Sunday, November 10, 2013

Lissu: CCM wana chuki na Warioba

MNADHIMU wa Kambi ya Rasmi ya Upinzani Bungeni, Tundu Lissu, jana alichafua hali ya hewa akisema kuwa CCM ina chuki na Tume ya Mabadiliko ya Katiba inayoongozwa na Jaji mstaafu Joseph Warioba.
Kwa mujibu wa Lissu, ambaye pia ni Mbunge wa Singida Mashariki (CHADEMA), Warioba na wenzake waliingiza mapendekezo ya serikali tatu kwenye rasimu, kinyume cha msimamo wa CCM.
Lissu aliibua tafrani hiyo bungeni jana wakati akichangia hoja ya kuunga mkono mapendekezo ya Mbunge wa Ubungo, John Mnyika, katika muswada wa marekebisho ya sheria ya mabadiliko ya Katiba akitaka mapendekezo ya serikali ya kuivunja Tume ya Katiba mara baada ya kukabidhi rasimu ya pili kwa Bunge Maalumu la Katiba yabadilishwe.
Badala yake, Mnyika alitaka tume hiyo iendelee na kazi hadi Bunge Maalumu la Katiba litakapomalizika ili kusaidia kutuoa ufafanuzi wa hoja zitakazojitokeza. 
Akichangia hoja hiyo baada ya wabunge kadhaa wa CCM kuwa wameipinga, Lissu alisema anajua kwanini hawataki.
“CCM wana chuki na tume ndiyo maana wanataka ivunjwe, isiwepo kabisa wakati wa Bunge Maalumu, sababu ni yule mzee Warioba kuingiza mapendekezo ya muundo wa serikali tatu ambao hawautaki.   
“Kwa hiyo hawa wanataka wale wajumbe wasiwepo kabisa maana wameingiza mambo kinyume cha matarajio yao,” alisema Lissu na kuongeza kuwa CCM wamefikia hata hatua ya kupingana na mwenyekiti wao katika hilo.
Baada ya Lissu kuketi, Lukuvi alisimama kwa hamaki akiomba kutoa taarifa huku akijigamba kuwa lazima afichue siri ya jambo hilo ingawa hakutaka kufanya hivyo.
“Mh. Spika alichokisema Lissu ni uongo, CCM haijawahi kupendekeza jambo hilo. Naomba nitoe siri, maana mimi nilikuwa mwenyekiti wa vikao hivyo vya majadiliano kati ya rais na vyama,” alisema.
Huku wabunge wakimsikiliza kwa umakini, Waziri Lukuvi alisema pendekezo hilo lililetwa na CUF kwa maandishi chini ya uwakilishi wa Naibu Katibu Mkuu wao (Bara), Julius Mtatiro.             
“Nasema siri hiyo ili mjue kuwa hilo ni wazo la CUF mshirika wa CHADEMA wala si la CCM,” alisema.
Wakati huohuo, Bunge lilikataa pendekezo jingine la Mnyika la kutaka idadi ya wajumbe wa tume wa kutoka kwenye makundi iongezeke kutoka 166 hadi 292, tofauti na pendekezo la serikali na kutoka 166 hadi 201.
Muswada huo ambao ulikuwa na mapendekezo matano ya serikali yaliyofikiwa baada ya majadiliano kati ya rais na vyama, ulipitishwa kwa pamoja na wabunge wote wakiuunga mkono.

No comments:

Post a Comment