Sunday, February 2, 2014

Mdee; Kati ya watu 5 nchini, 3 Chadema.

MBUNGE wa Jimbo la Kawe, Halima Mdee, amesema kati ya watu watano (5) walioko nchini, miongoni mwao watatu (3) ni waumini na wapenzi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).
Mdee alisema, hali hiyo ndiyo inayoisababishia Serikali ipate kigugumizi cha kuboresha daftari la kura, kwa kudai ina kasungura kadogo (hakuna fedha), kumbe wanafahamu wakifanya hivyo, chama cha mapinduzi (CCM) kitakua kimekwisha kazi yake.
Akiwahutubia wakazi wanaozunguka Mji Mdogo wa Madizini, Vijiji na Vitongoji vya Mtibwa jana, Mdee alisema, kati ya watu watano (5) walioko nchini, miongoni mwao watatu (3) ni waumini na wapenzi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).
Mdee, aliyeambatana na, Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Freeman Mbowe (Mb), Mbunge wa Viti Maalum na Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Morogoro, Suzani Kiwanga katika Chopa, aliwataka akina mama wa Mvomero kuikataa CCM na Propaganda zake katika sanduku la kura.
“Kila adha mnayoipata akina mama ikiwa ni pamoja na kuporwa ardhi kunakofanywa na vigogo wastafu wa Serikali ya CCM na walioko madarakani, madhara yake ni kwenu na watoto wenu, hivyo tuungane kuikataa CCM na kuichagua Chadema, ili kiwaletee hali bora na matumaini mapya”.alisema Mdee.


Mbowe asema; DC Mtaka amekurupuka.

Awali MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe, alimnyoshea Kidole Mkuu wa Wilaya ya Mvomero, Antony Mtaka, akidai uamuzi wake wa kufunga Kiwanda cha Mtibwa hadi kitakapolipa madeni ya wakulima na Wafanyakazi , ‘amekurupuka’.
Mbowe alitoa kauli hiyo leo (jana) kufuatia malalamiko ya wananchi walioshitushwa na uamuzi wa Serikali kupitia kwa Mkuu wa wilaya hiyo, kuamua kufunga kiwanda badala ya kumnyang’anya, kutokana na Mwekezaji huyo kushindwa kukiendesha hivyo kudaiwa na wakulima na Wafanyakazi zaidi ya Sh. Bilioni 1.2/-
Akihutubia umati wa wananchi wa Mji Mdogo wa Madizini na vitongoji vyake, Mbowe alimnyoshea Kidole Mkuu wa wilaya Mtaka akisema, “Madeni anayodaiwa Mwekezaji huyu, suluhu yake siyo kufunga Kiwanda, bali Serikali iltakiwa kutafuta fedha ya kuwalipa wakulima na Wafanyakazi hao.
“Katika hili DC amekurupuka, wakulima na Wafanyakazi wanataka Malipo yao, habari ya uamuzi wa kufunga kiwanda, ni kumnusuru mdaiwa asiwajibike, na wala haisaidii dai la msingi la wananchi, hivyo kilistahili ni Malipo na kuiangalia adha hiyo kitaifa maana inahusisha watu wengi”.alisema Mbowe.
Mbowe aliwaita viongozi chadema wamwambie malalamiko ya wananchi ili wamtune Kambi upinzani bungeni ikamhoji Waziri Mkuu Mizengo Pinda, ambapo Diwani wa Kata ya Mtibwa, Luka Mwakambaya, alieleza Manyanyaso, Dhuluma na ucheleweshaji wa Malipo yanayofanywa na mwekezaji dhidi ya wananchi na kuahidi kuyafanyia kazi
Mbali na Mbowe kusisistiza tena kuhusu kuboreshwa kwa daftari la kura na mchakato mzima wa Katiba, ameendelea kudai, lisipoboreshwa daftari hilo Chadema haitakuwa tayari kuingia katika kura ya maoni, ila itarudi kwa umma kuwataka kususia mchakato huo, unaokumbatiwa na CCM.

No comments:

Post a Comment