Wednesday, August 1, 2018

HALIMA MDEE NA WANACHAMA 13 WA CHADEMA WASHIKILIWA NA JESHI LA POLISI KAWE

Mwenyekiti wa BAWACHA Taifa na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama, Halima Mdee (Mb) pamoja na viongozi wengine, wanachama na wapenzi wa CHADEMA Jimbo la Kawe takriban 13, wamekamatwa na wanashikiliwa na Jeshi la Polisi Kituo cha Polisi Kawe.

Hadi sasa jeshi hilo halijatoa taarifa rasmi kueleza sababu ya kumshikilia mbunge huyo pamoja na wananchi wake baada ya kuwakamata maeneo ya Tanganyika Parkers, Kawe, jijini Dar es Salaam.

Awali, Mdee ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Kawe, alisimamishwa na wananchi alipopita maeneo hayo, wakitaka kumpatia kero zao. Baada ya kusikiliza malalamiko ya wapiga kura wake na kuondoka, inadaiwa polisi walifika eneo hilo na kuanza kuwakamata walioonekana kuwa na sare za CHADEMA. Alipopata taarifa hizo, Mdee alilazimika kurudi ambapo polisi hao wakiongozwa na Askari Polisi mwenye cheo cha Inspekta walimuamuru Mdee na viongozi hao kuelekea kituoni. Hadi sasa viongozi hao bado wako kituoni hapo.

Tumaini Makene.
Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano CHADEMA.



No comments:

Post a Comment