Friday, January 17, 2014

Rais Jakaya Kikwete amwondoe Prof. Jumanne Maghembe nafasi ya Waziri wa Maji

TAARIFA KWA UMMA
Rais Jakaya Kikwete amwondoe  Prof. Jumanne Maghembe nafasi ya Waziri wa Maji kwa kushindwa kuchukua hatua za haraka za kuongeza upatikanaji wa maji safi na ushughulikiaji wa maji taka katika Jiji la Dar Es Salaam na nchini kwa ujumla.
Rais Kikwete azingatie kwamba tarehe 10 Januari 2014 nilimtumia ujumbe Waziri Maghembe kumshauri ajiuzulu kutokana na kujirudia rudia kwa matatizo ya maji katika Jiji la Dar Es Salaam kinyume na maelezo yake ya uongo  aliyoyatoa bungeni tarehe 4 Februari 2013.
Aidha, kufutia maelezo yaliyotolewa na Mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dar es Salaam (DAWASA) Hawa Sinare kuhusu sababu za kuchelewa kwa miradi ya maji Jijini na majibu ya Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Maji Safi na Maji Taka Dar es Salaam (DAWASCO) Jackson Midala kuhusu kujirudia kwa matatizo ya maji; Rais Kikwete akumbuke ahadi yake ya kuitisha kikao Ikulu kujadili masuala maji mwezi Machi 2013 ambayo mpaka sasa hajaitekeleza.
Ikumbukwe kwamba mara baada ya kujirudia kwa matatizo ya maji katika Jiji la Dar Es Salaam niliwasiliana na mamlaka husika ziweze kuchukua hatua na pia nilitaka Wenyeviti wa Bodi na Watendaji wakuu wa Mamlaka zinazohusika na huduma ya maji jijini (DAWASA na DAWASCO) watoe maelezo kwa umma juu ya sababu za kweli za matatizo za matatizo hayo.
Kwa nyakati mbalimbali kati ya tarehe 10 na 14 Januari 2013 viongozi na watendaji mbalimbali wa DAWASA na DAWASCO walitoa maelezo yenye kuonyesha kwamba matatizo ya maji Jijini Dar Es Salaam yanayoendelea hivi sasa ni matokeo ya kudaiwa fedha za kulipia umeme na TANESCO, uchakavu wa mitambo, kuchelewa kutekelezwa kwa miradi, wizi na upotevu wa maji.
Rais Kikwete azingatie kwamba maelezo yaliyotolewa yanadhihirisha kwamba Wizara ya Maji, DAWASA na DAWASCO pekee hawawezi kukamilisha hatua za haraka hivyo mamlaka za juu ziingilie kati kuepusha Serikali kuendelea kupata hasara, uchumi wa nchi kuathirika na ugumu wa maisha kwa wananchi kuongezeka kwa kuzingatia kwamba maji huduma ya msingi ya kijamii na malighafi muhimu katika uzalishaji.
Rais Kikwete arejee hoja binafsi niliyowasilisha bungeni tarehe 4 Februari 2013 kuhusu hatua za haraka za kuongeza upatikanaji wa maji safi na kuboresha ushughulikiaji wa maji taka katika Jiji la Dar Es Salaam (Nimeambatanisha nakala ya sehemu ya hoja hiyo inayohusu mapendekezo ya hatua nane za haraka).
Rais Kikwete atambue kwamba ingejadiliwa na maazimio yote kutekelezwa matatizo ya maji katika Jiji la Dar Es Salaam na nchini kwa ujumla mpaka hatua ya sasa yangekuwa yamepungua katika maeneo mbalimbali kutokana na hatua ambazo nilipendekeza zichukuliwe.
Hata hivyo, badala ya kuunga mkono hoja hiyo ambayo ingeisaidia Wizara yake  na kurekebisha udhaifu uliokuwepo na hivyo kumrejeshea imani kwa umma ambavyo ilikuwa imepungua; Waziri Maghembe akaamua kinyume cha kanuni za Bunge kutoa hoja ya kuondoa hoja niliyowasilisha kwa maelezo kuwa Serikali inaendelea vizuri na utekelezaji.
Kwa kuwa toka Februari 2013 mpaka Januari 2014 imebainika kwa nyakati mbalimbali kwamba utekelezaji hauendi kama Serikali ilivyoahidi na kwamba kuna udhaifu wa usimamizi katika ngazi mbalimbali ikiwemo wizarani, ni muhimu Rais amwondoe Prof. Maghembe kuwa Waziri wa wizara hiyo.
Wenu katika uwakilishi wa wananchi,
John Mnyika (Mb)
14/01/2014




No comments:

Post a Comment