Tuesday, June 16, 2015

Chadema yakosoa ahadi watangaza nia CCM.

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema utitiri wa viongozi wa serikali kujitokeza kuchukua fomu ya kuomba kugombea urais ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu ni sawa na kuidhalilisha taasisi ya urais.

Aidha, kimesema idadi kubwa ya mawaziri kukimbilia kuwania urais kinaonesha kuwa huenda hawaridhishwi na utendaji kazi wa serikali ya chama chao, inayoongozwa na Rais Jakaya Kikwete.

Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Taifa kutoka Zanzibar, Salum Mwalimu, alisema hayo juzi wakati akihutubia mamia ya wakazi wa Manispaa ya Musoma katika mkutano wa hadhara uliofanyika viwanja vya Shule ya Sekondari Mara.

Alisema hatua ya wagombea wa CCM kila mmoja kuonyeshwa kuchukizwa na vitendo vya rushwa, umasikini unaosababishwa na Serikali iliyopo madarakani ni sawa na dharau kwa serikali yao.

Mwalimu alisema Watanzania hivi sasa wamechoka na umasikini, dhuruma na rushwa unaosababishwa na uongozi mbovu wa Serikali ya CCM.

“Kila mmoja anasema atakomesha rushwa, ufisadi na kukuza uchumi, maana yake ni nini kama siyo kejeli na dharau kwa Serikali yao ya CCM…sisi tukishinda tutamsaidia Rais Kikwete kupata mapumziko mema kwani wenzake hasa mawaziri wamemchoka,” alisema.

Kuhusu mgombea urais wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), alisema timu ya viongozi wa umoja huo itakayoongoza Serikali ya awamu ya tano itakuwa kama timu ya soka ya Barcelona na mgombea wake wa urais ni kama Lionel Messi.

Mwalimu alisema Ukawa wamejipanga vizuri kuhakikisha watakapoingia madarakani Oktoba mwaka huu wanashughulikia matatizo yanayowakabili wananchi, ikiwamo kukomesha rushwa, dhuluma, ufisadi, umasikini na kuboresha huduma zote za jamii.

“Serikali ya Ukawa itaendesha nchi kwa mfumo wa 4, 4, 2 yaani Morinho staili. Tutakomesha ufisadi, rushwa na kuwapeleka mchakamchaka Watanzania katika kumiliki uchumi unaostahili kimataifa,” alisema.

Alisema wananchi wamechoka na uongozi mbovu wa Serikali ya CCM na kwamba serikali itakayoundwa na Ukawa itajenga na kuimarisha viwanda, reli, kukuza uchumi na ajira, kuboresha huduma za afya, maji, elimu na kudhibiti rushwa mahakamani, polisi na taasisi zote za umma.

Mwalimu aliwasihi wananchi kujitokeza kwa wingi kujiandikisha kwenye daftari la wapiga kura, ili wapate fursa ya kuiangusha CCM na kuiweka madarakani Serikali ya Ukawa.

No comments:

Post a Comment