Thursday, September 12, 2013

CHADEMA yampuuza Nape

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimempuuza Katibu wa Halmashauri Kuu (NEC) ya CCM, Nape Nnauye, kikisema kuwa madai yake yanalenga kuhamisha wananchi kwenye hoja.
Mkurugenzi wa Mawasiliano na Habari wa CHADEMA, John Mnyika, amesema kuwa madai hayo ya Nape yanadhihirisha kile alichowahi kukisema bungeni kuwa nchi imefika hapa ilipo kutokana na upuuzi wa CCM.
Kauli ya CHADEMA inafuatia madai yaliyotolewa na Nape juzi mjini Kahama, mkoni Shinyanga juzi kwenye mkutano wa hadhara kuwa chama hicho kupitia kwa katibu mkuu wake kilipewa fedha na wafadhili nje ya nchi ili kuvuruga mchakato wa Katiba unaoendelea sasa.
Mnyika alisema kuwa ameshangazwa na madai hayo ya Nape ambayo aliyaita ya kipuuzi kutolewa mbele ya Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana.
“CCM kupitia Nape imetoa madai hayo kwa lengo la kuhamisha mjadala kutoka kwenye muswada mbovu wa sheria ya marekebisho ya Katiba uliopitishwa kwa nguvu bungeni,” alisema.
Alisema kuwa Katibu wao Mkuu, Dk. Willibrod Slaa, hajawahi kupewa fedha zozote nje ya nchi kwa ajili ya kukodi helikopta ili kuvuruga mchakato wa Katiba kama alivyodai Nape.
Aliongeza kuwa katika tukio hilo kanuni za Bunge zilivunjwa na Naibu Spika, Job Ndugai, hivyo kuathiri hadhi na heshima ya Bunge kwa kuruhusu wabunge kushambuliwa, kudhalilishwa na kuhamishwa bungeni na watu wasiohusika.
Mnyika alihoji kuwa kwenye udhaifu kama huo wa kiti cha spika kwa maelekezo ya CCM inawezekanaje CHADEMA kuvuruga mchakato huo unaoendeshwa kimizengwe licha ya wao kuwa waasisi wa hoja ya Katiba mpya.
“Madai ya CCM kupitia Nape ni ya kipuuzi na yanalenga kuwakatisha tamaa wananchi juu ya kazi inayofanywa na CHADEMA ya kuunganisha nguvu ya umma wa Watanzania dhidi ya udhaifu wa rais na uzembe wa Bunge linalohodhiwa na CCM katika mchakato wa Katiba mpya,” alisema.
Aliongeza kuwa CCM inalenga kurudisha nyuma Watanzania kwenye uamuzi unaosubiliwa kwa hamu.
Mnyika aliongeza kuwa CCM ilikataa kuandika Katiba mpya mbali ya Watanzania kuidai kwa nyakati tofauti na kuzimwa mpaka CHADEMA iliposhinikiza kupitia wabunge wake kutoka bungeni.
Kwamba baada ya kuandaa maandamano ndipo rais akakubali mchakato wa Katiba mpya uanze.
“CCM haikuwa na sera ya kuanzisha mchakato wa Katiba mpya, haina uhalali wa kimaadili wa kuinyooshea kidole CHADEMA iliyokuwa na sera ya Katiba mpya kwa madai ya kutumwa na mataifa ya nje kukwamisha mchakato huo,” alisema.
Mnyika alisema kuwa CCM imetoa msimamo na ufafanuzi wa maoni ya kupinga mazuri kwenye rasimu ya Katiba mpya. Kwamba inashangaza badala ya kuboresha mchakato wa kupata Katiba mpya yenyewe inataka kuuchakachua.
“Baada ya kushindwa kufanya hivyo kupitia mabaraza ya Katiba yaliyosimamiwa na Tume ya Marekebisho ya Katiba na mabaraza ya wazi yalioendeshwa na CHADEMA mengine kwa helikopta na mengine bila helikopta katika maeneo mbalimbali nchini, imeanza kuhadaa watu.
“Mbinu iliyobaki sasa kwao ni kuichakachua kwenye Bunge Maalumu la Katiba kwa kupenyeza watu wake kupitia kumpa rais mamlaka makubwa kwenye kuteua wajumbe 166 na pia kufanya uamuzi upite kwa wingi wa kura,” alisema.

No comments:

Post a Comment