Friday, January 11, 2013

MAONI KATIBA MPYA:Wadau wa habari wacharuka


  Wataka Wahariri walindwe, wasiingiliwe
  Pia serikali isimiliki vyombo vya habari
  Wafugaji: Rais asiwe na mamlaka ya ardhi
Wadau wa habari nchini wamependekeza Katiba mpya ijayo itamke na kutambua uhuru wa vyombo vya habari na kuwalinda Wahariri wasiingiliwe na chombo chochote wanapofanya kazi zao.

Kauli hiyo ilitolewa na wadau hao walipofika katika ofisi za Tume ya Mabadiliko ya Katiba ikiwa ni nafasi ya makundi maalum kutoa maoni yao.

Akitoa maoni kwa Tume hiyo, Mwenyekiti wa Chama Cha Wamiliki wa Vyombo vya Habari Nchini (MOAT), Dk. Reginald Mengi, alitaka itamkwe katika Katiba kwamba vyombo vya habari vipo huru pamoja na kuondoa vitisho dhidi ya vyombo hivyo ikiwamo sheria kandamizi ya magazeti ya mwaka 1976.

Dk. Mengi alisema MOAT inapendekeza Katiba itamke wazi kwamba kuanzisha chombo cha habari kusihitaji mtu kuomba leseni ya kukianzisha bali kianzishwe kama zinavyoanzishwa biashara nyingine.

Aidha, alisema MOAT inapendekeza kuanzisha vyombo huru vya habari vya dola ambavyo havitamilikiwa na serikali ili viweze kufanya kazi kwa uhuru na kwamba serikali isiruhusiwe kumiliki vyombo vya habari.

Dk. Mengi alipendekeza kuwe na kipengele katika Katiba ambacho kinalinda sekta ya elimu na kuwapo mipango ya kuinua pamoja na kutamka wazi namna ya kuwainua Watanzania kiuchumi.

Mapendekezo mengine yaliyotolewa na Mengi ni kuunda Mahakama maalum kwa ajili ya kushughulikia watu wanaotuhumiwa kutokana na vitendo vya rushwa.

Kwa upande wake, Mhariri mtendaji wa Gazeti la NIPASHE, Jesse Kwayu, akitoa maoni yake kwa Tume hiyo, alitaka Katiba mpya itamke kwamba sifa ya mtu kugombea nafasi ya ubunge iwe ni elimu ya Chuo Kikuu kuliko sifa ya kujua kusoma na kuandika ilivyo sasa.

Kwayu pia alipendekeza Rais kupunguziwa mzigo wa kuteua watendaji mbalimbali wa serikali na badala yake kazi hiyo kipewe chombo kingine.

Kuhusu uhai wa kuendelea kuwapo vyama vya siasa, Kwayu alipendekeza Katiba itamke kwamba kama chama katika uchaguzi hakikupata hata mwenyekiti wa serikali ya mtaa, diwani ama mbunge, kifutwe baada ya uchaguzi huo kumalizika kwa kuwa hakifai kuwapo.

Kwa upande Jukwaa la Wahariri Nchini (TEF), lilipendekeza kwa Tume kwamba kuwapo uhuru, haki ya kupata habari na haki ya kutoa maoni.

Akisoma tamko la TEF, Deodatus Balile, alitaka kuanzishwa Baraza la Taifa la Habari ambalo kazi yake itakuwa kusimamia vyombo vya habari na kuondolewa vizuizi vya kupata habari.

Kwa upande wake, Chama cha Wanahabari Wanawake (Tamwa), kilipendekeza kuwa Katiba mpya itamke haki za watoto na kuzilinda.

Akitoa mapendekezo yake, Mkurugenzi mtendaji wa gazeti la Mwanahalisi, Said Kubenea alitaka Katiba itamke kuwa Mkurugenzi wa Mashitaka ateuliwe na chombo huru na sio Rais pamoja na Rais asiwe na kinga ya kutoshtakiwa anapofanya makosa akiwa kazini na anapostaafu.

Wakati huo huo, Wafugaji jana waliwasilisha maoni yao kwa Tume ya Katiba na kutaka ardhi iwe chini ya wananchi na sio Rais kama ilivyo sasa pamoja na kutenga maeneo maalum kwa ajili ya ufugaji ambayo yatatambuliwa kisheria.

MAONI YA TASO

Nacho Chama cha Wakulima Tanzania (Taso), kimependekeza Katiba Mpya itambue umuhimu wa kilimo kwa kuwa ndiyo shina la maendeleo.

Mwenyekiti wa Taso, Engelbert Moyo, alisema jana kuwa kutokana na hilo katika mkutano wao na Tume jana, wamependekeza Katiba Mpya itamke kwamba, kilimo ni msingi wa maendeleo ya Watanzania wote kwa kuwa hivi sasa hakitambuliki hivyo kwa kuwa pia asilimia 80 ya Watanzania ni wakulima.

Alisema utaratibu wa kubadili misamiati ya kilimo ni mambo ya mpito, hivyo akasema wanataka katika Katiba Mpya kiwapo kifungu kitakachoibana serikali kuwekeza kwenye kilimo kufikia asilimia 15.

