Thursday, June 27, 2013

Msigwa: Makazi ya polisi yaboreshwe

Mbunge wa Iringa Mjini (Chadema), Mchungaji Peter Msigwa ameitaka serikali ieleze ni lini itawajengea askari nyumba bora ili waweze kuishi katika mazingira mazuri.Msigwa alitoa kauli hiyo jana Bungeni alipokuwa akiuliza swali la nyongeza kwa kuitaka serikali ieleze ni lini itawaboreshea makazi askari wa Jeshi la Polisi hususani askari wa Iringa Mjini kutokana na kuishi katika nyumba alizosema hazina hadhi.
“Mheshimiwa Mwenyekiti nataka serikali ieleze ni lini askari watajengewa makazi mazuri ili wasifanye kazi katika mazingira magumu ambayo huwafanya kushindwa kutekeleza wajibu wao ipasavyo?”, alihoji.
Akijibu, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Pereira Ame Silima alisema azma ya serikali ni kuhakikisha askari wote nchini wakiwa na makazi mazuri kadri bajeti inavyo ruhusu.
Alisema anakubaliana na wabunge kuwa kuna tatizo kubwa la makazi ya askari kutokuwa katika hali nzuri na kwamba serikali inatafuta fedha kwa ajili ya kuboresha makazi hayo.
Silima alisema serikali kwa kutumia mpango wa ushirikishaji umma itaendelea kutatua changamoto za ukosefu na uchakavu wa nyumba kwa Jeshi la Polisi.

No comments:

Post a Comment