Monday, March 31, 2014

Mbunge Kamili:Mwenyekiti wa CCM alihusika kunitesa

Mbunge wa Viti Maalum (Chadema), Rose Kamili, aliyedai ametekwa na kuteswa wakati wa uchaguzi mdogo mkoani Iringa, amemtuhumu Mwenyekiti wa CCM mkoani humo, Jessica Msambatavangu kuwa anahusika na mashambulizi dhidi yake.

Kamili alidai alitekwa, kupigwa na kujeruhiwa wakati wa kampeni za uchaguzi mdogo wa jimbo la Kalenga uliofanyika mapema mwezi huu.

 Akizungumza kwenye mkutano na wanahabari  mjini Dodoma, siku moja baada ya kula kiapo cha kuwa mjumbe wa bunge maalum la katiba, alisema akiwa vijijini alikokwenda kusambaza mawakala wa  kusimamia uchaguzi wa  Kalenga, alitekwa na watu asiowafahamu ambao walimwingiza kwenye gari na hadi ofisi za CCM mkoani  Iringa.

“Nilipofikishwa katika ofisi hizo nilianza kushushiwa kipigo kikali hata kabla sijashushwa kwenye gari. Nilipelekwa  katika moja ya ofisi na kukutana  Mwenyekiti wa CCM Msambatavangu na kumtambua,”alisema.

Alieleza kusikitishwa na hatua ya mwanamke mwenzake  akimfanyia visa hivyo.
Alisema kuwa Msambatavangu aliamuru aletwe baunsa ambaye ndiye aliyeanza kumpa kipigo kikali huku kiongozi huyo akisisitiza apigwe  zaidi.

Alisema  baada ya kupigwa kwa zaidi ya dakika 20, lilikuja gari la polisi na  wakamweleza kuwa wamefika mahali hapo kwa ajili ya kumwokoa na kumchukua kumpeleka kituoni.

Kamili alisema  alipofikishwa polisi hali yake ilianza kuwa mbaya  ndipo  walipomwandikia fomu namba tatu  (PF3) na kumkimbiza  kwenye  matibabu.

Alisema anasikitishwa kuwa hata baada ya kumtaja mbaya wake polisi, mwenyekiti huyo hajakamatwa na badala yake yupo ndani ya bunge la katiba huku kukiwa hakuna hata jalada alilofunguliwa dhidi ya kiongozi huyo.

Aidha Kamili alilituhumu Bunge la Jamhuri ya Muungano kwa upendeleo wa dhahiri na kutojali madhila yaliyompata.

“Tangu nijeruhiwe hakuna tamko lolote  lililotolewa na uongozi wa Bunge kuhusiana tatizo lililonikuta, licha ya kuwa Spika ni mwanamke.”

Alisema mbali na kutoa tamko, hakuna msaada wowote wa kitabibu alioupata kutoka bungeni, lakini wabunge wa CCM wanapougua  bunge linakuwa mstari wa mbele kutoa huduma.

Umoja wa wabunge wanawake wa vyama vya Upinzani wametoa tamko la kulaani kitendo hicho na kuitaka Serikali ichukue hatua haraka kushungulikia tatizo hilo.

Akitoa tamko hilo mbele ya wandishi wa Habari, Mwenyekiti wa wabunge hao, Suzan Lyimo alisema kuwa kitendo alichofanyiwa mwanamke mwenzao ni kibaya kinachowakatisha  wanawake tamaa.

No comments:

Post a Comment