Monday, January 27, 2014

Chadema waitaka CCM isikwamishe Katiba Mpya

Ngara/Njombe. 
Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe, amekitaka Chama Cha Mapinduzi (CCM) naSerikali yake kuacha kile alichokielezea kuwa ni hila ya kutaka kukwamisha mchakato wa Katiba Mpya.
Mchakato huo sasa unaelekea katika hatua ya Bunge Maalumu la Katiba. Amesema Watanzania hawako tayari kurudi nyuma kuendelea na katiba ya sasa.
Alikuwa akihutubia mkutano mkubwa wa hadhara huko Ngara, mkoani Kagera juzi, ambao ni sehemu ya operesheni ya Movement For Change (M4C) iliyopewa jina la ‘Pamoja Daima’.
Mbowe alisema yupo tayari kuwa wa kwanza kufungwa kwa kosa la kudai Katiba Mpya kama Serikali itaweka mazingira ya hila ambayo yatalazimisha kukwamisha mchakato wa kupata Katiba Mpya na kuwafanya Watanzania kuendelea na Katiba ya mwaka 1977.
Alisema watawala wasitumie hila na mwanya wowote kuitia nchi majaribuni kwa kulazimisha watu kuishi na katiba iliyokosa uhalali wa kisiasa na kisheria.
Alisema badala yake, wanatakiwa kuhakikisha kuwa kunakuwa na mazingira mazuri kwa Watanzania kujiamulia nama ya kuongozwa
Kiongozi huyo wa Chadema alisisitiza kuwa Katiba ni uhai wa taifa na si matakwa ya chama chochote cha siasa wala mtu binafsi.

Alisema Watanzania wengi wamependekeza kuwapo kwa shirikisho la Serikali tatu katika Rasimu ya Katiba Mpya, lakini akadai kuwa zipo njama zinazofanywa za kuchakachua uamuzi huo wa wananchi kwa ajili ya kukilinda CCM. Alisema kama hila hizo za kupindua maoni ya wananchi zitafanikiwa kupenyezwa kupitia bungeni, yuko tayari kuungana na Mtanzania yeyote kuzunguka nchi nzima kuwahamasisha wananchi waikatae rasimu hiyo.

Alisisitiza kwamba endapo wananchi wataikataa Katiba hiyo, pia hawatakuwa tayari kurudi kuendelea kutumia katiba ya zamani inayotumika hivi sasa kama ambavyo Serikali imekwishasema.

“Watawala lazima wajue. Watanzania hawa ambao wameipigania na kuililia Katiba Mpya kwa muda mrefu sasa hawako tayari tena kurudi nyuma,” alisema kiongozi huyo wa Chadema

No comments:

Post a Comment