Saturday, September 10, 2016

CHADEMA KUFUNGUA KESI KUOMBA MAHAKAMA KUU KUAMURU JESHI LA POLISI KUWAFIKISHA MAHAKAMANI WAFUASI WAKE WANAOSHIKILIWA KATIKA VITUO MBALIMBALI






CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimesema kinakusudia kufungua maombi katika Mahakama Kuu ya kuiomba mahakama hiyo kuiamuru Polisi kuwafikisha mahakamani watu wanaoshikiliwa katika vituo mbalimbali vya polisi jijini Dar es Salaam.

Hatua hiyo inatokana na chama hicho kudai kuwa kuna watu 10 ambao wanashikiliwa katika Kituo Kikuu cha Polisi (Central) na Kituo cha Oysterbay vya Dar es Salaam kwa zaidi ya wiki mbili bila kupewa dhamana ya polisi au kufikishwa mahakamani.

Kauli hiyo ya Chadema imetolewa na Mwanasheria Mkuu wa chama hicho, Tundu Lissu wakati akizungumza na waandishi wa habari makao makuu yake yaliyo mtaa wa Ufipa, Kinondoni jijini Dar es Salaam leo mchana.

Akifafanua kuhusu Habeas Corpus alisema, ni mamlaka iliyonayo Mahakama Kuu ya kuamuru mamlaka yoyote ya kiserikali inayomshikilia mtu kumpeleka mtu huyo mahakamani.

Lissu alisema, vijana hao walikamatwa katika mikoa mbalimbali kwa makosa aliyodai kuwa ni kujihusisha na haraka za kinachoitwa Umoja wa Kupambana na Udikteta (UKUTA) pamoja na masuala mengine ya kisiasa.

“Kama ikifika Jumanne hawajapelekwa mahakamani au hawajapewa dhamana ya polisi, tutakwenda Mahakama Kuu kufungua maombi ya habeas corpus, imuite IGP au DCI au Ma-RPC au wakuu wa vituo wanakoshikiliwa hao waeleze kwa kwanini wanawashikilia hao watu kwa zaidi ya wiki mbili,” alisema Lissu

Lissu alisema tayari wameshaanza maandalizi ya hati hizo ambazo zitapelekwa Mahakama Kuu ili iweze kuwaita kati ya Mkuu wa Polisi (IGP), Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DCI), Makamanda wa Polisi wa Mikoa au Wakuu wa Vituo vya Polisi wanakoshikiliwa watu hao.

Alifafanua kuwa alionana na watu hao ambao wamedai mbali na kushikiliwa lakini pia wamepigwa na kuteswa huku wakidai kuwa wamekuwa wakichukuliwa usiku na kupelekwa katika eneo lililopo Mikocheni ambako wanateshwa na kurudishwa polisi.

Alisema jeshi la polisi linakiuka sheria na haki za binadamu kwa kuwashikilia watu hao kwa muda mrefu bila kuwapa dhamana au kuwafikisha mahakamani kwa ajili ya kusomewa mashitaka.

No comments:

Post a Comment