Kuhusu migogoro baina ya wakulima na wafugaji, alisema wamependekeza suala la umiliki wa ardhi lifafanuliwe kwa kina na Katiba Mpya.

Alisema katika hilo, wamependekeza uwapo mwongozo unaojulikana kwa wakulima na wafugaji kuhusu umiliki wa ardhi na matumizi yake.

Moyo alisema iwapo wakulima na wafugaji kila mmoja atajua hilo, migogoro ambayo imekuwa ikijitokeza mara kwa mara baina pande mbili hizo itaondoka.

MAONI YA APPT-MAENDELEO

Chama cha APPT-Maendeleo kimependekeza Katiba Mpya imlazimishe rais kuteua Watanzania wenye sifa za kushika nafasi kuanzia juu hadi chini kutoka chama chochote cha siasa na kwa wasio na vyama.

Rais Mtendaji wa Chama hicho, Peter Mziray, alisema jana kuwa katika katika uteuzi huo, wanataka rais aanzie na wale alioshindana nao, lakini kwa hiari zao, akisema jambo hilo litaleta mshikamano wa kitaifa.

Mbali na hayo, alisema pia wamependekeza rais asiwe mwenyekiti, au makamu mwenyekiti, au katibu mkuu wa chama chochote cha siasa, na pia asiruhusiwe kuvaa mavazi au nembo ya chama chake cha siasa.

Mziray alisema vilevile, wamependekeza rais asiruhusiwe kuonyesha alama ya chama chake cha siasa kwa kuwa ni rais wa nchi na siyo wa chama chochote cha siasa mara anapotangazwa mshindi, na pia wanataka rais asiwe na mamlaka ya kulivunja Bunge.

Alisema katika mapendekezo yao, pia wanataka mtuhumiwa wa kosa lolote lile apewe dhamana iwapo baada ya miezi mitatu upande wa mashtaka watakuwa hawajakamilisha upelelezi, na pia uwakilishi kwa njia ya kura ndiyo utumike katika uchaguzi.

Mziray alisema vilevile, wamependekeza viti maalum vya wanawake viondolewe ili kuweka usawa, kuondoa mfumo dume na watu wa jinsia zote wagombee kupitia majimbo ya uchaguzi na uwakilishi.

“Akina mama watapewa uungwaji mkono maalum ili waweze kushinda katika majimbo na uwakilishi. Kwani kwa mtazamo wetu, viti maalum vinawadhalilisha, kuanzia ndani ya vyama vyao hadi katika Bunge lenyewe,” alisema Mziray na kuongeza:

“Kwa mfano, ndani ya vyama wanadaiwa rushwa mbalimbali, ikiwamo ya ngono pamoja na manyanyaso mengine, kama vile viti vya wanawake, wachaguaji ni wanaume, mgombea uwe mtiifu kwa watu fulani ndiyo upitishwe, uwe familia ya wenye chama nakadhalika.

Kadhalika, alisema kuwa na wabunge 352 katika nchi maskini kama Tanzania, ni tatizo na kwamba, la kusikitisha zaidi katika hao, wenye kuchaguliwa na wananchi kutoka katika majimbo ya uchaguzi ni 233 tu.

“Sasa hawa wabunge 119 wanamwakilisha nani? Na ukizingatia wanalipwa mabilioni ya fedha za walipa kodi kwa maslahi ya nani?” alihoji Mziray.

Kutokana na hali hiyo, alisema wamependekeza kuwapo na wabunge wasiozidi 280, baraza la mawaziri na naibu mawaziri wasiozidi 30.

Alisema pia wamependekeza kuwapo Mahakama ya Katiba, ambayo itasikiliza kesi zote zenye utata ndani ya katiba yenyewe na itaweka wazi utaratibu wa wananchi wa kawaida kupeleka suala la kufuta kipengele chochote kinachowanyanyasa.

Mziray alisema pia mahakama hiyo hiyo ishughulikie mambo ya Muungano na pia Katiba iweke utaratibu wa jinsi gani ya kuuvunja Muungano uliopo.

Alisema ikiwa watu hawautaki, upande mmoja wa Muungano uweze kufungua kesi katika Mahakama ya Katiba kuhusu shauri kama hilo na kwamba, Katiba itumikie wananchi na siyo wananchi watumikie katiba.

Mziray alisema pia wamependekeza chama tawala kirudishe mali za umma serikalini kwa kuwa mali zote zilizochumwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) wakati wa chama kimoja, zinawahusu wote.

Z’BAR WATAKA SERIKALI MBILI


Wakati huo huo, Mwandishi Wetu Mwinyi Sadallah, kutoka Zanzibar anaripoti kwamba vyama vinne vya siasa vimeungana na Chama cha Mapinduzi (CCM) kutetea Muungano wa Serikali mbili kupinga mfumo wa muungano mkataba ambao unatetetwa na chama cha Wanananchi  (CUF) na baadhi ya wanaharakati Zanzibar.

