote bila ya mfumo wa kielektroniki kwa ajili ya ukusanyaji wa mapato ili kuzuia ubadhirifu wa mapato katika mechi mbalimbali unaofanywa na watendaji wasiowaaminifu.
Nne, kupunguza misamaha ya kodi katika makampuni makubwa na kwa walipa kodi wakubwa na fedha hizo zitumike kuboresha baadhi ya viwanja ili kuinua uchumi na kutoa fursa za ajira zitakazotokana na uwekezaji wa viwanja nchini.
Aidha, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaitaka Serikali kufuta misamaha ya kodi ambayo kwa mwaka 2013/2014 ilifikia trilioni 1.5, ambapo kwa gharama ya shilingi bilioni 56.4 zilizotumika kujenga uwanja wa taifa , misamaha hiyo ya kodi ya trilioni 11.5 zingeweza kujenga viwanja 27 vya kisasa nchini, 25 kwa mikoa yote ya Tanzania Bara na viwanja viwili vya kisasa Zanzibar.
6.1.       UENDELEZAJI WA SEKTA YA SANAA NCHINI
Mheshimiwa Spika, lengo la kuendeleza sanaa nchini ni kuongeza nafasi za ajira pamoja na kuongeza vipato ili kukuza uchumi  nchini. Sanaa ikipewa kipaumble pamoja na kurasimishwa ina uwezo wa kuliongezea taifa mapato yatokanayo na kazi za wasanii kama ilivyo kwa soko la filamu nchini Nigeria. Mwanzoni mwa mwaka huu, Nigeria imetangazwa kuwa ndilo Taifa lenye uchumi mkubwa barani Africa na kuipita Afrika Kusini. Pato Ghafi la Ndani (Gross Domestic Product ‘GDP’) la Nigeria limefikia Dola Billion 509 huku lile la Afrika ya Kusini likifikia Dola Bilioni 322. Kwa mujibu wa Idara ya Takwimu ya Nigeria, Nigeria imekuwa Taifa lenye uchumi mkubwa Afrika baada ya wanauchumi wa nchi hiyo kuziongeza sekta za Mawasiliano na Filamu (Nollywood) kwenye takwimu. Ni dhahiri kuwa soko la Filamu la Nigeria linatoa mchango mkubwa mno katika ukuaji wa uchumi wa nchi hiyo. Kabla ya hapo Nigeria ilionekana kama taifa linalotegemea zaidi uuzaji wa mafuta na ilikadiriwa kuwa pato la mafuta lilichangia asilimia 32 kwenye GDP lakini ripoti ya wanauchumi hivi karibuni imeonesha sasa pato la mafuta huchangia Asilimia 15 tu ya pato ghafi la ndani. Nollywood ndiyo sekta ya pili kwa kutoa ajira katika nchi ya Nigeria baada ya sekta ya kilimo, na mchango wake kwa Taifa ni mkubwa sana kwani ina thamani ya Naira bilioni 853.9 (Dola za Marekani bilioni 5.1). Hii ni ishara ya jinsi gani sekta ya filamu inavyoweza kukuza na kubadili uchumi wa nchi yoyote, kwa njia ya utoaji wa ajira kama itachukuliwa kwa umakini mkubwa. Matokeo ya kukubalika kwa sinema pia huwafanya watayarishaji wa sinema, waigizaji na watendaji wengine kuwa na heshima kwenye jamii na hata kisiasa.
Mheshimiwa Spika, ni dhahiri kuwa sekta ya filamu ikiwa ni mojawapo ya kazi za sanaa ina umuhimu mkubwa katika kubadilisha sera za kiuchumi kuliko sasa ambapo Serikali inawatumia wasanii wa filamu kama daraja lao la kutimiza malengo ya kisiasa na si katika kuiboresha tasnia nzima ili kuleta mapinduzi ya kiuchumi. Mojawapo ya mafanikio ambayo Serikali ya CCM imekua ikiyafanya wimbo ni pamoja na kulinda haki za wasanii na kazi zao, wakati huo huo Serikali hii imeshindwa kuandaa Sera ya Sanaa itakayorasimisha sekta hii katika mfumo wa kiuchumi. Aidha, Serikali haina takwimu za uhalisia wala  utafiti wowote uliofanywa kuijua nguvu ya soko la sanaa nchini, hakuna miundombinu ya soko la sanaa, wala thamani ya mchango wa sekta hii katika uchumi wa taifa hautambuliwi ipasavyo. Kukosekana kwa hayo yote ni dhahiri kuwa kazi za sanaa hazilindwi, hazikuzwi, hazitangazwi, hazitambuliki na wala hazipewi umuhimu unaostahili kama ambavyo sekta iliyo rasmi inavyopaswa kuwa. Serikali imeshindwa kuitilia maanani, kuchukua hatua stahiki, kutoa takwimu halisi za mchango wa sekta hii kwenye uchumi wa taifa pamoja na ukuaji wa kasi wa sekta hii hali inayosababisha ishindwe kupata pato halisi linalotokana na sekta hii.
Mheshimiwa Spika, Shughuli nyingi zinafanyika kiholela bila wahusika kuwa na hakimiliki na sehemu kubwa ya mchango wake kwa pato la taifa haijarekodiwa katika vitabu vya mapato vya taifa. Hii inaonesha kuwa mchango wa sekta hii katika pato la taifa ni mkubwa zaidi kuliko takwimu zinavyoonyesha. Ili kama Taifa, tuweze kupiga hatua na kuimarisha sekta ya hakimiliki ni lazima sasa serikali iache porojo za kuwaongopea wasanii kuwa wanautambua mchango wao,  bali ielekeze nguvu kuhakikisha kuwa sera madhubuti za kusimamia sekta ya sanaa nchini zinatungwa pamoja na  sheria na kanuni zinazostahiki ili kuboresha uendeshaji wa sekta hii nchini. Uwepo wa sera bora zitachochea maendeleo ya kisekta, mazingira ya ubunifu yenye ushindani na salama ambayo serikali itayatumia kuendeleza sekta hii na kutambua thamani ya kazi za ubunifu.
Mheshimiwa Spika, sekta ya hakimiliki nchini mwaka 2009 ilichangia kiasi cha Sh676 bilioni sawa na asilimia 4.6 ya Pato la Taifa (GDP), likiwa ni zaidi katika uchumi wa taifa kuliko sekta ya hoteli, migahawa na madini. Taarifa hiyo ambayo imetolewa hivi karibuni kwa lugha ya Kiingereza ikiwa na jina: ‘The Economic Contribution of Copyright-Based Industries’ kwa mwaka 2012, imebainisha kwamba sekta ya madini imechangia asilimia 2.6 ya GDP wakati hoteli na migahawa imechangia asilimia 4.5, sekta ya hakimiliki imefanya vyema. Pia sekta hii imeajiri watu wengi zaidi ya wale walioajiriwa na sekta ya afya na ustawi wa jamii, fedha, majumba ya kukodisha, huduma za biashara, ujenzi, usafirishaji, mawasiliano, madini, umeme, gesi na sekta ya maji. Mchango wa sekta ya hakimiliki kwa malipo ya wafanyakazi, ulikuwa Sh 80.474 bilioni sawa na asilimia 5.
Aidha, nchi kadhaa ambazo sasa zimeendelea zilikuwa na uchumi sawa na Tanganyika  (sasa Tanzania) wakati tukipata uhuru mwaka 1961, nchi hizo ni pamoja na Singapore, Korea Kusini, Thailand, Malaysia na kadhalika, ila kilichowafanya kutuacha kimaendeleo na kupata maendeleo ya haraka ni ulinzi na uendelezaji wa Miliki Bunifu katika kazi za sanaa. Leo hii Korea Kusini imekuwa ni Taifa kubwa na lenye mchango katika kazi za sanaa Barani Asia kwa sababu tu ya kulitambua kundi la wasanii na kuweka mazingira mazuri ya ulinzi wa Miliki Bunifu kiasi cha kubatizwa jina la Marekani ya Asia. Korea imefanikiwa sana kueneza utamaduni wake katika nchi zingine za Asia, na walitumia fursa ya mtikisiko wa kiuchumi uliozikumba nchi za Asia mwaka 1997, ambapo wao waliamua kuwekeza katika sanaa na utamaduni kwa lengo la kuzalisha na kuuza nje kama bidhaa. Hata Rais wa wakati huo, Kim Dae-jung, alipenda kujiita Rais wa Utamaduni na alianzisha mradi huo na kutenga dola za Kimarekani milioni 148.5. Leo hii, Tanzania inashindwa nini katika kuirasimisha sanaa ambayo CCM inaitumia kujipatia kura?
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani, inaelekeza nguvu zake za kuhakikisha kuwa muswada wa Sera ya sanaa unaletwa Bungeni ili kufanikisha utungaji wa Sheria na Kanuni utakaongoza kazi mbalimbali za sanaa nchini ili kuweza kuongeza fursa za ajira na ukusanyaji wa mapato kwa taifa zima kwa ujumla.

