Tuesday, January 1, 2013

SERIKALI ITOE MAELEZO YA KINA KWA VIJANA NA WANACHI WA MTWARA KWA UJUMLA JUU YA RASILIMALI YA GESI ASILIA


SERIKALI ITOE MAELEZO YA KINA KWA VIJANA NA WANACHI WA MTWARA KWA UJUMLA JUU YA RASILIMALI YA GESI ASILIA
Wananchi wa Mtwara wameandamana kupinga zoezi la serikali kusafirisha gesi asili inayotoka mkoani humo hadi Dar es salaam. Wengi wa walioandamana walikuwa ni vijana waliobeba mabango yenye ujumbe mbalimbali kwa watawala kuhusiana na rasilimali hiyo.
Kwetu sisi BAVICHA, wananchi wa Mtwara hususan vijana wana haki ya kupinga hilo kwa sasa ili kuepuka yale yanayotokea kwenye maeneo mengine ya nchi yetu ambayo rasilimali zake zimekuwa zikitapanywa huku si wananchi wa eneo husika wala taifa wakinufaika vyema na rasilimali hizo hasa kwa Maendeleo endelevu. Maeneo yenye mathalani migodi ya dhahabu na almasi ni kielelezo tosha cha jambo hili.
Wanachopinga Vijana na wananchi wa Mtwara kimsingi sio gesi kusafirishwa kwenda Dar es salaam bali ni wao kuelezwa na kuoneshwa watanufaika vipi na gesi asili  jambo ambalo serikali haijaweza kulifanya mpaka sasa.
Maandamano ya watu wa Mtwara hususani vijana kwa upande mwingine ni kielelezo tosha cha jinsi sera za Chama cha Mapinduzi zilivyofubaa na hivyo kutokidhi haja za watanzania ambao mpaka sasa ni maskini wa kutupwa.
Mfumo mbovu wa utawala wa Tanzania chini ya serikali ya CCM ndio umetufikisha hapa na wananchi wa Mtwara na mikoa ya jirani wanapaswa kuelewa hilo. Kwani kwa sasa mfumo huu umeweka mamlaka yote ya kuamua la kufanya Dar es Salaam (Ikulu) juu ya rasilimali za taifa bila kujali mahitaji halisi ya wakazi wa eneo husika na hata taifa kwa ujumla  . Na kwenda kinyume kivitendo na kile wanachokihubiri kuwa na “serikali sikivu” kumbe ni “serikali kiziwi na babe”.
BAVICHA inasisitiza kuwa tatizo la matumizi  mabovu ya rasilimali si la Mtwara pekee bali ni la nchi nzima ambako rasilimali nyingi ambazo matumizi yake mpaka sasa hayajawanufaisha wakazi wa maeneo hayo wala taifa. Serikali ya CCM haina sera makini na daima haitakuwa nazo zaidi ya ubabaishaji uliopo na ambao umekuwapo kwa zaidi ya miaka 51 sasa.
BAVICHA inawataka Vijana na wananchi wa Mtwara na Tanzania kwa ujumla kuelewa kuwa mbadala halisi wa sera haramu ya CCM na Serikali yake ambayo CHADEMA imekuwa ikiwaeleza wananchi ni ile ya kubadili mfumo wa utawala wa sasa wa kila kitu kuamuliwa Dar es salaam na kuweka mfumo mpya unaotokanana sera ya MAJIMBO. Sera ambayo licha ya kuhakikisha matumizi sahihi ya rasilimali za taifa kwa manufaa ya taifa zima, pia unawapa mamlaka wananchi wa eneo husika lenye rasilimali hizo kuamua njia bora za kuzitumia rasilimali hizo kwa maslahi yao pia na kuhakikisha maslahi ya taifa zima.
Kwa sera hii ya CHADEMA ya mfumo mpya ya Utawala kwa njia ya MAJIMBO, rasilimali kama ya Gesi asili ingekuwa msaada kwa wananchi wa eneo la Mtwara (na Lindi) ambako mitambo ya gesi ingefungwa huko Mtwara (na Lindi) na kuzalisha  kama ni umeme ungezalishwa huko huko na kuingizwa kwenye gridi ya taifa. Kama ni viwanda basi vingejengwa Mtwara (na Lindi) na kuzalisha bidhaa husika na kisha kusafirishwa kwenye maeneo mengine ya nchi yetu. Kwa mtindo huu ajira kwa Vijana wa Mtwara na maeneo ya jirani zingepatikana kwa wingi na kuinua uchumi wa watu wa Mtwara na Lindi. Jambo ambalo lingeondoa tatizo la uhamaji wa nguvu kazi toka vijijini kuja mijini kama Dar es Salaam ambalo kwa sasa linakua siku hata siku.
BAVICHA tunasisitiza pamoja na wanachi wa Mtwara na hata mikoa  mingine ambayo ina rasilimali nyingi ambazo mpaka sasa zimegeuka kuwa laana kwa taifa hili, kupinga kitendo hiki cha matumizi mabovu ya rasilimali, wanapaswa kuunga mkono Sera ya CHADEMA ya kuweka mfumo mpya wa Utawala wa MAJIMBO ambao utazuia ukwapuaji na utoroshaji wa rasilimali hizi kutoka kwenye mikono ya wanachi wa Tanzania. Ni Mfumo ambao licha ya  kuweka rasilimali hizi kama gesi ya Mtwara (na Lindi) mikononi mwa wananchi, pia itawapa nguvu ya kufanya maamuzi yao  juu ya rasilimali hizo na kuwawajibishwa viongozi wao wanaoshirikiana na kikundi cha watu wachache kuzitorosha na kuwaacha wao wananchi wakiwa wasindikizaji kama si washangaaji wa matumizi ya rasilimali zao. Na hii ndiyo demokrasia ya kweli kwa maendeleo endelevu kwa taifa kwa kuhakikisha ushirikishi hai na mpana wa wananchi wote.
Imetolewa leo tarehe 30/12/2012 Jijini Dar es salaam na:
Deogratias Munishi
Katibu Mkuu –BAVICHA

No comments:

Post a Comment