Wednesday, December 28, 2016

Viongozi 22 wa kitaifa CHADEMA kuzindua kampeni kanda ya Kaskazini

Viongozi 22 wa kitaifa wa Chadema wanatarajia kushiriki uzinduzi wa kampeni za uchaguzi mdogo wa udiwani katika kata nne za mikoa ya Arusha, Manyara na Kilimanjaro kuanzia kesho.

Kampeni hizo zitazinduliwa kwenye Kata ya Duni, mjini Babati ambako chama hicho kimemteua Ally Muhidini kugombea udiwani.

Katibu wa Chadema Kanda ya Kaskazini, Aman Golugwa amesema watazindua kampeni kwa kila kata ikiongozwa na viongozi wa kitaifa na wabunge.

Golugwa amesema wabunge 22 wa Chadema Kanda ya Kaskazini wamepangwa kusimamia kata hizo na kwamba wanne watakuwa katika kata moja. Pia, madiwani 352 wa chama hicho katika kanda hiyo watashiriki kwenye kampeni.

“Tumejipanga kushinda kata zote, katika uchaguzi uliopita tulishinda kata moja tu kati ya hizi nne,” amesema.

Golugwa amesema uzinduzi wa kampeni kwenye kata nyingine tatu utatangazwa baadaye. Hata hivyo, amesema wameshaanza kampeni za nyumba kwa nyumba ili kuhakikisha Januari 22 wanashinda viti hivyo.

No comments:

Post a Comment