7.     MAENEO YA KIPAUMBELE KATIKA MWAKA WA 2014/15
Mheshimiwa Spika, taarifa ya mpango huu umeainisha maeneo ya kitaifa ya kimkakati kwa mwaka wa 2014/15 ambayo ni miundombinu, kilimo, viwanda, maendeleo ya rasilimali watu, huduma za fedha na utalii huku maeneo mengine  muhimu kwa ukuaji wa uchumi yakiwa ni elimu/mafunzo ya ufundi, afya na ustawi wa jamii, mifugo na uvuvi, misitu na wanyamapori ,madini, ardhi, nyumba na makazi, usafiri wa anga, hali ya hewa, biashara na masoko, ushirikiano wa kikanda na kimataifa, utawala bora, vitambulisho vya taifa, sensa ya watu na makazi, kazi na ajira pamoja na mazingira.
8.      REAL ESTATE REGULATORY AUTHORITY
 Mheshimiwa Spika, katika ushauri wetu kwa bajeti ya mpango iliyopita tuliitaka Serikali kuanzisha mamlaka ya kudhibiti sekta hii kwani fedha nyingi za kodi ya majengo na kodi ya ardhi (Property tax and Land Rent) hazikusanywi na hivyo kuikosesha Serikali mapato.
Mheshimiwa Spika, kuanzishwa kwa mamlaka hii ni dhahiri kodi itakusanywa kulingana na ardhi ilipo katika miji na majiji (land value depend on location). Ni ukweli kwamba tumekuwa tukikosa mapato mengi sana kutokana na kukosekana kwa mdhibiti katika sekta hii ya ardhi yenye majengo.
9.     KUKUZA UCHUMI VIJIJINI (Rural growth)
Mheshimiwa Spika, kukuza uchumi vijiji ni kipaumbele cha kwanza kwa Kambi Rasmi ya Upinzani kwa miaka kadhaa iliyopita na kitaendelea kuwa kipaumbele chetu. Kambi Rasmi ya Upinzani inaamini kuwa kama mkatakati utawekwa kwa kila Halmashauri za vijijiji za kutengeneza mazingira ya kutoa ajira rasmi zipatazo mia tano kila mwaka basi zitakuwa zimepiga hatua kukabiliana na wimbi kubwa la vijana kukimbilia mijini kwa ajili ya kutafuta ajira.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa mazingira ya vijijini yanatofautiana  na kwa kuwa rasilimali zilizo katika maeneo ya wilaya za vijijini zinatafoutiana pia kati ya wilaya na wilaya, hivyo basi Serikali kuu  inatakiwa kuweka kiwango mkakati (threshold) cha maendeleo kinachotakiwa kufikiwa na kila Wilaya kulingana na fedha zilizotengwa kwa ajili kukuza uchumi vijijini.
Mheshimiwa Spika, kwa njia hii, mabadiliko ya kimaendeleo yataonekana zaidi kuanzisha mifuko ya uwezeshaji  ambayo wanafaikaji ni wale waishio mijini zaidi na kwa upande wa wilayani ni wale wenye uwezo tayari.

Mheshimiwa Spika, Kambi rasmi ya Upinzani Bungeni imeainisha maeneo yafuatayo kama vipaumbele vya Mpango wa Taifa wa Maendeleo:
  1.  Kukuza Uchumi Vijijini
  2. Miundombinu na Usafiri wa anga
3.      Ardhi, Nyumba na Makaazi
4.      Elimu na Afya
5.      Michezo na Sanaa

10. UGHARAMIAJI WA MPANGO
Mheshimiwa Spika, mpango wa maendeleo wa serikali  kwa mwaka 2014/2015 ni dira ya kuakisi mpango wa kibajeti kwa mwaka  2014/2015, na ili kuweza kutekeleza mpango kwa ufanisi ni dhahiri kuwepo kwa  umuhimu wa kubainisha vyanzo vya mapato vya uhakika ambavyo vitawezesha kugharimia miradi ya maendeleo inayokusudiwa, kuna haja ya serikali sasa kutafakari kwa kina na kuona kazi  kubwa  inayofanywa na kambi rasmi ya upinzani bungeni kuishauri serikali juu ya uongezaji wa mapato ya ndani ili kupunguza utegemezi wa kibajeti kila mwaka  inaweza kuijengea heshma nchi yetu na pia kuboresha huduma kwa wananchi wake na si kwa kutegemea mapato ya nje ambayo yameendelea kuidhoofisha nchi yetu mbele ya uso wa dunia kwa kuwa taifa tegemezi.

Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani, inapendekeza  kukusanya mapato ya ndani 25% ya GDP  ili kuweza kuendesha miradi yetu wenyewe. Uwezo wa makusanyo hadi kufikia hapo tunao, kwanza ni kupambana na makampuni makubwa ya kimataifa ili yalipe kodi stahiki na kuacha ujanja wa kukwepa kodi, kuondoa misamaha ya kodi na kuzuia upoteaji mapato ya ndani, Kuwaelimisha na kuwahamasisha wananchi wa kada zote  kulipa kodi kwa kuwawekea mazingira wezeshi na aminisho ya matumizi ya kodi zao. Ni dhahiri kuwa mapato ya ndani yaweza kutekeleza vipaumbele vyetu ili kukabiliana na matatizo tuliyoainisha.

Mheshimiwa Spika, katika miaka kadhaa kambi rasmi ya upinzani bungeni kwa nia njema ya kuijenga nchi yetu ilipendekeza mambo kadhaa  ili kuweza kuongeza mapato ya serikali na moja ya mambo yaliyopendekezwa ni kuhakikisha kwamba serikali inakusanya kodi kwa kiwango cha asilimia 30 kama ‘ongezeko la mtaji’ (‘capital gains’) kutokana na mauziano ya Kampuni yoyote ambayo mali zake zipo Tanzania.  Je, utekelezaji wa ushauri huo umefika wapi?

Mheshimiwa Spika, lakini pia Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni ilipendekeza kupunguza misamaha ya kodi hadi kufikia asilimia moja ya pato la Taifa kama wenzetu wa Uganda na Kenya. Serikali ilikubaliana na pendekezo hili kwa maneno lakini imeshindwa kulitekeleza licha ya kutoa ahadi za kufanya hivyo kila mwaka. Hivi sasa misamaha ya kodi imefikia asilimia 4.1 ya Pato la Taifa.
Mheshimiwa Spika, bajeti mbadala itatoa mgawanyo wa fedha kwa vipaumbele hivyo katika utekelezaji wake.
11. HITIMISHO
Mheshimiwa Spika, Tanzania ni nchi yenye wachumi wazuri na waliobobea na ukweli ni kwamba nchi jirani zimekuwa zikipanga mipango yake kwa kutumia wataalam wetu. Ni ukweli kwamba mipango ya hao wanaotumia mipango na wataalam wetu wameendelea kuliko sisi. Hoja kubwa ya kujiuliza ni kwanini kama mipango mizuri tunayo na wataalam tunao mambo hayaonekani kuwa yanasonga mbele?
Mheshimiwa Spika, tatizo la msingi hapa ni kuwa nchi zilizoendelea uchumi ndio unatakiwa kuongoza mfumo wa siasa, lakini kwetu sisi siasa ndio inaongoza mfumo wa uchumi kwa maana mipango yetu inapangwa kwa kuangalia zaidi matakwa ya kisiasa.
Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka Serikali kujikita zaidi kwenye kutekeleza mpango na sio kwenda kwa matakwa ya viongozi wa kisiasa kama inavyofanya  hivi sasa.
Mheshimiwa Spika, Mwisho lakini kwa umuhimu mkubwa, ni aibu kubwa kwa nchi makini na tajiri kama Tanzania kuendelea kupangisha ofisi kwa ajili ya mabalozi wake nje ya nchi wakati nchi inamiliki viwanja katika mataifa hayo, Serikali pia imeendelea kupanga nyumba za watumishi na maofisi kwa gharama za juu. Aidha, katika hilo ni kwa vipi nchi makini inauza nyumba za watumishi wake  hasa madaktari na kuwapatia viwanja vya kujenga nyumba zao maeneo ya mbali na sehemu wanazotolea huduma. Hii ndiyo mipango ya Serikali ya CCM au ni wizi wa viongozi Serikali? Hujuma hizi kwa taifa zinazofanywa na Mawaziri waliopewa dhamana ya kusimamia raslimali za watanzania lakini wanashindwa, Kambi Rasmi ya Upinzani inawataka Mawaziri wahusika wajipime kama kweli bado wanafaa kuendelea kuwa watumishi wa wananchi.
Mheshimiwa Spika, katika mazingira tatanishi kama haya ni lini tunaweza kujitapa kuwa tunafikia malengo ya milenia?
Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo kwa niaba ya kambi Rasmi ya Upinzani, naomba kuwasilisha.
……………….
Esther Nicholas Matiko(Mb)
Msemaji Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani- Ofisi ya Rais Mahusiano na Uratibu
16.06.2014


No comments:

Post a Comment