Vyama hivyo vimetoa msimamo huo muda mfupi baada ya kutoa maoni mbele ya Tume ya Katiba chini ya Mwenyekiti wake, Jaji Joseph Warioba aliyeambatana na Makamu wake, Jaji Augustino Ramadhan.

Vyama hivyo ni Tadea, Jahazi Asilia, NLD na Chama Cha wakulima Tanzania (AFP) ambao wamesema mfumo wa Muungano wa mkataba iwapo utazingatiwa katika mabadiliko ya katiba ni mwanzo wa kuuvunja.

Katibu Mkuu wa Tadea, Juma Ali Khatib alisema chama chake kinapinga mfumo wowote unaoashiria kuvunja Muungano ikiwemo muundo wa Muungano wa mkataba unaoruhusu Zanzibar kuwa na mamlaka yake nje ya nchi.

Khatib alisema kwamba Tadea inaafiki muungano wa serikali mbili na kwamba mfumo wowote unaoashiria kuvunja muungano wa Tanzania ni hatari kwa mustakabali wa amani na ulinzi wa nchi.

“Tunafikiri mfumo wa serikali tatu na mkataba hatma na dhamira yake ni kuvunjika kwa muungano mfumo pekee utadumisha muungano ni kuendelea na serikali mbili yaani ya Muungano na ya Mapinduzi Zanzibar,”alisema Khatib.

Msimamo kama huo uliungwa mkono na Naibu Katibu Mkuu wa Jahazi Asilia, Jabir Mtumweni aliyesema kwamba lazima kuwepo kwa Muungano wa maridhaino wa pande mbili ikiwemo Rais wa Zanzibar kurejeshewa wadhifa wake kama Makamu wa Rais wa Muungano.

Mtumweni alisema Zanzibar ipewe nafasi ya kutambulika kimataifa chini ya mfumo wa serikali mbili na kupendekeza mambo ya nje yabaki kuwa ya muungano na Zanzibar ikipewa fursa ya kuwa na mahusiano ya kujiunga na taasisi za kimaitaifa.

Mkurugenzi wa Sera ma Uendeshaji wa AFP, Rashid Mchenga alisema Muungano wa Serikali mbili ndiyo usalama wa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar na kutaka Tume ya mabadiliko ya katiba kuzingatia maoni yanayolenga kulinda amani na umoja wa kitaifa baina ya pande mbili za Muungano.

Alisema Muungano iwapo utavunjika Zanzibar inaweza kuathirika kutokana na kuwa na eneo dogo la ardhi na watu wake wengi kuishi nje ya visiwa hivyo.

Alisema kwamba kwa kuwa Zanzibar uchumi wake ni mdogo, mabadiliko ya katiba yaangaliwe gawio la Zanzibar kutoka katika mapato ya Muungano ifikie asilimia 15 badala ya asilimia 4.5 ya sasa.

Kwa upande wa Naibu Katibu Mkuu wa NLD, Khamis Haji Mussa alisema masuala ya utafiti na takwimu, biashara ya nje na elimu kila upande ni vyema ukaendesha wenyewe.

Mussa alisema makao makuu ya baadhi ya taaasisi, mashirika ya umma na sekta za wizara ya Muungano yawe Zanzibar ili kuonyesha mizania ya muungano.

Wakati hayo yanatokea, Jaji Warioba jana alivunja ukimya na kukosoa sera ya CUF  kuwa ina kasoro kutokana na viongozi Zanzibar kuwa ni watetezi wa Muungano wa mkataba wakati wenzao wa Bara wakitaka Muungano wa Serikali tatu.

Katika kikao hicho Jaji Warioba ambaye ni Waziri Mkuu mstaafu aliwashauri viongozi wa kitaifa wa chama hicho kukaa pamoja na kuwa na msiomamo wa pamoja wa kisera kuhusu  muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

Alisema tofauti hizo zinaifanya Tume yake kubaki njia panda na kushindwa kufahamu sera ya kitaifa ya chama hicho ni ipi kati ya hizo mbili.

Katika hatua nyingine Mwenyekiti wa chama cha Democratic Party Mchunganji Chriostopher Mtikila alisema anajipanga kufungua kesi katika umoja wa Afrika (AU) ili Tume ya Warioba isitishe mara moja kazi ya kukusanya maoni ya uundwaji wa katiba.

Akizungumza na NIPASHE kabla ya kikao hicho Mtikila alisema Tume hiyo kimsingi haiwezi kutenda haki kwasababu inafanya kazi kwa kuwafurahisha watawala badala ya wananchi wanyonge wasiofaidi rasilimali za nchi yao.

Alisema Tume hiyo ilitakiwa kuundwa na wananchi na siyo serikali na ndiyo maana imeamua kufanya kazi zake kwa siri na kuzuia waandishi wa habari.

Kama kawaida Tume hiyo imendelea na utaratibu wake mpya wa kuzuia waandishi wa habari kuingia katika kumbi za kutoa maoni baada ya mwandishi wa habari hizi jana kutimuliwa na watendaji wa tume hiyo.
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment