Wednesday, February 4, 2015

Ndesamburo ajitwisha mgogoro wa ardhi Moshi

Mjumbe wa Baraza la Wadhamini wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na Mbunge wa Moshi Mjini, Philemon Ndesamburo, amejitwika ‘msalaba’ wa mgogoro unaohusu tuhuma za uporaji wa uwanja wa wazi wa Manispaa ya Moshi, baada ya kuingilia kati na kumtaka Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kuwapumzisha kazi watendaji wanaodaiwa kuhusika katika sakata hilo, la sivyo atawasilisha hoja ya dharura Bungeni.

Alisema kama Ofisi ya Waziri Mkuu, haitaona umuhimu wa kumaliza mgogoro huo, unaoweza kuchochea hasira za wananchi dhidi ya watendaji wa serikali; atamwomba Spika wa Bunge, Anna Makinda, kuwasilisha hoja ya dharura katika mkutano wa 18 unaoendelea ili wabunge wajadili kwa kina suala la uporaji wa viwanja vya umma na kumilikishwa baadhi ya matajiri au vikundi vya watu. Ndesamburo, alikuwa akizungumza jana na Waandishi wa habari kuhusu tuhuma za rushwa na uporaji wa uwanja wa wazi wa Mawenzi, wenye usajili namba L.O 9850 na hati namba 10660 ambao Manispaa ya Moshi imekuwa ikiumiliki kwa zaidi ya miaka 33 sasa.

“Nitapeleka hoja ya dharura Bungeni kuomba wabunge, wajadili sakata la uporaji wa maeneo ya wazi ya serikali kama Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Hawa Ghasia na Waziri Mkuu mwenyewe (Pinda), watashindwa kumaliza mgogoro huu kwa kufanya maamuzi magumu ya kuurejesha uwanja huo kumilikiwa na Manispaa ya Moshi,” alisisitiza. Alisema mojawapo ya dokezo la serikali lililotolewa linachochea Halmashauri hiyo kunyang’anywa karibu asilimia 80 ya maeneo yote inayohodhi kwa vile yanasomeka hati za wamiliki wa zamani.

Wiki mbili zilizopita, theluthi mbili ya madiwani wote wanaounda Baraza la Halmashauri ya Manispaa ya Moshi, lilipitisha azimio la kuitaka Mamlaka ya Uteuzi, (Rais, Kikwete), kumsimamisha kazi mara moja Mkurugenzi Mtendaji wa Manispaa hiyo, Shaaban Ntarambe, kutokana na kutuhumiwa kuhusika kwake katika sakata hilo.

No comments:

Post a Comment