Tuesday, January 14, 2014

Chadema yampitisha Mwimbaji wa Nyimbo za Injili Kuwania Udiwani.

HATIMAE Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Mkoa wa Dodoma, kimempitisha rasmi Mwimbaji wa Nyimbo za Injili wa Kanisa Kuu la Kianglikana Dodoma, Josiah Mtonyi,  kugombea udiwani wa Kata ya Mpwayungu, wilaya ya Chamwino.

Katibu Mkuu wa Chadema mkoani Dodoma, Stephen Masawe,  amethibitisha Chama chake kumpitisha Mtonyi kugombea nafasi hiyo na kwamba ameshachukua fomu na wana uhakika atatoa ushindani wenye ushindi kwa sababu mgombea wao anakubalika na wananchi wa Kata kwa ubora na uaminifu.

Mtonyi alichukua fomu hiyo katika Ofisi ya Kata hiyo mwishoni mwa wiki saa 10.18 jioni kwa Kaimu Mtendaji wa Kata ya Mpwayungu ambaye pia ni Mratibu wa Elimu Kata, Mwalimu Ester Musa, akisindikizwa na Umati wa watu kwa vifijo, ngoma na nderemo, wakiwemo viongozi wa Chadema Mkoa. 

Uchaguzi huo unafanyika kutokana na baadhi ya Madiwani kufariki, kupoteza Sifa na kujiuzulu ambapo Kata hiyo iko wazi kutokana na kifo cha aliyekuwa Diwani wa Kata na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Chamwino Dodoma, Laurent Hoya, aliyefariki Agosti 16, mwaka jana.

Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) hivi karibuni ilitangaza uchaguzi mdogo wa madiwani katika kata 27 za Halmashauri 23Februari 9, 2014.
Mtonyi ambaye ni Mhitimu wa Shahada ya Maendeleo Vijijini ya Chuo Kikuu cha Sokoine Morogoro, ameahidi kuwapatia Maendeleo ya Kielimu, Kiuchumi, Kiafya, Kijamii, Kisiasa na Kimawasiliano wananchi hao, kwa kile alichosema, wamemsomesha kwa tabu hadi alipofikia hapo, hivyo anataka kuwatumikia.

Mgombea Mtonyi (Chadema), atapambana vikali na Mgombea mwenzake wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Edward Mgaya, ambaye alipitishwa na Chama chake hivi karibuni, ambapo aliwashinda wenzake wanne katika kura za maoni katika Kata hiyo.


Aidha Wananchi waliohojiwa katika vitongoji na vijiji vinavyozunguka Kata ya Mpwayungu, wamesema hawana sababu ya kutomchagua Msomi Mtonyi wakidai ana sifa na ueledi wote, hana Kashifa wala tone la ufisadi, ameitendea Haki Jamii hiyo Kielimu na kadharika, hivyo wanaamini atawasaidia kimaendeleo.

No comments:

Post a Comment